Advertisements

Sunday, February 18, 2018

DEREVA, KONDAKTA WASIMULIA TUKIO LA MWANAFUNZI WA NIT KUPIGWA NA RISASI


By Mwandishi Wetu, Mwananchi mwananchipapers@mwananchi.co.tz

Dereva na kondakta wa daladala alilopanda mwanafunzi wa Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), Akwilina Akwiline aliyeuawa juzi kwa kupigwa risasi na polisi wamesimulia mkasa ulivyokuwa.

Akwilina alikuwa mwanafunzi wa mwaka wa kwanza wa Shahada ya Ununuzi na Ugavi (Procurement and Logistics) katika chuo hicho, lakini maisha yake yalikatishwa juzi akiwa ndani ya basi la daladala.

Tukio hilo lilitokea wakati polisi wakiwatawanya wanachama wa Chadema wakiongozwa na mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe waliokuwa wakielekea katika ofisi ya msimamizi wa uchaguzi Jimbo la Kinondoni, Aaron Kagurumjuli kudai hati za viapo vya mawakala wao.

Jana, Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa alikiri kuwapo kwa kifo cha mtu mmoja aliyepigwa risasi na askari wakati wakizuia maandamano hayo. Wakizungumza na Mwananchi, kondakta na dereva wa daladala alilokuwa amepanda mwanafunzi huyo akitokea katika chuo hicho eneo la Mabibo kwenda Makumbusho walisema alipigwa risasi wakiwa Mkwajuni, Kinondoni baada ya kuwakuta wafuasi wa Chadema wakiandamana.

No comments: