Advertisements

Tuesday, February 27, 2018

MO Dewji aahidi kuongeza idadi ya wanafunzi wanaopata ufadhili wa taasisi yake

 Taasisi ya Mo Dewji imetangaza orodha ya wanafunzi 22 wa elimu ya juu waliopata ufadhili kutoka katika taasisi hiyo kwa mwaka wa masomo 2017/2018 kupitia mpango wa Mo Scholars. Wanafunzi hao ni Neema Charles, Winfrida Mrope, Henritha Rwegasira, Monica Ubushimbali, Suzana Mkindi, Hamisa Selemani, Beatrice Shupa, Phoebe Mwankemwa, Amon Abraham, Venance Makambe na Amos Ntandu. Wengine ni Benjamin Mkondya, Ally Mashaka, Amuniri Sebarua, Iddi Mbilinyi, Samwel Ponda, Eram Temu, Busumilo Tumaini, Cosmadeus Mayunga, Amos Kashinje, Kelvin Ernest na Barnaba Barnaba ambao wote ni wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM). Akizungumza kuhusu ufadhili huo, Mwanzilishi wa Taasisi ya Mo Dewji, Mohammed Dewji aliwapongeza washindi kwa kufanikiwa kupata ufadhili huo, lakini akiwataka kujituma ili waweze kufikia malengo waliyojiwekea katika maisha yao.

Mohammed Dewji akizungumza na wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambao wanafadhiliwa na Taasisi ya Mo Dewji (hawapo kwenye picha) katika hafla ya kutangaza washindi wa mpango wa ufadhili kwa wanafunzi wa elimu ya juu (Mo Scholars). Picha zote na Rabi Hume.

“Mmepata ufadhili huu muutumie vizuri, wapo wengi ambao walituma maombi lakini nyie mmefanikiwa kupata ufadhili. Msome kwa bidii na baadae mpate kazi nzuri ambazo zitawasaidia kupata kipato na kusaidia ukuaji wa uchumi wa nchi,” alisema Dewji. Dewji alisema aliamua kuanza kutoa ufadhili kwa wanafunzi wa elimu ya juu ili kuunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli ya kuhakikisha kila mtoto anapata elimu.
Mohammed Dewji akizungumza na wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambao wanafadhiliwa na Taasisi ya Mo Dewji katika hafla ya kutangaza washindi wa mpango wa ufadhili kwa wanafunzi wa elimu ya juu (Mo Scholars).

Aliongeza kuwa, dhamira yake ni kuona Watanzania wengi wananufaika na mpango huo na amejipanga kuhakikisha kuwa idadi ya wanufaika wa mpango wa ufadhili unaotolewa na taasisi yake unaongezeka kila mwaka. “Kasi yetu bado ni ndogo sana kulinganisha na ninavyotaka. Wakati tunaanza kutoa ufadhili tuliamua kuanza na wanafunzi 10 lakini mimi nataka tuwape ufadhili Watanzania wengi ikiwezekana tufike hata 100. Kwangu ni jambo jema sana kusaidia Watanzania wenzangu kwa sababu nimezaliwa hapa na nitazikwa hapa sina pengine pa kwenda,” alisema Dewji.
Mmoja wa wanafunzi ambaye kabla ya kupata ufadhili aliweka tangazo kwenye mtandao wa kijamii kwamba anauza figo yake, Amos Ntandu akielezea histori ya maisha yake hadi alilopata ufadhili wa Taasisi ya Mo Dewji.

Nae mmoja wa wanafunzi ambaye kabla ya kupata ufadhili aliweka tangazo kwenye mtandao wa kijamii kwamba anauza figo yake, Amos Ntandu aliishukuru Taasisi ya Mo Dewji kwa ufadhili ambao imewapatia kwani baadhi yao waliokuwa wamepoteza matumaini ya kuendelea na masomo, lakini pia kuomba uongozi wa taasisi kuendelea kutoa ufadhili kwa Watanzania ili wapate elimu. “Mimi nilikuwa tayari kuweka maisha yangu hatarini kwa kutangaza kuuza figo langu, lakini ufadhili huu mliotupatia umebadili maisha yetu. Idadi ya wanafunzi wanaokosa mkopo ni kubwa hivyo nawaomba muwe na moyo wa kuendelea kuwasaidia ili na wao wafikie ndoto zao,” alisema Ntandu.
Mkuu wa Taasisi ya Mo Dewji, Barbara Gonzalez akizungumza kuhusu mpango wa ufadhili kwa wanafunzi wa elimu ya juu (Mo Scholars).

Pamoja na kutangaza washindi hao, pia taasisi hiyo ilitoa zawadi ya kompyuta mpakato (laptop) kwa wanafunzi wa mwaka wa masomo 2016/2017 ambao inawafadhili waliofanya vizuri katika masomo yao kwa mwaka wa kwanza chuoni. Kwa sasa idadi ya wanafunzi ambao wanapata ufadhili kutoka Taasisi ya Mo Dewji imefikia 30, ambapo kati yao wanafunzi 7 ni wa mwaka wa masomo 2016/2017 na wanafunzi 22 mwaka wa masomo 2017/2018.
 Baadhi ya wanufaika wa mpango wa ufadhili kwa wanafunzi wa elimu ya juu (Mo Scholars).

 Mwanzilishi wa Taasisi ya Mo Dewji, Mohammed Dewji akikabidhi zawadi kwa baadhi ya wanafunzi wa elimu ya juu waliopata ufadhili kutoka katika taasisi hiyo kwa mwaka wa masomo 2017/2018 kupitia mpango wa Mo Scholars.
 
 Mwanzilishi wa Taasisi ya Mo Dewji, Mohammed Dewji akikabidhi zawadi ya laptop kwa baadhi ya wanafunzi wa elimu ya juu waliopata ufadhili kutoka katika taasisi hiyo kwa mwaka wa masomo 2016/2017 kupitia mpango wa Mo Scholars.

No comments: