Advertisements

Monday, May 7, 2018

Biteko apiga marufuku bei holela madini ya ujenzi

 Mkuu wa Wilaya ya  Tanga (kulia) Thobias Mwilapwa akielezea Sekta ya Madini katika Wilaya yake kwa watendaji mbalimbali kutoka Wizara ya Madini, Vyombo vya Ulinzi na Usalama na Vyombo vya Habari (hawapo pichani) kwenye ziara ya Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko.
 Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (katikati mbele) akiendelea na ziara katika eneo linalotumika kwa ajili ya uchimbaji wa madini ya ujenzi aina ya kokoto  lililopo katika eneo la Amboni Wilayani Tanga mkoani Tanga.
 Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (kushoto) akizungumza na mponda kokoto, Helena  Joackim (aliyekaa chini) kwenye machimbo ya kokoto yanayomilikiwa na Swalehe  Khama yaliyopo katika eneo la Amboni Wilayani  Tanga mkoani Tanga.
 Mchimbaji mdogo wa madini ya kokoto Swalehe Khama akifafanua jambo kwa Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (hayupo pichani) kwenye ziara hiyo.
 Mponda kokoto, Husna Bakari akiwasilisha kero yake kwa Naibu Waziri wa Madini Doto Biteko (hayupo pichani) katika ziara hiyo.
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko akifafanua jambo kwa wachimbaji madini ya ujenzi aina ya kokoto kwenye ziara hiyo.

Na Greyson Mwase, Tanga
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko amepiga marufuku tabia ya wachimbaji wa madini ya ujenzi ya kushusha bei ya madini hayo kwa ajili ya kuuza kwa wingi, badala ya kufuata bei elekezi iliyowekwa na Serikali  huku wakiwalipa  vibarua kiasi kidogo cha fedha kisichoendana na kazi ngumu wanazofanya.
Naibu Waziri Biteko ameyasema hayo  mapema leo alipofanya ziara katika machimbo ya madini ya ujenzi aina ya kokoto katika eneo la Amboni mkoani Tanga lengo likiwa ni kukagua shughuli za uchimbaji wa madini pamoja na kuzungumza na wananchi.
Biteko alisema kumekuwepo na tabia ya baadhi ya wamiliki wa leseni kuuza madini aina ya kokoto kwa bei  ya chini na kupata faida huku wakiwalipa kiasi kidogo vibarua wanaofanya kazi ngumu ya kuponda kokoto kwa kutumia vifaa duni.
Akijibu kero mbalimbali zilizowasilishwa na wachimbaji madini ya kokoto Biteko alisema kuwa nia ya Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na  Rais Dkt. John Pombe Magufuli ni hukakikisha kuwa rasilimali za madini zinawanufaisha watanzania na kuwataka kuunda vikundi ili kurahisisha upatikanaji wa vifaa na ruzuku kutoka Serikalini.
Alisema Wizara ya Madini kupitia Mradi wa Usimamizi  Endelevu wa Rasilimali Madini (SMMRP) imepanga mikakati ya kuwawezesha wachimbaji wadogo kupitia ruzuku na ununuzi wa vifaa vya uchimbaji ili waweze kufanya kazi katika mzaingira rafiki na kuwa na mchango mkubwa katika ukuaji wa  Sekta ya Madini.
Akielezea hatua zilizofanywa na Serikali katika kuimarisha sekta ya madini nchini alisema imeanza na kufanya marekebisho katika Sheria ya Madini na kanuni zake, kuondoa urasimu ikiwa ni pamoja na kupambana na rushwa.
Alisema pia Serikali imeanzisha Tume ya Madini itakayokuwa na jukumu la kusimamia shughuli zote za madini  ikiwa ni pamoja na  kusogeza huduma za utoaji wa leseni za madini.
Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Biteko aliwataka wachimbaji wa madini ya ujenzi kulinda rasilimali za madini kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama.
“Kumekuwepo na tabia ya baadhi wa wachimbaji madini kutorosha madini nje ya nchi na kukamatwa na vyombo vya ulinzi na usalama, na kama Serikali tumejipanga kuhakikisha tunalinda rasilimali za madini kwa nguvu zote,” alisisitiza Biteko.

Aidha katika hatua nyingine Biteko aliwataka wachimbaji wa madini kufuata sheria za madini pamoja na kanuni zake.

No comments: