Advertisements

Wednesday, April 24, 2024

WAKUU WA WILAYA TATU ZA MKOA WA KILIMANJARO WAKABIDHIWA MAGARI MAPYA


Na WILLIUM PAUL, MOSHI.
MKUU wa Mkoa wa Kilimanjaro, Nurdin Babu amekabidhi magari matatu kwa ajili ya wakuu wa wilaya za Rombo, Mwanga na Same ili kuongeza ufanisi wa utendaji na kuleta maendeleo ya mkoa yenye thamani ya zaidi ya milioni 200.

Akizungumza katika hafla fupi ya makabidhiano hayo nje ya viwanja wa ofisi za mkuu wa mkoa, Babu amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameanza kutekeleza maombi mbalimbali ya mkoa wa Kilimanjaro ya kuwapatia Wakuu wa wilaya vitendea kazi.

Babu alisema kuwa, Wabunge wamekuwa wakilalamika Bungeni kuhusiana na wakuu wa wilaya kukosa magari ambapo mkoa ulipanga kuhakikisha bajeti ya mwaka wa fedha 2023/24 mpaka ifikapo mwezi Juni mwaka huu wawe wameshanunua magari matatu ya wakuu wa wilaya.
Mkuu huyo wa Mkoa alisema kuwa, magari hayo yatatumika kwa ajili ya shughuli za kiserikali na kuwataka kwenda kuyatunza magari hayo kwani yamenunuliwa kwa gharama.

Aidha Babu amewataka Wakuu wa wilaya kuwaachia Madereva wafanye kazi zao kwani ndio waliyosomea kuendesha gari na kuachana na kumwambia kuvunja sheria ili kuwahi kule unapoenda ili kuepuka ajali zisizo na ulazima.

Kwa upande wake, Mkuu wa wilaya ya Rombo, Raymond Mangwala alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwajali wasaidizi wake na kuwapa vitendea kazi na kuahidi kutumia gari hilo kufanya kazi iliyokusudiwa ikiwemo kuhakikisha miradi inaenda kukamilika.

Naye mkuu wa wilaya ya Same, Kasilda Mgeni alisema kupatikana kwa vitendea kazi kutachangia kuwafikia wananchi na kutatua kero zao .

No comments: