Advertisements

Saturday, February 16, 2019

NAIBU WAZIRI NISHATI AWATAKA WANA-PWANI WACHANGAMKIE UMEME WA REA

 Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu (kulia), akiwakabidhi wauguzi wa Zahanati za Ngarambe na Tapika wilayani Rufiji, vifaa mbalimbali zikiwemo Taa zinazotumia umeme jua (solar) ili kuboresha utoaji huduma kwa wagonjwa. Naibu Waziri alikuwa katika ziara ya kazi wilayani humo Februari 15, 2019.
 Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu akizungumza na wananchi wa Kata ya Ngarambe, wilayani Rufiji, Mkoa wa Pwani, akiwa katika ziara ya kazi, Februari 15, 2019.
 Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu akisalimiana na watumishi mbalimbali wa Halamshauri ya Wilaya ya Rufiji, alipowasili katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, akiwa katika ziara ya kazi, Februari 15, 2019.
 Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu (kulia), akimsikiliza Mkuu wa Wilaya ya Rufiji, Juma Njwayo (mwenye fulana ya njano), alipomtembelea ofisini kwake, Februari 15, 2019 akiwa katika ziara ya kazi wilayani humo. Wengine pichani ni baadhi ya viongozi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo pamoja na wataalamu kutoka wizarani, REA na TANESCO.
Mmoja wa wakazi wa Ngarambe wilayani Rufiji, akitoa maoni yake kuhusu utekelezaji wa miradi ya umeme, mbele ya Naibu Waziri wa Nishati Subira Mgalu (hayupo pichani); wakati wa ziara yake wilayani humo, Februari 15, 2019.
 Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu (mwenye kilemba cha pinki) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya viongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji, maafisa kutoka wizarani, REA na TANESCO. Naibu Waziri alikuwa katika ziara ya kazi wilayani humo, Februari 15, 2019.

Na Veronica Simba – Pwani
Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu ametoa rai kwa wananchi wa Mkoa wa Pwani, hususan wanaopitiwa na Mradi wa Umeme Vijijini kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), kuchangamkia fursa hiyo kutokana na unafuu wa gharama zake.

Alitoa rai hiyo jana, Februari 15, 2019 kwa nyakati tofauti akiwa katika ziara ya kazi kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya umeme, kuwasha umeme na kuzungumza na wananchi katika wilaya za Rufiji na Kibiti.

Alisema, gharama za uunganishaji umeme wa REA kwa kila mwananchi ni shilingi 27,000 tu lakini pindi mradi huo utakapoisha muda wake, gharama za uunganishaji zitakuwa kubwa zaidi. 

Hivyo, aliwaasa wananchi kutumia fursa hiyo ipasavyo kwa kujitokeza kwa wingi kulipia ili waunganishiwe.Aidha, Naibu Waziri aliwataka wananchi walio katika maeneo ambayo miradi mbalimbali ya umeme ilikwishapita na hawakufikiwa, kutulia kwani iko miradi mingine itakayotekelezwa katika maeneo yao hususan mradi wa ujazilizi (Densification).

Akifafanua, alisema, hakuna mwananchi au eneo ambalo litaachwa pasipo kupelekewa huduma ya umeme; ndiyo maana serikali kupitia Wizara ya Nishati, inaendelea na utekelezaji wa miradi mbalimbali inayolenga kuyafikia maeneo yote na kuhakikisha wananchi wote wanapata umeme, zoezi linalofanyika hatua kwa hatua.

Vilevile, Naibu Waziri Mgalu aliutaja mradi mkubwa wa umeme wa maji ya mto Rufiji maarufu kama Stiegler’s, ambao tayari mkandarasi amekabidhiwa rasmi kuanza kuujenga; kuwa utakuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi wa Pwani ambao ndiyo mkoa unaoubeba mradi husika.

Akiwa wilayani Rufiji, aliwataka kuzitumia fursa zitakazotokana na utekelezaji wa mradi wa umeme wa Rufiji katika eneo lao kwa kuwa wabunifu ili kujiongezea kipato kupitia shughuli mbalimbali.“Mradi wa Stiegler’s utaanza na ni fursa kwenu wana-Rufiji. Rai yangu tujipange kutumia fursa hizo. Rufiji hii itakuwa nyingine.”

Akiwa katika Kata ya Ngarambe, Naibu Waziri alitoa taa zinazotumia nguvu ya jua (solar), kwa wauguzi wa Zahanati za Ngarambe na Tapika wilayani Rufiji, ili kusaidia utoaji huduma kwa wagonjwa, wakati wakisubiri kufikiwa na huduma ya umeme. Pia, alitoa msaada wa mashuka katika Zahanati hizo.
Kwa upande wao, viongozi mbalimbali wakiwemo Wakuu wa Wilaya za Kibiti na Rufiji, viongozi wa Halmashauri na Mbunge wa Kibiti, walipongeza jitihada ambazo zimekuwa zikifanywa na Serikali ya Awamu ya Tano, kupitia Wizara ya Nishati, katika kuhakikisha maeneo mbalimbali yanafikiwa na huduma ya umeme.

Waliomba jitihada hizo ziendelee kwa kasi ili kuyafikia maeneo yote hususan ya vijijini.Katika ziara hiyo, Naibu Waziri Mgalu aliambatana na viongozi na wataalamu mbalimbali kutoka wizarani, TANESCO na REA. Alitembelea vijiji vya Ngarambe, Azimio, Umwe, Kitembo na Mkupuka.

No comments: