Advertisements

Monday, January 21, 2019

CAG aanza kuhojiwa na kamati ya Bunge

Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali
By Habel Chidawali, Mwananchi hchidawali@mwananchi.co.tz

Dodoma. Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Mussa Assad leo asubuhi Januari 21, 2019 amefika mbele ya kamati ya Maadili, Haki na Madaraka ya Bunge kwa ajili ya kuhojiwa kuhusu kauli yake ya “udhaifu wa Bunge.”

CAG Assad aliyeteuliwa na Rais Jakaya Kikwete, Desemba Mosi mwaka 2014 ameitwa mbele ya kamati hiyo kujieleza kuhusu kauli aliyoitoa wakati alipokuwa akihojiwa na kituo cha televisheni cha idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa (UN) akiwa New York, Marekani alikokuwa akihudhuria mkutano.

Alitumia neno “udhaifu” wa Bunge alipokuwa akieleza sababu za kutofanyiwa kazi kwa ripoti zake ambazo zimekuwa zikibainisha ufisadi.

Mara baada ya kuingia katika ukumbi yanapofanyika mahojiano hayo saa 5:01 asubuhi, CAG aliyekuwa amebeba begi dogo jeusi, aliwasha kompyuta yake mpakato na kisha kuwasalimu wajumbe wa kamati hiyo.

Alifika katika viwanja vya Bunge saa 4:49 asubuhi akiwa peke yake bila wasaidizi, akateremka katika gari jeupe na kupita katika mashine za ukaguzi.

Katika mashine hizo Profesa Assad alivua viatu, koti, saa, miwani na kisha kuvaa tena vitu hivyo baada ya ukaguzi.

Huku ulinzi ukiwa umeimarishwa, baada ya ukaguzi Profesa Assad alikwenda kuketi eneo la mapumziko na msaidizi wa Spika, Said Yakubu alimpelekea kitabu cha kusaini.

Soma Zaidi: Dakika za mwisho joto la Ndugai, CAG

No comments: