Advertisements

Tuesday, April 16, 2024

KINANA AKEMEA UKABILA,ASHAURI VIONGOZI WACHAGULIWE KWA SIFA

MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Tanzania Bara Abdulrahman Kinana amekemea tabia ya baadhi ya wanaCCM na wananchi kuendekeza ukabila na kwamba ukabila ni jambo ambalo limepitwa na wakati na halina tija katika Taifa.

Amesisitiza hakuna faida yeyote ambayo inapatikana kwa kuendekeza ukabila zaidi ya kuleta mgawanyiko katika Taifa huku akifafanua Hayati Baba wa Taifa Mwalim Julius Nyerere alikemea ukabila.

“Kuwa na makabila ni jambo la kawaida ila ukabila ni jambo baya na kwamba kumuhukumu mtu kwa jambo ambalo hana uwezo nalo sio sahihi.”
Kinana aliyekuwa akizungumza na wanachama wa CCM Wilaya ya Rorya mkoani Mara moja ya malalamiko aliyopewa ni kuwepo kwa ukabila ka baadhi ya wanaCCM katika wilaya hiyo.

Hivyo wakati anazungumzia malalamiko hayo Makamu Mwenyekiti Kinana ameeleza Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere alitoka katika kabila dogo mkoani hapa lakini aliongoza nchi kwa miaka 24, alipendwa, aliheshimiwa, alithaminiwa si kwa sababu ya ukabila bali kutokana na kazi nzuri aliyoitenda kwa uadilifu na kuheshimika Tanzania, Afrika na duniani kote.

Amefafanua usimpe mtu nafasi ya uongozi kwa sababu ya kabila lake, dini au umbile kwani hayo ni mambo ya kizamani na yamepitwa na wakati.

“Tuangalie mtu anauwezo atafanya kazi atajituma na kujitolea, mnampima kwa vigezo sio kwamba huyu ni ndugu yangu.Mmoja katika kabila lako akipata cheo anakusaidia nini?

“Mgekuwa mnagawana mshahara sawa, kila mmoja anakuletea 300,000 kutoka kwenye mshahara wake kwa sababu ni kabila lako sawa... wekeni watu kwa uwezo wao na si kwa makabila yao." alieleza.

Aidha, alisema kuwa jambo ambalo Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere aliwaachia Watanzania ni umoja wa kitaifa, hivyo uendelezwe kwa maslahi ya nchi.



No comments: