Advertisements

Friday, March 2, 2018

JAJI MKUU WA GAMBIA AMTEMBELEA MWANASHERIA MKUU

Mwanasheria Mkuu wa Serikali Dk. Adelardus Kilangi akibadilishana mawazo na Jaji Mkuu wa Gambia Mhe. Hassan Bubacar Jallow, leo Ofisi kwa Mwanasheria Mkuu. Jaji Mkuu yupo hapa nchini kwa ziara ya kikazi yenye madhumuni ya kujifunza uboreshaji wa sekta ya sheria na utoaji haki hapa nchini. Baadhi ya mambo waliyobadilishana mawazo ni pamoja na uwezeshwaji kwa wanasheria wa Serikali na watumishi wengine katika sekta ya sheria kimaslahi na kimafunzo.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali akiagana na Mgeni wake Jaji Mkuu wa Gambia Mhe. Hassan Bubacar Jallow mara baada ya mazungumzo yao. Jaji Mkuu Jallow alisoma sheria Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (1970-1973) na pia amewaji kuwa Mwendesha Mashtaka wa iliyokuwa Mahakama ya Kimataifa ya Mauaji ya Kimbari ya Rwanda ( ICTR) (2003-2015).
Mwanasheria Mkuu Dk. Adelardus Kilangi akisalimiana na Balozi wa Tanzania nchini Sweden, Mhe Wilbroad Slaa walipokutana nje ya Jengo ambalo lina Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki . Mwanasheria Mkuu alikuwa akimsubiri kumpokea mgeni wake Jaji Mkuu wa Gambia Mhe. Hassan Jallow ambaye yupo nchini kwa ziara ya kikazi.
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
OFISI YA MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI

Anwani ya Simu “LEGAL” Dar es Salaam
Simu: +255-2118178/82                           20 Barabara ya Kivukoni                            
Fax No: +255-2113236 11492 Dar es Salaam
S.L.P 9050
       Tanzania.

JAJI MKUU WA GAMBIA AMTEMBELEA MWANASHERIA MKUU.
Na Mwandishi Maalum
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Dk. Adelardus Kilangi, leo (Alhamisi) amekutana na kuwa na mazungumzo na  Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Gambia Mhe.   Hassan Bubacar Jallow.
Jaji Mkuu wa Gambia, yupo hapa  nchini kwa  ziara ya kikazi    ya kujifunza na kujipatia uzoefu kuhusu mfumo wa utoaji haki  hapa nchini pamoja na maboresho mbalimbali  yakiwamo ya maslahi ya  watumishi yanayoendelea katika   Mahakama ya Tanzania na Taasisi  nyingine za  Sheria na  utoaji  haki.
Jaji Mkuu  Jallow amemueleza Mwanasheria Mkuu wa Serikali  Dk. Adelardus Kilangi kwamba, Gambia, baada ya mabadiliko ya Serikali yaliyofanyika mwaka jana nchini humo, ipo katika mchakato wa kuifanyia  mabadiliko na maboresho   sekta ya sheria nchini humo.
"Nimekuja kwa ziara ya kikazi kwa madhumuni ya  kujifunza  kutoka Tanzania namna gani na sisi (Gambia) tutakavyoweza kuboresha na kuifanyia mageuzi makubwa  sekta  yetu ya Sheria na mfumo mzima wa  utoaji wa haki".
Akabainisha kwamba, anafahamu, namna gani  Mahakama ya Tanzania imeweza,  kwa kushirikiana na   Serikali na  Wadau wa  Maendeleleo  hususani Benki ya Dunia  kufanya  mageuzi  na maboresha makubwa  katika mfumo wa utoaji haki.
"Ningependa kujifunza mbinu  ambazo Mahakama iliweza kuzitumia kuivutia Benki ya Dunia hata ikawa mdau wake muhimu katika  maboresha yanayoendelea hivi sasa. Na pia  nitumie fursa hii kubadilishana mawazo  pamona na wewe Mwanasheria Mkuu na  nikupongeze kwa  kuteuliwa kwako." akaeleza Jaji  Mkuu.
Pamoja na  kumtembelea   Mwanasheria Mkuu wa Serikali,  miongoni mwa    sehemu anazotarajiwa kutembelea kama sehemu ya kujipatia  uzoefu ni  Chuo cha  Uongozi wa Mahakama   Lushoto  (IJA).
" Ninakwenda pia Lushoto na  pamoja na mambo mengine ninataka  kuangalia uwezekano wa kuanzisha ushirikiano na  Chuo  hicho kwa kuwaleta watu wetu na pia kuwaalika  wataalamu kutoka  Chuo hicho kuja  nchini Gambia". amesisiza  Jaji Mkuu Jallow.
Kwa upande wake Mwanasheria Mkuu  ameunga mkono wazo la  Jaji Mkuu la kuanzisha uhusiano wa karibu na Chuo cha Uongozi wa  Mahakama kwa kile alichosema ni  moja ya Taasisi muhimu sana katika utoaji wa mafunzo.  
Akabainisha kuwa  hata Ofisi ya Mwanasheria Mkuu nayo inaangalia namna bora zaidi ya kukitumia  Chuo  katika kuwajenga uwezo na kuwapiga msasa  wafanyakazi wa Ofisi  yake.
Kuhusu maslahi na mazingira bora ya kufanyia kazi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali alisema ni eneo ambalo  linatakiwa kuangaliwa na kufanyiwa kazi.
"Maslahi ya wafanyakazi katika sekta ya  utoaji  haki ni muhimu sana, na hasa ukizingatia  kwa mfano katika  Ofisi yangu , wanafanya kazi kubwa, nzuri, kwa uadilifu na uzalendo wa hali ya juu sana. Kuna haja na umuhimu wakuangalia pia maslahi yao ili  siyo tu kuwapa motisha ya kutekeleza majukumu yao  vizuri zaidi lakini pia  kuwafanya wapende kubaki na kufanya  kazi serikalini. akaeleza Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Dk. Kilangi amemshukuru   Jaji Mkuu wa Gambia kwa kuitembelea Ofisi ya Mwanasheria Mkuu na kubadilishana   uzoefu  na kwamba wakati wowote Ofisi hiyo itakuwa tayari kushirikiana na  Gambia  kupitia  sekta ya   sheria na utoaji haki.
Jaji Mkuu Hassan Jallow   pia si mgeni sana kwa Tanzania  kwa sababu  shahada yake ya kwanza ya  Sheria aliipata katika Chuo Kikuu cha Dar Es s Salaam ( 1973)  na pia amewahi  kuwa Mwendesha Mashtaka wa    iliyokuwa Mahakama ya Kimataifa ya  Mauaji ya Kimbari ya Rwanda ( ICTR) (2003-2015)  




No comments: