Wednesday, June 12, 2013

SERIKALI YA MAPINDUZI ZANZIBAR HOTUBA YA WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS – FEDHA, UCHUMI NA MIPANGO YA MAENDELEO

MHESHIMIWA OMAR YUSSUF MZEE

KUHUSU MPANGO WA MAENDELEO NA MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA SERIKALI KWA MWAKA WA FEDHA 2013/14 KATIKA BARAZA LA WAWAKILISHI


UTANGULIZI
1. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja kuwa Baraza lako tukufu likae kama Kamati maalum ya kujadili na hatimae kuidhinisha mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mwaka 2013/14. Ombi hili linalenga kutimiza matakwa ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, kama ilivyorekebishwa. Kama ilivyo desturi, sambamba na Hotuba hii, naomba pia kuwasilisha Mapitio ya Hali ya Uchumi mwaka 2012 na Utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo na Bajeti kwa mwaka 2012/13 kama yanavyoonekana katika Kitabu cha Kwanza. Aidha, katika Kitabu cha Pili nawasilisha Mwelekeo wa Hali ya Uchumi na Mpango wa Maendeleo kwa mwaka 2013/14 na mwisho ni rasimu ya Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka 2013/14. Naomba maelezo hayo nayo yawekwe katika kumbukumbu za Baraza.
2. Mheshimiwa Spika, tumekutana tena hapa kuzungumzia Mipango muhimu ya maendeleo ya nchi yetu na watu wake, Wazanzibari. Naomba kumshukuru Mwenyezi Mungu Muumba kwa kutubariki uwezo huu wa kujumuika tena leo hii. Namuomba atujaalie hekima katika kukiendesha kikao hiki muhimu na tumalize kikao tukiwa tumewatumikia vyema, kwa busara na kwa ukweli Wananchi wenzetu tunaowawakilisha.
3. Mheshimiwa Spika, tumeshuhudia kipindi chengine cha juhudi kubwa kwa Mheshimiwa Rais wetu na wasaidizi wake katika kutuletea maendeleo. Tumeshuhudia pia kuimarika kwa amani na utulivu nchini petu, pamoja na matukio machache yaliyoashiria kuharibu utulivu wetu. Hatua za haraka za kuyadhibiti matukio hayo zilizochukuliwa na Serikali yetu zimeweza kurejesha hali ya nchi kuwa ya shwari. Kifungu cha 26 cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 kinatamka kwamba Rais ndie “Mkuu wa Nchi ya Zanzibar, Kiongozi Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi, na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi”. Hatua za maendeleo na utulivu tunazozishuhudia, kwa hivyo, ni matokeo ya uongozi huo wa Mheshimiwa Rais. Naomba basi nichukue fursa hii kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Dr. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa uongozi wake uliojaa hekima, busara na kuona mbali. Kwangu binafsi, namshukuru pia kwa kuendelea kuniamini na kunipa jukumu la kuiongoza Ofisi yake hii muhimu inayoshughulikia Fedha, Uchumi na Mipango ya Maendeleo.

4. Mheshimiwa Spika, nimesema kuwa tulikuwa na matukio machache ya kuharibu utulivu katika kipindi hiki. Miongoni mwa matukio hayo ya kusikitisha na kutia huzuni ni yale ya kushambuliwa na kuathiriwa kwa viongozi tofauti wa dini na Sheha. Kwanza, Sheikh Fadhil Soraga, aliemwagiwa tindikali mapema ya asubuhi ya tarehe 6 Novemba 2012. Likafuatia tukio la kupigwa risasi kwa Mchungaji Amros Mkenda asubuhi ya tarehe 25 Disemba mwaka 2012. Mwenyezi Mungu muumba alituonesha uwezo wake, akamlinda na kwa rehema zake bado Padri Mkenda yuko hai. Tukio kubwa zaidi ni lile lililotokea asubuhi ya tarehe 17 Februari mwaka huu kwa kupigwa risasi na kuuwawa kwa Mchungaji Everest Mushi. Tukio la karibuni kabisa ni la kumwagiwa tindikali Sheha wa Shehia ya Tomondo, Bw. Mohammed Said Kidevu lililotokea tarehe 23 Mei mwaka huu.

5. Mheshimiwa Spika, kwa vyovyote vile matukio yote hayo yalilenga kuwadhuru kwa kiasi kikubwa viongozi wetu hao wa dini zetu kubwa na shehia; yalilenga kuleta fitna kubwa katika jamii yetu kwa kugombanisha waumini wa dini tofauti; na hatimae yalilenga kuleta fujo nchini na kuondoa utulivu uliozoeleka. Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuepusha na shari zote za matukio hayo na kutuepusha na makusudio ya wahusika. Nawashukuru na kuwapongeza sana wananchi wote, na hasa ndugu, jamaa na wafuasi wa karibu wa viongozi wote hao. Nawashukuru na kuwapongeza kwa utulivu wao na imani yao kwa Serikali katika kipindi chote cha majaribu.

6. Mheshimiwa Spika, wakati Serikali bado inaendelea na jitihada za kuwapeleka wahusika katika mikono ya sheria, tuendelee wote kunasihiana katika kudumisha utulivu tuliouonesha wakati wachache wetu walipotutia majaribuni. Kwa Sheikh Soraga, Mchungaji Mkenda na Sheha Mohammed Kidevu tunawaombea kwa Muumba muweza awaponyeshe haraka na kuwaondolea khofu ya matukio yao. Kwa Mchungaji Mushi tunamuombea malazi mema na kwa ndugu, marafiki na waumini wake tunawaombea subira zaidi. Hakika Mwenyezi Mungu atalipa kwao kwa subira yao na hataacha kuwalipa waliotenda uovu huu kwa dhulma yao kwa viongozi hao wote wasio na hatia.

7. Mheshimiwa Spika, naamini uongozi mzuri wa Mheshimiwa Rais umesaidiwa pia na utendaji na ushauri anaoupata kutoka kwa wasaidizi wake wakuu, Mheshimiwa Maalim Seif Sharif Hamad, Makamo wa Kwanza wa Rais na Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, Makamo wa Pili wa Rais. Naomba nitumie fursa hii kuwapongeza kwa dhati Makamo hao wa Rais kwa uongozi wao.
8. Mheshimiwa Spika, kipindi kama hiki mwaka jana, wananchi wenzetu wa Jimbo la Bububu hawakuwa na Mwakilishi katika Baraza hili kufuatia kifo cha aliekuwa Mwakilishi wao, Salum Amour Mtondoo. Kupitia uchaguzi mdogo, tayari pengo hilo limezibwa, na limezibwa vyema. Nawapongeza sana wananchi wa Jimbo la Bububu kwa kuchagua Muwakilishi wao. Na mimi nachukua fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Hussein Ibrahim Makungu (Bhaa) kwa kuchaguliwa kuliwakilisha Jimbo hilo humu Barazani. Naamini kwa utendaji aliouonesha Mheshimiwa Hussein tokea kuchaguliwa kwake, wananchi hao wameridhika na chaguo lao. Namtakia kila la kheri Mheshimiwa Hussein katika kuwatumikia na kuwawakilisha vyema wananchi wa Jimbo la Bububu.

9. Mheshimiwa Spika, baada ya utangulizi huo, naomba sasa niwasilishe Mapitio ya Hali ya Uchumi kwa mwaka 2012 na Utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo na Bajeti kwa mwaka 2012/13 hadi kufikia Machi 2013.


MAPITIO YA UCHUMI NA UTEKELEZAJI WA MPANGO WA MAENDELEO NA BAJETI KWA MWAKA 2012/13

Hali ya Uchumi Duniani na Kikanda


10. Mheshimiwa Spika, uchumi wa dunia unaendelea kukua taratibu kutokana na matatizo ya kiuchumi na fedha yaliozikumba nchi za Ulaya. Uchumi wa dunia mwaka 2012 umekuwa kwa wastani wa asilimia 3.2 ikilinganishwa na ukuaji wa wastani wa asilimia 4.0 mwaka 2011. Kanda zote nazo zimeshuhudia kasi ndogo ya kukua kwa uchumi wake kwa mwaka 2012, kama hivi ifuatavyo:
(i) Uchumi wa nchi zilizoendelea umekuwa kwa wastani wa asilimia 1.2 kutoka asilimia 1.6 mwaka 2011;
(ii) Uchumi wa nchi zinazoendelea na zinazoibuka kiuchumi umekuwa kwa wastani wa asilimia 5.1 kutoka asilimia 6.4 mwaka 2011;
(iii) Uchumi wa nchi zilizo Kusini mwa Jangwa la Sahara umekua kwa wastani wa asilimia 4.8 kutoka asilimia 5.3 mwaka 2011; na
(iv) Katika Afrika ya Mashariki ukuaji ulifikia wastani wa asilimia 4.5 kutoka asilima 5.9 mwaka 2011.

MFUMKO WA BEI WA DUNIA, AFRIKA NA KANDA


11. Mheshimiwa Spika, tofauti na ukuaji wa uchumi, mwenendo wa utulivu wa bei za bidhaa na huduma Duniani na katika Kanda zote umekuwa wa kuridhisha kwa mwaka 2012, kwa kupungua kasi ya wastani wa mfumko wa bei, kama inavyobainishwa hapa chini:
(i) Kasi ya mfumko wa bei duniani imepungua kutoka asilimia 3.8 mwaka 2011 kufikia 3.3 mwaka 2012;
(ii) Kwa nchi zilizoendelea ilishuka na kufikia asilimia 1.3 mwaka 2012 kutoka asilimia 1.4 mwaka 2011;
(iii) Kwa nchi zinazoibuka kiuchumi na zinazoendelea ilishuka kutoka asilimia 7.2 mwaka 2011 na kufikia asilimia 5.9 mwaka 2012; na
(iv) Nchi zilizoko Kusini mwa Jangwa la Sahara mfumko wa bei ulipungua hadi asilimia 9.1 mwaka 2012 kutoka asilimia 9.3 mwaka 2011.
(v) Kwa nchi za Afrika ya Mashariki, ulishuka kutoka asilimia 13.2 mwaka 2011 hadi wastani wa asilimia 11.5 mwaka 2012.

MWENENDO WA UCHUMI WA ZANZIBAR


Pato la Taifa


12. Mheshimiwa Spika, uchumi wa Zanzibar umeonesha mwenendo mzuri tofauti na ule wa dunia na Kanda. Ukuaji halisi wa uchumi umeimarika zaidi mwaka 2012 na kufikia asilimia 7.0 ikilinganishwa na asilimia 6.7 wa mwaka 2011. Pato la Taifa kwa bei za miaka husika limefikia jumla ya TZS 1,354 bilioni mwaka 2012 ikilinganishwa na TZS 1,198 bilioni kwa mwaka 2011.
Miongoni mwa mambo yaliyochangia ukuaji huo ni pamoja na haya yafuatayo:
(i) Ongezeko la ukuzaji rasilimali kwa asilimia 41.3 kutoka thamani ya TZS 183.20 bilioni mwaka 2011 mpaka TZS 258.87 bilioni. Ongezeko hili limesababishwa na uwekezaji mkubwa katika maeneo ya ujenzi wa nyumba za kuishi na biashara, zana za usafirishaji na ujenzi vijijini.
(ii) Ukuaji mzuri wa sekta ya viwanda ambayo imekua kwa asilimia 9.2 mwaka 2012 kutoka asilimia 5.8 mwaka 2011.
(iii) Kuimarika kwa sekta ya huduma ambayo imekuwa kwa asilimia 8.7 ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 8.6 mwaka 2011.


PATO LA MTU BINAFSI

13. Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia kiasi hicho cha Pato la Taifa na idadi ya watu milioni moja na laki tatu wa Zanzibar, kwa wastani, Pato la kila mtu limeongezeka mwaka 2012 na kufikia TZS 1,003,000/= (USD 638) kwa mwaka kutoka TZS 960,000/= (USD 617) mwaka 2011, sawa na ongezeko la asilimia 4.5.

UKUAJI NA MICHANGO YA KISEKTA KATIKA PATO LA TAIFA
14. Mheshimiwa Spika, kiujumla, sekta zote zimeonesha ukuaji katika mwaka 2012 ingawa kwa viwango tofauti na kwa kasi tofauti ikilinganishwa na mwaka 2011. Viwango hivyo vya ukuaji kwa mwaka 2012 ni kama hivi ifuatavyo:
(i) Sekta ya Huduma ilikuwa kwa asilimia 8.7 ikionesha kuimarika kidogo kutoka asilimia 8.6 mwaka 2011;
(ii) Sekta ya Kilimo ilikuwa kwa asilimia 1.3 na hivyo kasi yake imeshuka kutoka asilimia 2.7 ya mwaka 2011; na
(iii) Ukuaji wa Sekta ya Viwanda ulifikia asilimia 9.2 kutoka asilimia 5.8 ya mwaka 2011, ukichangiwa zaidi na kuimarika kwa shughuli za ujenzi wa nyumba za kuishi na za biashara.
15. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa mchango ya Sekta hizi katika Pato la Taifa, mchango wa Sekta ya Huduma umeimarika zaidi na kufikia asilimia 45.3 kutoka asilimia 44.0 mwaka 2011. Matokeo ya kuimarika huko ni kushusha michango ya sekta nyengine. Sekta ya Kilimo imechangia asilimia 30.2 kutoka asilimia 32.2 mwaka 2011 wakati sekta ya Viwanda imechangia asilimia 11.7 mwaka 2012 kutoka mchango wa asilimia 12.0 mwaka 2011.

MFUMKO WA BEI ZANZIBAR


16. Mheshimiwa Spika, mwenendo wa bei Zanzibar umeshabihiana na ule wa dunia na Kanda kwa mwaka 2012. Kasi ya mfumko wa bei ilipungua hadi kufikia asilimia 9.4 na hivyo kuwa juu kidogo kuliko matarajio ya kufikia asilimia 8.7. Hata hivyo, bado kasi hii ni chini ya kiwango cha wastani wa nchi za Afrika ya Mashariki. Kufikiwa kiwango cha tarakimu moja ni hatua nzuri ikilinganishwa na kiwango cha Mfumko wa Bei cha asilimia 14.7 kwa mwaka 2011. Kwa kuwa sehemu kubwa ya Mfumko wa Bei Zanzibar inachangiwa na uingizaji bidhaa, kasi nafuu ya Mfumko wa Bei imechangiwa na utulivu wa bei katika nchi tunazofanya nazo biashara, mwenendo mzuri wa bei za chakula na mafuta ya Petroli katika soko la dunia na utulivu wa thamani ya sarafu ya Tanzania kulinganisha na Dola ya Marekani.


SEKTA YA NJE

17. Mheshimiwa Spika, Mizania ya Biashara inaonesha kuwa nakisi katika urari wa biashara imeendelea kupanuka zaidi mwaka 2012 na kufikia TZS 203.9 bilioni kutoka nakisi ya TZS 102.9 bilioni ya mwaka 2011. Hali hii imechangiwa na kasi kubwa ya kukua kwa uingizaji ikilinganishwa na ukuaji wa usafirishaji bidhaa nje. Katika mwaka huo, uingizaji ulikuwa kwa asilimia 65.2 kutoka TZS 164.2 bilioni mwaka 2011 hadi TZS 271.3 bilioni mwaka 2012. Kwa upande mwengine, katika kipindi hicho usafirishaji ulikuwa kwa asilimia 10 tu kutoka TZS 61.3 bilioni hadi TZS 67.4 bilioni. Hali hii imetokana na kasi kubwa zaidi ya uingizaji wa vifaa vya chuma kama nondo, mashine na vifaa vya umeme.


UTEKELEZAJI WA BAJETI YA SERIKALI 2012/13

18. Mheshimiwa Spika, Baraza lako liliidhinisha Bajeti ya TZS 648.9 bilioni kwa mwaka wa fedha 2012/13, zikihusisha TZS 315.8 bilioni kutokana na mapato ya ndani yatokanayo na kodi, mapato yasiyo ya kodi na mikopo ya ndani. Kiasi kilichobakia cha TZS 333.1 bilioni ni kutokana na Washirika wa Maendeleo, ikiwemo kwa ajili ya Programu na Miradi na Misaada ya Kibajeti. Kwa upande wa matumizi, jumla ya TZS 307.8 bilioni ziliidhinishwa kwa kazi za kawaida na TZS 341.1 bilioni kwa ajili ya Programu na Miradi ya Maendeleo.

Mapato ya Ndani

19. Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2012/13 Serikali ilikadiria kukusanya mapato kutokana na vyanzo vya ndani ya TZS 294.13 bilioni sawa na asilimia 21.3 ya Pato la Taifa. Kati ya fedha hizo, jumla ya TZS 274.13 bilioni kutokana na vyanzo vya kodi na TZS 20.00 bilioni ni kutokana na vyanzo visivyokuwa vya kodi. Kati ya TZS 274.13 bilioni zilizotokana na kodi, Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) ilitarajiwa kukusanya kiasi cha TZS 146.00 bilioni. Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ilikadiriwa kukusanya TZS 106.73 bilioni na TZS 21.4 bilioni zilikadiriwa kukusanywa na Idara ya Mhasibu Mkuu wa Serikali kutokana na Kodi ya Mapato kwa wafanyakazi wa SMT waliopo Zanzibar.

20. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha miezi tisa (Julai 2012 hadi Machi mwaka 2013), Serikali ilikadiria kukusanya mapato ya ndani ya TZS 224.24 bilioni. Makusanyo halisi yalifikia TZS 201.24 bilioni sawa na asilimia 90 ya makadirio ya kipindi hicho. Kati ya makusanyo hayo, mapato kutokana na kodi yalifikia TZS 192.41 bilioni ambazo ni sawa na asilimia 91 ya makadirio wakati mapato yasiyokuwa ya kodi yalifikia TZS 8.83 bilioni sawa na asilimia 69 ya makadirio ya kipindi hicho. Yakilinganishwa na makusanyo halisi ya TZS 169.6 bilioni ya kipindi kama hicho mwaka uliopita (2011/12), kunajitokeza ukuaji wa mapato kwa TZS 31.6 bilioni sawa ongezeko la asilimia 18.7. Ukusanyaji mapato kitaasisi na kwa kulinganisha na kipindi kama hicho mwaka uliopita ni kama hivi ifuatavyo:

(i) Mamlaka ya Mapato Tanzania imekusanya jumla ya TZS 79.51 bilioni sawa na asilimia 99 ya makadirio. Ukusanyaji huu unamaanisha ukuaji wa mapato wa asilimia 18.5 kutoka TZS 67.1 bilioni;
(ii) Bodi ya Mapato Zanzibar imekusanya jumla ya TZS 109.48 bilioni sawa na asilimia 85 ya makadirio zikiwemo TZS 100.65 bilioni za mapato ya kodi sawa na asilimia 87 ya makadirio na jumla ya TZS 8.8 bilioni zilitokana na mapato ya mawizara. Mapato ya ZRB yamekuwa kwa asilimia 15.6 kutoka TZS 94.7 bilioni za mwaka jana;


(iii) Idara ya Mhasibu Mkuu wa Serikali imekusanya TZS 12.3 bilioni kutokana na Kodi ya Mapato (PAYE) kwa wafanyakazi wa SMT waliopo Zanzibar ambayo ni sawa na asilimia 78 ya makadirio ya kipindi hicho.

21. Mheshimiwa Spika, matarajio ya sasa ni kukusanya TZS 269.6 bilioni kutokana na mapato ya ndani hadi kufikia Juni 2013, sawa asilimia 91 ya makadirio ya mwaka huo. Kati ya mapato hayo, mapato ya kodi yanatarajiwa kufikia TZS 258.3 bilioni sawa na asilimia 94 ya makadirio, wakati mapato yasiyokuwa ya kodi yanatarajiwa kufikia TZS 11.33 bilioni, sawa na asilimia 57 ya makadirio. TRA inatarajiwa kukusanya jumla ya TZS 105.51 bilioni sawa na asilimia 99 ya makadirio. Kwa upande wake, ZRB inatarajiwa kukusanya jumla ya TZS 142.68 bilioni ambazo ni sawa na asilimia 86 ya makadirio na mapato ya PAYE ni TZS 21.4 bilioni sawa na asilimia 100 ya makadirio.

Mapato ya Nje


22. Mheshimiwa Spika, kati ya TZS 333.2 bilioni zilizotarajiwa kutoka kwa Washirika wa Maendeleo, jumla ya TZS 196.3 bilioni zimepatikana hadi kufikia Machi 2013, zikiwa ni pungufu ikilinganishwa na TZS 199.05 bilioni zilizopatikana hadi kufikia Machi 2012. Kati ya fedha hizo, TZS 175.8 bilioni ni ruzuku na mikopo kwa ajili ya Program/Miradi ya Maendeleo ambayo kimsingi haikuongezeka sana kutoka TZS 174.95 bilioni za mwaka 2011/12. Misaada ya kibajeti imeshuka hadi kufikia TZS 20.5 bilioni mwaka 2012/13 kutoka TZS 24.1 bilioni mwaka 2011/12 ambazo ni pungufu kwa asilimia 17.5. Hali hii imesababishwa na kukwama, kwa sababu za kiutendaji, kwa sehemu ya Zanzibar ya misaada inayopitia Serikali ya Jamhuri ya Muungano

DENI LA TAIFA

23. Mheshimiwa Spika, Deni la Taifa hadi mwezi wa Machi, 2013 limefikia TZS 252.3 bilioni sawa na asilimia 18.6 ya Pato la Taifa. Deni hili ni sawa na ongezeko la asilimia 20 kutoka deni la TZS 209.9 bilioni lililoripotiwa katika mwezi wa Machi 2012. Kati ya deni hilo, deni la ndani ni TZS 48.5 bilioni na lile la nje ni TZS 203.8 bilioni (USD 128.1 milioni). Kati ya deni la ndani, TZS 3.1 bilioni ni deni la Kiinua Mgongo baada ya kulipa jumla ya TZS 5.8 bilioni kwa wastaafu 617. Matarajio kwa kipindi cha miezi mitatu iliyobaki ni kuwa deni hili litafikia jumla ya TZS 3.5 bilioni kwa wafanyakazi watakaostaafu mwezi wa Aprili hadi Juni 2013.

MATUMIZI


24. Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza awali, Serikali ilitarajia kutumia jumla ya TZS 648.3 bilioni kwa mwaka unaoendelea wa fedha. Kwa miezi tisa, matumizi yote yalitarajiwa kufikia TZS 434.1 bilioni. Katika kipindi cha tathmini, matumizi halisi yamefikia jumla ya TZS 428.0 bilioni sawa na asilimia 98.6 ya makadirio ya miezi tisa au asilimia 66 ya makadirio ya mwaka. Kwa upande wa matumizi ya fedha za ndani, jumla ya TZS 231.67 bilioni sawa na asilimia 93 ya makadirio ya miezi tisa zimetumika. Kati ya matumizi hayo TZS 205.79 bilioni ni kwa kazi za kawaida sawa na asilimia 97 ya makadirio ya TZS 212.34 bilioni na TZS 25.88 bilioni ni mchango wa Serikali katika kazi za maendeleo, sawa na asilimia 71 ya lengo la miezi tisa. Kiasi kilichobakia cha TZS 196.3 bilioni kimetokana na fedha kutoka kwa Washirika wa Maendeleo.


MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA MPANGO WA MAENDELEO KWA MWAKA 2012/2013
25. Mheshimiwa Spika, Mpango wa Maendeleo kwa mwaka 2012/13 ulilenga kutekeleza jumla ya programu 38 na miradi 84 ya maendeleo kupitia klasta tatu zinazounda MKUZA II ambapo programu sita na miradi 18 ni mipya. Jumla ya TZS 341.1 bilioni zilitengwa kwa madhumuni hayo. Kati ya fedha hizo TZS 47.9 bilioni sawa na asilimia 14 ni kutoka Serikalini na TZS 293.2 bilioni sawa na asilimia 86 kutoka kwa Washirika wa Maendeleo.

Katika kipindi cha utekelezaji wa Julai - Machi 2012/13, jumla ya TZS 201.69 bilioni zimetumika kugharamia utekelezaji wa Programu/Miradi ya Maendeleo ikiwa ni sawa na asilimia 59 ya bajeti yote ya maendeleo. Kati ya fedha hizo TZS 25.88 bilioni ni mchango wa Serikali sawa na asilimia 54 ya makadirio ya mwaka ya mchango wa Serikali na TZS 175.81 bilioni ni mchango wa Washirika wa Maendeleo sawa na asilimia 60 ya makadirio ya fedha kutoka kwa Washirika wa Maendeleo.

26. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa utekelezaji ki-Klasta, Klasta ya kwanza ya Ukuzaji Uchumi na Upunguzaji Umaskini wa Kipato ilitekeleza jumla ya programu 21 na miradi 25 yenye makisio ya jumla ya TZS 197.9 bilioni sawa na asilimia 58 ya bajeti ya maendeleo kwa mwaka 2012/13. Fedha zilizotolewa kwa kipindi cha miezi tisa cha Julai-Machi ni TZS 136.8 bilioni sawa na asilimia 69 ya bajeti ya Klasta. Kati ya fedha hizo, Serikali imechangia TZS 8.2 bilioni sawa na asilimia 43.4 ya fedha iliyojipangia na Washirika wa Maendeleo walichangia TZS 128.6 bilioni sawa na asilimia 71.8 ya fedha zilizopangwa. Miongoni mwa Miradi mikubwa iliyokamilika chini ya Klasta hii ni ule wa uwekaji wa njia mpya ya umeme kutoka chini ya Bahari uliofadhiliwa na Serikali ya Marekani kupitia shirika lake la Changamoto za Milenia (MCC). Kwa mara nyengine tena kwa niaba ya Serikali na watu wa Zanzibar, nawashukuru sana watu wa Marekani na Serikali yao kwa msaada huu adhimu kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa Zanzibar.
27. Mheshimiwa Spika, Klasta ya pili ya Huduma na Ustawi wa Jamii ilitekeleza jumla ya programu 11na miradi 33 iliyokadiriwa kutumia jumla ya TZS 117.7 bilioni sawa na asilimia 35 ya bajeti ya maendeleo katika mwaka 2012/13. Fedha zilizotolewa kwa kipindi cha miezi tisa ni TZS 50.9 bilioni sawa na asilimia 43 ya bajeti ya Klasta. Kati ya fedha hizo, Serikali imechangia TZS 5.85 bilioni sawa na asilimia 42.7 ya fedha iliyojipangia na Washirika wa Maendeleo walichangia TZS 45.07 bilioni sawa na asilimia 43.3 ya fedha zilizopangwa.
28. Mheshimiwa Spika, Klasta ya tatu ya Utawala Bora na Umoja wa Kitaifa ilitekeleza jumla ya programu sita na miradi 26 yenye jumla ya TZS 25.42 bilioni sawa na asilimia 7.4 ya bajeti ya maendeleo katika mwaka 2012/13. Fedha zilizotolewa kwa kipindi cha miezi tisa cha Julai - Machi ni TZS 13.97 bilioni sawa na asilimia 54.9 ya bajeti ya Klasta. Kati ya kiasi hicho, Serikali imechangia TZS 11.82 bilioni sawa na asilimia 77.2 ya fedha iliyojipangia na Washirika wa Maendeleo walichangia TZS 2.14 bilioni sawa na asilimia 21.2 ya fedha zilizopangwa.


UTEKELEZAJI MAENEO YA KIPAUMBELE KWA MWAKA 2012/13


29. Mheshimiwa Spika, Serikali ilibainisha maeneo mbalimbali ya kipaumbele katika katika Bajeti yake ya mwaka 2012/13. Maeneo hayo ni pamoja na Kuimarisha huduma za afya; Kuimarisha ajira kwa vijana; Kuimarisha ustawi wa wazee; Kuimarisha elimu ya lazima; Kuimarisha uchumi; na Kuimarisha mashirikiano ya Sekta Binafsi na Umma. Tumeendelea kupiga hatua katika kuyafikia malengo yetu. Hata hivyo, utekelezaji umefikia viwango tofauti baina ya Sekta. Maelezo kamili ya hatua iliyofikiwa kwa kila eneo yatatolewa na Waheshimiwa Mawaziri husika katika Hotuba zao za Bajeti.


SENSA YA WATU NA MAKAAZI


30. Mheshimiwa Spika, itakumbukwa kuwa nchi yetu ilifanya Sensa ya Watu na Makaazi katika mwezi wa Agosti mwaka 2012. Serikali ilifanya jitihada maalum kuwaelimisha wananchi juu ya umuhimu wa Sensa. Matokeo ya Sensa hii yalitangazwa rasmi na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tarehe 31/12/2012. Matokeo hayo yameonesha kuwa nchi yetu, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, sasa ina jumla ya wakaazi 44,928,923. Sensa pia imebainisha kuwa idadi yetu katika visiwa vyetu vya Unguja na Pemba imefikia watu 1,303,569 ambapo watu 896,721, sawa na asilimia 69, wanaishi Unguja na watu 406,868, sawa na asilimia 31 ya watu wote wa Zanzibar, wanaishi katika kisiwa cha Pemba.

31. Mheshimiwa Spika, Matokeo haya ya Sensa pia yanaashiria kuwa idadi ya watu Zanzibar imekuwa ikiongezeka kwa wastani wa asilimia 2.8 kwa mwaka tokea Sensa ya mwaka 2002. Pamoja na kupungua kwa kasi yetu ya ukuaji wa idadi ya watu kutoka asilimia 3.1 kwa mwaka baina ya Sensa zilizopita, bado kiwango hiki cha asilimia 2.8 ni kikubwa na jitihada zaidi zinahitajika ili kukidhibiti. Kwa upande mwengine, Sensa pia imebainisha changamoto nyengine muhimu ambayo ni mkusanyiko mkubwa wa watu katika miji yetu. Kwa mujibu wa takwimu za Sensa, karibu nusu ya Wazanzibari wote, yaani asilimia 46, sawa na watu 593,678, wanaishi katika Mkoa wa Mjini Magharibi. Kwa kuzingatia ukubwa wa Mkoa wenyewe, idadi hiyo ya wakaazi inafanya wakaazi wa kila kilomita moja ya mraba kwa mkoa huu kuwa ni watu 2,581 ambayo ni ya pili kwa ukubwa kwa Tanzania ikitanguliwa na Dar Es Salaam yenye wastani wa wakaazi 3,133 kwa Kilomita ya Mraba. Uchambuzi muhimu wa takwimu za Sensa unaendelea na matokeo yake yataendelea kutolewa kwa awamu.

MAANDALIZI YA KATIBA MPYA YA JAMHURI YA MUUNGANO


32. Mheshimiwa Spika, katika Hotuba yangu ya mwaka jana nilizungumzia pia mchakato wa uandaaji wa Katiba mpya ya Jamhuri yetu ya Muungano na kuwanasihi wananchi WOTE kujiepusha na vitendo vya uvunjifu wa amani. Niliwaomba kustahamiliana pale tunapokuwa na mitazamo inayotofautiana. Nawashukuru wananchi walio wengi kwa kuisikiliza Serikali na kuwa watulivu. Hata hivyo, sio wote walikuwa na busara na hekima ya ustahamilivu. Wakati kwa ujumla mchakato wa ukusanyaji wa maoni juu ya Katiba hiyo umekwenda vizuri, kulijitokeza matukio yasiyopendeza na ya kuhatarisha amani. Tunashukuru hali imetulia kwa sasa lakini lazima tutumie uzoefu wa mchakato huo kujifunza. Tunahitaji kukuza demokrasia yetu kwa ustaarabu wa kuruhusu misimamo na mitazamo tofauti miongoni mwetu. Mchakato wenyewe wa kuipata hiyo Katiba mpya unaendelea. Mafunzo tuliyoyapata katika hatua ya ukusanyaji wa maoni yatuongoze vyema katika hatua zitakazofuata hadi kukamilika kwake.
33. Mheshimiwa Spika, tayari Tume ya Mabadiliko ya Katiba imeshatoa Rasimu ya Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kuna hatua nyengine kadhaa hadi kupatikana kwa Katiba mpya kama zilivyooneshwa katika Sheria ya Tume hiyo. Ni wajibu wa kila mmoja wetu na sote kwa pamoja kuhakikisha kwamba mageuzi haya muhimu katika nchi yetu hayatufarakanishi, sio wenyewe kwa wenyewe miongoni mwetu Wazanzibari wala baina yetu na ndugu zetu wa Tanzania Bara. Kwa vyovyote vile, kwa kuzingatia historia, muingiliano na ukaribu wa nchi zetu bado tunahitajiana baina yetu na Tanzania Bara. Bado tunahitaji ujirani ulio mwema na wa mashirikiano hata kama tungekuwa nchi tofauti, seuze leo tumo katika Jamhuri moja ya Muungano. Tukamilishe basi mchakato wa kupatikana Katiba mpya tukiendelea kuwa wamoja na ndugu.
34. Mheshimiwa Spika, baada ya mapitio hayo ya utendaji wetu wa miezi tisa ya mwanzo ya mwaka 2012/13, naomba sasa nieleze kwa mukhtasari mwelekeo wa Hali ya Uchumi kwa mwaka 2013 na Mpango wa Maendeleo na Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2013/14.
MAADHIMISHO YA MIAKA 50 YA MAPINDUZI


35. Mheshimiwa Spika, kuwepo kwetu hapa leo na demokrasia tunayojinasibisha nayo ni matokeo ya kazi kubwa na ya kishujaa iliyofanywa na wazee wa Taifa letu ambao walijumuika na kujitolea muhanga ili kizazi chetu kiwe huru na kuweza kujiamulia wenyewe mambo yake na kujiletea maendeleo. Matokeo ya kujitolea kwao muhanga ni Mapinduzi matukufu ya tarehe 12 Januari 1964. Tukijaaliwa, tarehe kama hiyo mwakani tutaadhimisha kutimia kwa mwaka wa 50 tokea kugombolewa kwa Zanzibar yetu. Hii ni siku adhimu na itahitaji maadhimisho yanayofanana nayo. Serikali imejipanga na kujiandaa vyema na maadhimisho hayo.


MWELEKEO WA HALI YA UCHUMI 2013


Uchumi wa Dunia na wa Kanda


36. Mheshimiwa Spika, uchumi wa dunia unatarajiwa kukua kufikia asilimia 3.3 mwaka 2013 ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 3.2 kwa mwaka 2012. Hali hii ya ukuaji mzuri inatarajiwa pia katika kila Kanda kama ifuatavyo :


(i) Kwa nchi zilizoendelea ukuaji unatarajiwa kufikia asilimia 1.2 mwaka 2013 kama ilivyokuwa mwaka 2012.


(ii) Kwa nchi zinazoendelea na zinazoibuka kiuchumi uchumi unatarajiwa kukua kwa asilimia 5.3 kwa mwaka 2013 ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 5.1 mwaka 2012;


(iii) Uchumi wa nchi zilizo Kusini mwa Jangwa la Sahara unatarajiwa kuimarika zaidi kwa kukua kwa asilimia 5.6 mwaka 2013 ikilinganishwa na asilimia 4.8 mwaka 2012.


MFUMKO WA BEI WA DUNIA


37. Mheshimiwa Spika, kasi ya mfumko wa bei duniani unatarajiwa kushuka kufikia asilimia 3.1 kwa mwaka 2013 ukilinganishwa na asilimia 3.3 mwaka 2012. Nchi zilizoendelea, kasi ya mfumko wa bei inatarajiwa kupanda kufikia asilimia 1.4 kwa mwaka 2013 ikilinganishwa na asilimia 1.3 mwaka 2012. Aidha, mfumko wa bei kwa nchi zinazoendelea na zinazoibuka kiuchumi hautakuwa na mabadiliko unatarajiwa kuwa asilimia 5.9 kwa mwaka 2013 kama ilivyokuwa mwaka 2012. Hata hivyo, mfumko wa bei kwa nchi za Kusini ya Jangwa la Sahara unatarajiwa kushuka hadi kufikia asilimia 7.2 mwaka 2013 ukilinganishwa na asilimia 9.1 mwaka 2012.


HALI YA UCHUMI WA ZANZIBAR


38. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2013 uchumi wa Zanzibar unatarajiwa kuendelea kuimarika na kukua kwa asilimia 7.5 kutoka ukuaji wa asilimia 7.0 mwaka 2012.

Matarajio ya ukuaji wa uchumi kwa mwaka 2013 yanatokana na mambo yafuatayo:
(i) Kukamilika kwa uwekaji wa waya wa umeme wa chini ya bahari kutoka Rasi Kiromoni Tanzania Bara hadi Rasi Fumba.
(ii) Kuimarika kwa sekta ya utalii kutokana na kupanuka kwa wigo wa bidhaa na huduma za utalii zinazofanywa na wajasiri amali, vile vile kukuza na kutangaza utalii katika soko la ndani na nje ya nchi kwa dhana ya utalii kwa wote.
(iii) Kuendelea kuimarika kwa vyanzo vya mapato.


(iv) Utekelezaji wa program ya mapinduzi ya kilimo Zanzibar.


(v) Kuendelea kuimarika kwa mashirikiano baina ya sekta za Umma na Binafsi.


(vi) Kupatikana kwa mkongo (fiber optic) ambao utarahisisha shughuli za huduma ya mawasiliano.


(vii) Kuvutia wawekezaji katika kuimarisha maendeleo ya viwanda vidogo vidogo nchini.


(viii) Kuimarisha uvuvi wa bahari kuu na ufugaji wa mazao ya baharini.


(ix) Kuendelea kwa uwekezaji katika kuimarisha miundombinu hasa ya barabara na viwanja vya ndege.


(x) Kuendelea na jitihada za usambazaji wa umeme vijijini na visiwa vidogo vidogo.


(xi) Kuendelea kuimarika kwa amani na utulivu wa kisiasa.


Mfumko wa Bei


39. Mheshimiwa Spika, mfumko wa bei unatarajiwa kushuka hadi kufikia asilimia 7.9 mwaka 2013 ukilinganishwa na asilimia 9.4 mwaka 2012. Matarajio hayo ya kushuka kwa kasi ya mfumko wa bei yanatokana na:


(i) Kushuka kwa mfumko wa bei duniani;


(ii) Kuimarika kwa uzalishaji wa ndani wa mazao ya chakula na biashara;


(iii) Kuimarika kwa Sekta ya Uvuvi; na


(iv) Kuendelea na utulivu wa sarafu ya Tanzania.


MWELEKEO WA MPANGO WA MAENDELEO KWA MWAKA 2013/14


40. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2013/14 Mwelekeo wa Mpango wa Maendeleo utazingatia zaidi utekelezaji wa Dira ya Maendeleo 2020, Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini (MKUZA II), Utekelezaji wa Mpango wa Miaka Mitano wa MKUZA II, Malengo ya Maendeleo ya Milenia ya mwaka 2015 na Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010.


MAENEO YA KIPAUMBELE KWA MWAKA 2013/14


41. Mheshimiwa Spika, haitarajiwi kwamba vipaumbele vya Serikali viwe vinabadilika sana mwaka hadi mwaka. Mengi ya maeneo ya kipaumbele yanahitaji uwekezaji wa muda mrefu ili kufikia malengo ya maendeleo ya nchi. Tunahitaji kujenga Taifa lenye maendeleo makubwa ya kiuchumi; lenye watu walioelimika, wataalamu wenye hadhi ya kimataifa na wenye siha na wasiosumbuliwa na maradhi yanayoepukika. Kwa kuzingatia ukweli huu, bado kipaumbele cha Serikali kitaendelea kuwa katika kukuza kwa kasi zaidi uchumi wetu na kuongeza ajira, hususan kwa vijana, kuimarisha ubora wa elimu, kuimarisha huduma za afya hususan katika upatikanaji wa dawa za lazima na katika upatikanaji wa maji safi na salama. Maeneo haya yote yataendelea kujitokeza kama kipaumbele kwa miaka ijayo ya fedha.

42. Mheshimiwa Spika, ajira itaendelea kuimarishwa kupitia Program mbalimbali za uwekezaji kama vile katika Kilimo, Viwanda na Utalii. Jambo la msingi ni kuhakikisha uendelevu wa ukuaji wa uchumi, kwa kasi kubwa zaidi na kwamba ukuaji huo lazima utafsirike katika kuleta ajira bora. Kuhusu elimu, Sekta hii inapaswa kuwa kipaumbele cha Taifa kwa muda wote. Mafanikio makubwa tayari yamefikiwa katika usawa wa kijinsia katika upatikanaji wa elimu hadi ngazi ya sekondari. Kipaumbele cha serikali katika sekta hii muhimu kitaendelea kuwa katika kuimarisha ubora wake. Kwa upande wa afya, bado upatikanaji wa dawa na visaidizi (sundries) utaendelea kupata umuhimu maalum. Kwa upande mwengine, Serikali inatambua shida wanayoipata wananchi katika maeneo mbalimbali kuhusiana na upatikanaji wa maji safi na salama. Mkazo utaendelea kuwekwa katika kuhakikisha kuwa huduma hii ya lazima kwa uhai inapatikana kwa wananchi walio wengi.

43. Mheshimiwa Spika, mambo yote haya yatafanyika bila ya kupuuza umuhimu wa miundombinu ya msingi kama vile barabara, bandari, viwanja vya ndege, umeme ikiwemo kutafuta chanzo mbadala cha nishati hiyo, kwa maendeleo ya nchi yetu. Katika Mpango wa Maendeleo wa mwaka ujao wa Fedha, Miundombinu ya Barabara, Viwanja vya ndege na Bandari imepangiwa jumla ya TZS 62.7 bilioni, ile ya Kilimo na Ufugaji jumla ya TZS 15.0 bilioni na ya Nishati jumla ya TZS 9.6 bilioni.
44. Mheshimiwa Spika, itakumbukwa kwamba wakati tukiendelea na bajeti ya Serikali ya mwaka 2012/13, nilitoa kauli ya Serikali juu ya ahadi yake ya ununuzi wa meli mpya ya abiria na mizigo. Sote kwa pamoja tulikubaliana na haja ya kujibana katika matumizi, kwa kukata bajeti ya Wizara zote, ili kupatikana fedha kwa madhumuni hayo. Kwa bahati mbaya, mchakato wa kupata mjenzi wa meli hiyo umehitaji muda mrefu kukamilika. Hii ni kutokana na ukweli kwamba Serikali imeamua kujenga meli hiyo badala ya kununua meli iliyotumika. Aidha, kwa maumbile yake, suala hili limehitaji majadiliano ya kina ya kiufundi, kifedha na kisheria. Hata hivyo, nina furaha kulijulisha Baraza lako Tukufu kuwa hatimae mchakato huu umepiga maendeleo mazuri na tayari mkataba wa ujenzi umeshatayarishwa na unatarajiwa kutiwa saini mwezi huu baina ya SMZ na Kampuni ya Daewoo International ya Korea ya Kusini. Meli hiyo yenye uwezo wa kuchukua abiria 1,200 na tani 200 za mizigo itagharimu Dola za Kimarekani 30.4 milioni sawa na TZS 48.6 bilioni na inatarajiwa kujengwa kwa kipindi cha miaka miwili na kuwasili nchini mwezi Juni 2015.

45. Mheshimiwa Spika, naomba nitaje kwa ufupi jinsi maeneo ya kipaumbele yalivyozingatiwa katika Bajeti ya Maendeleo kama ifuatavyo:
(i) Jumla ya TZS 55.4 bilioni zimetengwa kwa ajili ya Miradi ya Maji safi na salama;

(ii) Sekta ya Elimu imetengewa TZS 32.8 bilioni;
(iii) Sekta ya Afya imetengewa jumla ya TZS 23.9 bilioni; na
(iv) Programu ya Ajira kwa Vijana imetengewa TZS 1.1 bilioni kwa ajili ya ajira ya moja kwa moja, zaidi ya ile inayotokana na utekelezaji wa Programu na Miradi mbalimbali kama nilivyoeleza awali.
Kwa ujumla, katika Bajeti ya mwaka ujao wa fedha, maeneo haya manne tu ya kipaumbele yametengewa jumla ya TZS 113.2 bilioni kati ya TZS 305.4 bilioni. Kiasi hiki ni zaidi ya theluthi moja ya Bajeti yote ya Mpango wa Maendeleo, sawa na asilimia 37 ya Bajeti hiyo. Kwa kuzingatia kiasi hicho kikubwa cha uwekezaji kinachotengwa kwa ajili ya huduma hizo, bajeti ya mwaka ujao wa fedha ni Bajeti ya Huduma za Jamii kwa wananchi wa Zanzibar.
46. Mheshimiwa Spika, sambamba na vipaumbele hivyo, maeneo mbalimbali ya utekelezaji wa Dira ya 2020 na MKUZA II yamewekwa katika Programu tano kubwa kama ifuatavyo:
A. Programu ya Mageuzi ya Kiuchumi


Programu hii inakusudia kuziimarisha sekta ya utalii, biashara, viwanda na kilimo.
B. Programu ya Mageuzi ya Serikali
Programu hii ina lengo la kuimarisha Utawala Bora, Uwajibikaji na utoaji huduma kwa matokeo kwa utendaji, na utoaji huduma wa Serikali kwa kupima viashiria vya msingi vya utendaji (KPIs); kupambana na rushwa na kujenga uwezo.
C. Programu ya Kujenga Uwezo wa Rasilimali Watu
Kwa upande wa Kujenga Uwezo wa Rasilimali watu maeneo yatakayozingatiwa ni kuimarisha huduma za afya na ubora wa elimu.

D. Masuala Mtambuka
Kuzingatia mabadiliko ya tabia nchi, maafa na uhifadhi wa mazingira, jinsia na watu wenye mahitaji maalum.

E. Visaidizi (enablers)
Kwa utekelezaji wa mageuzi yaliyotangulia Serikali itahitaji viwezeshaji muhimu vitakavyojumuisha uimarishaji wa miundombinu, kukuza ujuzi wa kazi na ujasiriamali, ubora na viwango na mkakati wa kuendeleza sekta binafsi.
RASILIMALI KWA AJILI YA UTEKELEZAJI WA MPANGO WA MAENDELEO KWA MWAKA 2013/14
47. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/14 Serikali inatarajia kutekeleza jumla ya Programu 35, moja ikiwa ni mpya, na Miradi 75 ya maendeleo ambapo tisa ni mipya. Jumla ya TZS 305.4 bilioni zinatarajiwa kutumika kwa kutekeleza Programu na Miradi hiyo. Kati ya fedha hizi, Serikali itatoa TZS 70.0 bilioni na Washirika wa Maendeleo watachangia TZS 235.4 bilioni ikiwemo ruzuku ya TZS 86.8 bilioni na mikopo TZS 148.6 bilioni.

MAANDALIZI YA BAJETI INAYOZINGATIA PROGRAMU


48. Mheshimiwa Spika, kwa miaka miwili sasa Serikali imeendelea na matayarisho ya maandalizi ya mageuzi ya mfumo wa bajeti yenye lengo la kuimarisha uandaaji, utekelezaji na usimamizi wa bajeti na unaosisitiza matokeo kutokana na matumizi ili kuleta ufanisi katika utekelezaji wa bajeti. Mfumo huu umeanza kutekelezwa kwa majaribio mwaka huu 2012/13 na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, Wizara ya Afya, Wizara ya Kilimo na Maliasili, Wizara ya Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati, Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano na Ofisi ya Rais Fedha, Uchumi na Mipango ya Maendeleo. Majaribio hayo yamehusu kutayarisha Muundo na Maelezo ya Programu yenye kuhusisha malengo, matokeo, viashiria, shabaha na gharama za Programu. Maelezo hayo yaliwasilishwa sambamba na mfumo wa sasa wa bajeti. Kwa Bajeti za mwaka ujao wa fedha wa 2013/14, wizara zote zilizobakia nazo zimeingia katika maandalizi hayo ya mfumo mpya wa Bajeti kwa kuhusisha maeneo yaliyotajwa. Matarajio ni kwamba ifikapo mwaka 2014/15 Bajeti ya Serikali iwe inaandaliwa na kutekelezwa kwa kuzingatia mfumo huo wa Programu.
MWELEKEO WA BAJETI 2013/14

SURA YA BAJETI

Mapato


49. Mheshimiwa Spika, Serikali inatarajia kutumia jumla ya TZS 658.5 bilioni katika mwaka wa fedha 2013/14 ikimaanisha ongezeko dogo la asilimia 1.5 kutoka Bajeti ya TZS 648.9 bilioni mwaka 2012/13. Kwa kuzingatia uwezo wa sasa wa mapato kutokana na vyanzo vya ndani, inatarajiwa kuwa mapato ya ndani yatafikia jumla ya TZS 333.7 bilioni na hivyo kufanya jumla ya mapato hayo kufikia TZS 338.7 bilioni ikichanganywa na TZS 5.0 bilioni zinazotarajiwa kusalia mwisho wa mwaka. Mapato ya ndani yanahusisha mapato ya Kodi na yasiyo ya kodi, ikiwemo gawio kutoka Benki Kuu na Mashirika ya Serikali. Ikilinganishwa na matumizi yanayotarajiwa kama nilivyoyataja, kiasi hicho cha mapato cha TZS 338.7 bilioni kitaacha nakisi ya TZS 310.5 bilioni.


50. Mheshimiwa Spika, katika mwaka huo wa 2013/14, Serikali inatarajia kupokea jumla ya TZS 277.9 bilioni kutoka kwa Washirika wa Maendeleo. Fedha hizi zinajumuisha TZS 235.4 bilioni za Mikopo na Ruzuku kwa Programu na Miradi ya Maendeleo, TZS 40.0 bilioni za Msaada wa Kibajeti na TZS 2.5 bilioni kutokana na msamaha wa madeni (MDRI). Yakichanganywa na mapato ya ndani, jumla ya mapato yote ya Serikali inafikia TZS 616.6 bilioni. Kwa kuzingatia matumizi yote ya Serikali ya TZS 658.5 bilioni mapato haya yanaacha nakisi ya TZS 41.9 bilioni.


51. Mheshimiwa Spika, ili kuziba pengo hilo la Bajeti, Serikali inakusudia kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha mapato ya ndani kwa kurekebisha viwango vya kodi na ada za huduma mbalimbali. Kwa ujumla, hatua hizo zinatarajiwa kuingiza TZS 16.9 bilioni, na hivyo kuzidi kupunguza pengo la bajeti na kufikia TZS 25.0 bilioni. Serikali inakusudia kukopa ndani kwa kiwango hicho cha TZS 25 bilioni na hivyo kuleta uwiano wa mapato na matumizi katika Bajeti.


Matumizi


52. Mheshimiwa Spika, kati ya matumizi ya TZS 658.5 bilioni yanayotarajiwa kwa mwaka 2013/14, TZS 353.1 bilioni sawa na asilimia 53.6 ni kwa ajili ya kazi za kawaida na TZS 305.4 bilioni sawa na asilimia 46.4 ni kwa kazi za maendeleo. Itakumbukwa pia kuwa Serikali, kupitia kwa Mheshimiwa Rais, iliahidi kuimarisha kipato cha Mfanyakazi kila hali ya uchumi na uwezo wa serikali inaporuhusu. Katika kutekeleza ahadi hiyo, marekebisho makubwa ya maslahi ya wafanyakazi yalifanyika kuanzia mwezi Oktoba 2011. Ahadi ya Mheshimiwa Rais bado ipo na itaendelea kutekelezwa kama alivyoahidi. Kwa azma hiyo, katika mwaka ujao wa fedha, Serikali inakusudia kuimarisha tena maslahi ya wafanyakazi. Jumla ya TZS 17.5 bilioni zimetengwa kwa madhumuni hayo na kuhudumia na ajira mpya na marekebisho mengine muhimu. Kwa kutambua mchango mkubwa wa Baraza lako, marekebisho pia yamefanywa kwa maslahi ya Wajumbe wako ambao nao wana majukumu mengi.


53. Mheshimiwa Spika, matumizi yaliyotajwa hapo juu ya TZS 658.5 bilioni ni jumla tu ya mtumizi yote. Matumizi haya yanahusisha pia yale ya lazima, kwa mujibu wa Sheria, na mengine ambayo tayari Serikali yetu ilikwishajifunga na hivyo ni lazima yafanyike. Miongoni mwa matumizi ya lazima (Mandatory Expenditure) ni haya yafuatayo:

(i) Mishahara (pamoja na ruzuku) TZS 176.3 bilioni.


(ii) Malipo ya Kiinua Mgongo na Pencheni – TZS 20.6 bilioni.


(iii) Malipo ya Dhamana za Hazina na Hati Fungani – TZS 14.5 bilioni


(iv) Huduma za Viongozi wakuu, Hospitali na chakula cha vikosi– TZS 11.5 bilioni.


(v) Mchango wa Washirika wa Maendeleo kwa Programu na Miradi ya Maendeleo – TZS 235.4 bilioni.


(vi) Mchango wa SMZ kwa Programu na Miradi ya Maendeleo inayoendelea na ambayo ina mikataba yenye thamani TZS 56.0 bilioni.


(vii) Mahitaji ya dawa, vifaa vidogo vidogo (sundries) pamoja na dawa za maabara zenye thamani ya TZS 2.1 bilioni.


54. Mheshimiwa Spika, kwa ujumla, kiasi cha TZS 516.4 bilioni tayari zina matumizi maalum na haziwezi kugawanywa. Hali hii inabakisha TZS 142.1 bilioni ambazo ndio zimegawanywa kwa ajili ya kazi za kawaida kwa Serikali na taasisi zake zinazopokea ruzuku, matumizi ya Mfuko Mkuu wa Serikali na mchango wa Serikali kwa miradi mingine ya maendeleo.


55. Mheshimiwa Spika, pamoja na kuendelea kusisitiza kuchukua hatua za kuimarisha mapato, Serikali pia inaendelea na hatua maalum zinazolenga kuangalia uwezekano wa kubana matumizi kwa kazi za kawaida bila ya kuathiri utendaji. Lengo ni kuwa kama kuna fedha zitakazookolewa, fedha hizo zitumike kwa kazi za maendeleo. Kwa sasa, zoezi la kufanya mapitio ya majukumu ya kila Wizara/Taasisi linaendelea. Kukamilika kwake kunatarajiwa kusaidia kuongeza ufanisi kupitia marekebisho ya kitaasisi na kuepusha mgongano wa kimajukumu.

MAPENDEKEZO YA HATUA ZA KUIMARISHA MAPATO


56. Mheshimiwa Spika, moja ya lengo la Serikali ni kuhakikisha utulivu wa mfumo wa kodi ili uwe wenye kutabirika na hivyo kuvutia uwekezaji. Hatua za kuongeza kodi huchukuliwa pale tu inapokuwa ni lazima. Kwa upande mwengine, sasa hivi, kuliko ilivyokuwa kwa wakati mwengine wowote ule, haja ya kupunguza utegemezi wa wafadhili inajitokeza. Changamoto zinazojitokeza kutokana na athari ya msukosuko wa kiuchumi na fedha katika eneo la Ulaya na kukua kwa mahitaji ya huduma kwa wananchi na dhamira ya Serikali ya kuimarisha ubora wa huduma hizo kunapelekea haja ya kuimarisha zaidi mapato yetu ya ndani. Kwa kuzingatia mambo yote haya muhimu, na ili kuziba nakisi ya bajeti katika mwaka ujao wa fedha 2013/14 kama nilivyoeleza awali, Serikali inapendekeza kufanya marekebisho ya sheria na viwango vya kodi na ada mbalimbali kwa kurekebisha Sheria zifuatazo:

(i) Sheria ya VAT, namba 4 ya mwaka 1998.


(ii) Sheria ya Kodi za Hoteli namba 1 ya mwaka 1995.


(iii) Sheria ya Ada za Bandari namba 2 ya mwaka 1999.


(iv) Sheria ya Ushuru wa Stempu namba 6 ya mwaka 1996.


(v) Sheria ya Kodi za Mafuta namba 7 ya mwaka 2001.


(vi) Sheria ya Usafiri wa Barabara namba 7 ya mwaka 2003 na Kanuni zake.


(vii) Sheria ya Kodi ya Mapato ya mwaka 2004 (Presumptive Tax Scheme).


(viii) Sheria ya Ardhi namba 12 ya mwaka 1992.


(ix) Sheria ya Kuvutia na Kulinda Vitega Uchumi namba 11 ya mwaka 2004.


(x) Sheria ya Usimamizi wa Kodi namba 7 ya mwaka 2009.


(xi) Sheria ya Rufaa ya Kodi namba 1 ya mwaka 2006.

A. Marekebisho ya Sheria ya VAT
57. Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio ya uwekezaji katika sekta ya utalii na mchango wake mkubwa katika uchumi wa nchi yetu, bado kumekuwa na udanganyifu katika ulipaji wa kodi zinazotokana na sekta hii. Baadhi ya Wawekezaji wameendelea kudanganya kuhusu kiasi wanachopaswa kulipa kwa kutaja kiwango kidogo cha kutozea kodi kwa mahoteli. Pamoja na hatua mbalimbali za kisheria na kiutawala zilizochukuliwa na Serikali ili kurekebisha hali hii, bado kuna fursa ya kuimarisha zaidi mapato hayo ikiwemo kwa kudhibiti zaidi msingi wa kutozea kodi. Kwa mnasaba huo, inapendekezwa kurekebisha kiwango cha usajili wa mahoteli katika kodi ya VAT kwa kuzisajili tu hoteli zinazofikia kiwango cha chini cha usajili wa VAT na zenye kutoza ada ya huduma kuanzia USD 100 kwa mtu kwa siku (au sawa na thamani hiyo kwa Shilingi za Kitanzania). Hoteli nyengine zote zisizofikia kiwango hicho zitalipa Kodi ya Hoteli (Hotel Levy).

58. Mheshimiwa Spika, nchi nyingi zinapata tabu juu ya udhibiti wa udanganyifu katika misamaha ya kodi. Serikali imekuwa ikichukuwa jitihada za kudhibiti misamaha ya kodi lakini bado kuna fursa ya kudhibiti zaidi. Chini ya utaratibu wa sasa wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT), Serikali hutoa unafuu kwa Taasisi mbalimbali chini ya Jadweli la Tatu la Sheria ya VAT. Ili kukabiliana na udanganyifu na kuimarisha zaidi udhibiti wa misamaha, inapendekezwa kupunguza unafuu unaotolewa kwa baadhi ya Taasisi. Unafuu wa asilimia 100 ubakie tu kwa ofisi za Kibalozi na Miradi yenye ufadhili wa Washirika wa Maendeleo, vifaa na huduma zinazostahili. Kwa Taasisi nyengine zote zinazostahiki msamaha huo chini ya Jadueli hilo unafuu utolewe kwa asilimia 80 tu ili kiasi kilichobakia cha asilimia 20 kilipiwe kodi.

Kwa kuzingatia na hatua nyengine za kiutawala zitazochukuliwa katika VAT, hatua hiyo inatarajiwa kuongeza mapato ya Serikali kwa TZS 4.56 bilioni.
B. Marekebisho ya Sheria ya Kodi za Hoteli
59. Mheshimiwa Spika, sambamba na marekebisho ya Sheria ya VAT, inapendekezwa pia kufanya marekebisho kwenye Sheria ya Kodi za Hoteli kwa kutoza kodi kwa kuzingatia hadhi ya hoteli. Inapendekezwa kuwa hoteli zote zinazotoa huduma kwa kiwango kisichozidi Dola za Kimarekani (USD) 45 kwa mgeni kwa siku ziendelee kulipa VAT kwa kiwango maalum (specific). Hata hivyo, inapendekezwa kupandisha kiwango hicho kutoka USD 5 kwa mtu kwa siku ya sasa hadi USD 8. Hoteli zilizobakia zinazotoza zaidi ya USD 45 lakini hazitimizi sifa ya kusajiliwa chini ya VAT zitaendelea kutozwa Kodi ya Hoteli kwa kiwango cha asilimia 18 kama ilivyo sasa. Marekebisho haya yanatarajiwa kuiingizia Serikali jumla ya TZS 2.86 bilioni.
C. Kurekebisha Sheria ya Ada ya Viwanja vya Ndege
60. Mheshimiwa Spika, marekebisho yanayopendekzwa kufanywa katika Sheria hii yanalenga kuleta uwiano baina ya kiwango kinachotozwa Zanzibar cha ada ya uwanja wa ndege na viwango vinavyotozwa katika nchi nyengine za Afrika ya Mashariki. Inapendekezwa kupandisha ada hiyo kutoka USD 35 kwa mtu iliyopo sasa hadi USD 40 kwa mtu kama ilivyo kwa nchi jirani za Afrika ya Mashariki. Marekebisho haya yatagusa tu wasafiri waendao nje ya nchi. Kwa wasafiri wa ndani ya nchi, kiwango cha sasa kitaendelea kutumika kama kilivyo. Matarajio ni kwamba hatua hiyo itaongeza mapato kwa TZS 1.2 bilioni.
D. Marekebisho ya Ushuru wa Stempu
61. Mheshimiwa Spika, Sheria hii ilifanyiwa marekebisho ya viwango mwaka jana. Hata hivyo, wakati wa utekelezaji, imebainika haja ya Serikali kuangalia tena unafuu wa kodi unaotolewa kwa bidhaa za vyakula muhimu. Kwa upande mwengine, kumejitokeza pia ugumu wa utekelezaji katika maeneo ya baadhi ya hati zinazopaswa kulipiwa Ushuru wa Stempu. Ili kuondoa kasoro zilizojitokeza, marekebisho yafuatayo yanapendekezwa:


(i) Kushusha rasmi kiwango cha Ushuru wa Stempu kwa bidhaa za mchele na unga wa ngano kutoka asilimia 3 cha sasa hadi asilimia 2;


(ii) Aidha, inapendekezwa kupanua ukomo wa kiwango cha malipo ya ushuru huu uliotolewa mwaka jana kwa mikopo ili utumike kwa hati nyengine zenye hadhi ya mikopo kama vile “Debentures”. Kwa utaratibu huu, marekebisho yataweka kiwango cha juu cha Ushuru huu cha TZS 100,000.


(iii) kurekebisha Sheria ya Ushuru wa Stempu kulingana na utaratibu wa “Presumptive Tax” kama unavyopendekezwa hapa chini.


62. Mheshimiwa Spika, sambamba na marekebisho hayo ya sheria, Serikali kupitia ZRB inakusudia kuchukua hatua kadhaa za kiutawala zikiwemo za kuanzisha ofisi za ZRB katika Mikoa ya Kusini na Kaskazini Unguja ili kuweza kuhudumia kwa karibu zaidi walipakodi waliopo katika maeneo hayo na kutoa uwakala wa zuio la Ushuru wa Stempu (withholding Tax) kwa hoteli mbalimbali. Tayari ZRB inazo ofisi katika miji ya Chakechake, Wete na Mkoani kwa Pemba. Kwa pamoja hatua hizi zinategemewa kuingiza jumla ya TZS 600.0 milioni.
E. Kuimarisha utaratibu wa utozaji kodi ya mafuta
63. Mheshimiwa Spika, kumeendelea kuwepo upotevu wa mapato ya Serikali kupitia magendo katika biashara ya mafuta. Hali hii haiwezi kuachwa iendelee. Serikali kupitia TRA, ZRB na vikosi vya ulinzi itafanya operesheni maalum na ya kudumu ya kudhibiti magendo na vituo visivyo rasmi ya kuuzia mafuta. Aidha, ili kudhibiti uingiaji wa mafuta ya magendo, makubaliano ya msingi yamefikiwa baina ya TRA/ZRB na Mamlaka ya Mapato ya Kenya (KRA) ya kuanzisha utaratibu rasmi wa kubadilishana taarifa za uingizaji wa mafuta. Lengo ni kuzuia udanganyifu unaofanywa na waingizaji wasio waaminifu na hivyo kuchangia katika kuwepo kwa magendo. Matarajio ni kwamba hatua hizi zitaongeza mapato ya TZS 5.0 bilioni. Sambamba na hatua hizo, ili kuzuia uwezekano wa udanganyifu na kuhakikisha kuwepo kwa bidhaa hiyo muhimu kwa muda wote, Serikali itafanya upembuzi yakinifu juu ya uwezekano na utaratibu bora wa kuwa na muingizaji mmoja tu wa mafuta (single importer), kama ilivyokuwa kabla.
F. Marekebisho ya utaratibu wa malipo ya leseni ya njia
64. Mheshimiwa Spika, moja ya msingi muhimu wa kutoza kodi ni kuwa kodi ilipwe kwa kuzingatia matumizi na faida inayopatikana kutokana na matumizi ya huduma husika (benefit principle). Utaratibu wa sasa wa malipo ya matumizi ya barabara hauzingatii msingi huu muhimu na unawezesha kuwepo kwa leseni bandia za njia na hivyo kuikosesha mapato serikali. Ili kukabiliana na kasoro hizo, inapendekezwa kubadilisha utaratibu wa ukusanyaji wa ada hiyo kwa kuiingiza katika mafuta. Kwa kuzingatia wastani wa matumizi ya kawaida na bila ya kumuongezea mzigo mtumiaji wa kawaida wa barabara, inapendekezwa kutozwa TZS 35 kwa lita ya dizeli au petrol itakayouzwa nchini kama leseni ya njia. Kwa kuwa kiwango hicho hakitaongeza mapato (revenue neutral), hatua hiyo inatarajiwa kuongeza mapato kwa TZS 124 milioni tu kutokana na udhibiti wa leseni bandia na ucheleweshaji wa sasa wa malipo.
G. Marekebisho ya viwango vya malipo ya leseni za udereva
65. Mheshimiwa Spika, kwa muda sasa Zanzibar imekuwa ikitumia leseni za kisasa za udereva ambazo gharama za utengenezaji wake zimeendelea kupanda. Ili kufidia gharama zinazotumika kutayarisha nyaraka za leseni za udereva na leseni hizo za kisasa kuwa endelevu, inapendekezwa kurekebisha kiwango cha leseni za udereva kutoka TZS 15,000 hadi TZS 20,000 kwa leseni ya mwaka mmoja, TZS 25,000 hadi TZS 30,000 kwa leseni ya miaka miwili na TZS 35,000 hadi TZS 40,000 kwa leseni ya miaka mitatu. Hatua hii inatarajiwa kuongeza mapato ya Serikali kwa TZS 120 milioni.
H. Kuweka utaratibu wa kusajili magari mara tu yanakapoingia nchini
66. Mheshimiwa Spika, kutokana na kuimarika kipato cha wananchi na biashara, kumejitokeza kushamiri kwa biashara ya magari hapa nchini katika sehemu mbalimbali. Kwa bahati mbaya, kumejitokeza mtindo wa baadhi ya watu kutembelea magari hayo bila ya kutiwa nambari za usajili. Tabia hii ikiachiliwa inaweza kuathiri usalama wa watumiaji wa barabara (safety) na pia kuongeza vitendo vya uhalifu. Ili kukabiliana na hali hiyo, kuanzia mwaka ujao wa fedha, vyombo vya moto vitasajiliwa mara tu vinapokamilisha taratibu za Forodha na kabla ya kutoka bandarini. Sambamba na hatua hiyo, mambo yafuatayo yanapendekezwa:
(a) Kuongeza kiwango cha usajili (registration) wa vyombo vya moto kutoka TZS 50,000 hadi TZS 70,000, na hivyo kuongeza mapato kwa TZS 288 milioni; na
(b) Ili kuepusha kurundikana sana kwa nambari zisizotumika kwa magari yaliyokusudiwa kupitia tu nchini kwa ajili ya biashara, kuanzisha namba maalum kwa vyombo vya moto vinavyoingizwa kwa kusafirishwa nje ya Zanzibar kibiashara. Hatua hiyo itaongeza mapato ya Serikali kwa TZS 347.
I. Sheria ya Kodi ya Mapato 2004 (Presumptive Tax Scheme (PTS)
67. Mheshimiwa Spika, moja ya eneo ambalo limekuwa likilalamikiwa sana ni utaratibu wa kutoza kodi kwa wafanyabiashara wadogowadogo katika sekta isiyo rasmi. Wengi wa wafanyabiashara hawa hawana uwezo wa kuweka kumbukumbu zinazohitajika kutozea kodi ya mapato na Ushuru wa Stempu. Serikali inahitaji kuwalea wafanyabiashara hao na kuwapunguzia mzigo wa kutimiza matakwa ya taratibu za kodi (compliance burden). Utaratibu unaotumika katika nchi nyengine, ikiwemo Tanzania Bara, ni kuwatoza kodi wafanyabiashara kama hawa kwa utaratibu wa “Presumptive Tax” ambao ni mwepesi zaidi kuufata kwani unaunganisha kodi ya mapato na ushuru wa Stempu na hauhitaji wafanyabiashara kuwasilisha Marejesho (returns) kila mwezi. Hadi sasa utaratibu wa PTS kwa Zanzibar unatumika kwa kuwatoza kodi ya mapato wamiliki wa magari ya biashara tu (taxi, daladala, gari za kukodisha na za mizigo).
Inapendekezwa kutumia utaratibu huo wa PTS kuanzia mwaka ujao wa fedha kwa wafanyabiashara ambao mauzo yao kwa mwaka hayazidi TZS 10 milioni. Wafanyabiashara wote watakaotozwa kodi chini ya utaratibu huu hawatalazimika tena kulipa Ushuru wa Stempu. Hatua hii inatarajiwa kuongeza mapato kwa TZS 400 milioni.
J. Marekebisho ya Misamaha ya Kodi
68. Mheshimiwa Spika, kwa muda mrefu SMZ imekuwa ikitumia vivutio mbalimbali ili kushajiisha uwekezaji binafsi nchini. Moja ya sababu ya kiwango cha vivutio vilivyopo ni kasoro mbalimbali za kisoko (market distortions) zilizokuwepo wakati huo hasa katika kukosekana miundombinu ya msingi kama vile barabara za lami, umeme na maji katika maeneo yote ya uwekezaji. Hivi sasa hali imebadilika kwani tayari miundombinu hiyo inapatikana katika takriban maeneo yote ya uwekezaji na kupelekea kupatikana mafanikio makubwa katika uwekezaji katika sekta ya utalii hususan ujenzi wa hoteli. Haja inayojitokeza sasa ni kupanua uwekezaji katika maeneo mengine muhimu ya kiuchumi ambayo hayajapata msukumo mkubwa kama vile viwanda na kilimo. Ili kuimarisha mapato ya serikali na kuweza kuvutia uwekezaji katika maeneo mapya ya viwanda na kilimo, mambo yafuatayo yanapendekezwa:


(i) Kurekebisha Sheria ya ZIPA kwa kufuta misamaha ya Kodi kwa vifaa vya ujenzi na vyengine vidogovidogo kwa miradi yote ya hoteli na mikahawa. Msamaha utaendelea kutolewa kwa vifaa vya uwekezaji (capital goods) kama vile mashine na vifaa vyengine vikubwa vya uwekezaji;


(ii) Kuandaa na kutoa unafuu maalum kwa uwekezaji katika viwanda, kilimo na uwekezaji wenye umuhimu maalum (Strategic Investment) kama utakavyowekewa utaratibu hapo baadae;


(iii) Ili kuzuia udanganyifu wa thamani ya uwekezaji unaopelekea kuonekana kiwango kikubwa cha misamaha, kusamehe asilimia 80 tu ya mapato kwa misamaha yote ya watu binafsi, taasisi za kidini, NGOs na uwekezaji. Kiasi kilichobakia kitakusanywa.
Hatua hizi zinatarajiwa kuiingizia Serikali jumla ya TZS 5.4 bilioni.
K. Kuimarisha Mapato kutokana na Ukodishaji wa Ardhi
69. Mheshimiwa Spika, Zanzibar ni kisiwa kidogo na hivyo ardhi yake ni rasilimali muhimu sana. Serikali imekuwa ikikodisha ardhi yake ili iweze kutumika kwa shughuli za uwekezaji ili kuendeleza uchumi na jamii. Watu wengi wamekuwa wakihoji udogo wa viwango vya kodi ya ardhi vinavyotumika Zanzibar. Pamoja na udogo wa viwango hivyo, Serikali pia imekuwa ikisamehe kodi kwa kipindi chote cha ujenzi wa mradi. Ili kuweza kunufaika zaidi na rasilimali hii muhimu, inapendekezwa yafuatayo kuhusiana na kodi ya ardhi:
(i) Kuyatambua na kuyaweka katika “database” maeneo yote ya ardhi yaliyokodishwa;
(ii) Kurekebisha viwango vya kodi kwa kuweka uwiano kwa matumizi yanayofanana kwa kuzingatia mahali lilipo eneo na matumizi yake;


(iii) Kuweka viwango maalum vya kuvutia uwekezaji katika maeneo ya vipaumbele vya viwanda, kilimo na miradi maalum (strategic investments); na


(iv) Ili kuondoa mtindo wa maotoe katika kukodi ardhi (speculation) na kuhakikisha inatumika vyema kwa maendeleo ya uchumi, kufuta utaratibu wa kutoa muda wa msamaha kwa matumizi ya ardhi (grace period). Anaekodishwa atalazimika kuanza kuilipia mara tu baada ya kukodishwa.
Mwaka ujao wa fedha unatarajiwa kuwa wa kujipanga zaidi na usimamizi ili uwezeshe kupatikana makisio sahihi ya kodi baada ya kuimarishwa usimamizi. Hata hivyo, hatua hizi zinatarajiwa kuiongezea Serikali mapato kwa angalau TZS 500 milioni.
L. Hatua za Kiutawala
70. Mheshimiwa Spika, pamoja na hatua zilizopendekezwa hapo juu, bado taasisi za ukusanyaji za TRA na ZRB zitaendelea kuchukua hatua nyengine za kiutawala na utendaji zikiwemo za kuwatambua na kuawasijili walipakodi wapya, kusimamia maeneo yaliyoonesha udhaifu kama vile mikataba ya ukodishaji wa hoteli bila ya kuwepo dhamana, matumizi ya “tax clearance”, kusajili Washauri wa Kodi (Tax Consultants) na kugomboa kodi zilizo mikononi mwa walipakodi. Inatarajiwa kuwa hatua hizi zitaongeza mapato kwa TZS 500 milioni.
Kwa jumla hatua zote zinazopendekezwa zinatarajiwa kuongeza mapato ya Serikali kwa TZS 16.9 bilioni.
SURA YA MAPATO KWA MWAKA UJAO WA FEDHA 2013/2014
Mapato ya Ndani
71. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka ujao 2013/14 Serikali inakusudia kuongeza juhudi ya ukusanyaji mapato yafikie asilimia 22.1 ya Pato la Taifa kutoka asilimia 21.3 ya mwaka 2012/13. Katika mwaka ujao wa fedha, mapato kutokana na vyanzo vya ndani yanakadiriwa kufikia TZS 324.6 bilioni. Kitaasisi, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inakadiriwa kukusanya TZS 147.9 bilioni, Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) TZS 171.7 bilioni, TZS 5.0 bilioni gawio kutoka Benki Kuu na Mashirika ya SMZ, TZS 26.0 bilioni zitazokusanywa na Mhasibu Mkuu wa Serikali kama Kodi ya Mapato kwa wafanyakazi wa SMT waliopo Zanzibar na mkopo wa ndani wa TZS 25.0 bilioni. Zikichanganywa na TZS 5.0 bilioni za kuanzia mwaka, jumla ya mapato ya ndani yanatarajiwa kufikia TZS 380.6 bilioni.
Misaada ya Nje

72. Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2013/2014 inatarajia kupata jumla ya TZS 277.9 bilioni kutoka kwa Washirika wa Maendeleo kwa mwaka ujao wa fedha. Kati ya fedha hizo, TZS 235.4 bilioni ni kwa ajili ya Programu na Miradi ya Maendeleo ikiwemo TZS 148.6 bilioni za Mikopo na TZS 86.8 bilioni za ruzuku. Misaada ya kibajeti (GBS) inatarajiwa kufikia TZS 40.0 bilioni ikihusisha TZS 26.5 bilioni za ruzuku na TZS 13.5 bilioni ambazo ni mikopo. Kiasi kilichobakia cha TZS 2.5 bilioni kinatokana na salio la sehemu ya mgao Zanzibar kutokana na Msamaha wa Madeni (MDRI).
73. Mheshimiwa Spika, muundo wa Mapato unaojitokeza hapo juu unamaanisha kuwa utegemezi wa bajeti kutoka kwa Washirika wa Maendeleo, unaopimwa kama uwiano wa ruzuku kwa jumla ya matumizi, utaendelea kupungua hadi kufikia asilimia 17.2 mwaka 2013/2014 kutoka asilimia 21 mwaka 2012/2013. Aidha, uwiano wa ruzuku kwa Pato la Taifa unatarajiwa kupungua hadi kufikia asilimia 8.5 kwa mwaka wa 2013/2014 kutoka asilimia 11.2 mwaka 2012/2013. Ni muhimu kuendelea kuhakikisha kuwa mapato ya ndani yanakuwa kwa kasi zaidi kuliko ile ya ruzuku.
74. Mheshimiwa Spika, mukhtasari wa mfumo wa Bajeti ya mwaka 2013/14 baada ya hatua mbalimbali za mapato na mgawanyo wa matumizi ni kama unavyoonekana katika Jadweli hapa chini.
Mfumo wa Bajeti ya mwaka 2013/14
Maelezo Makisio Makisio Ongezeko

2012/13 2013/14 (%)

MAPATO


A. Mapato ya ndani 294.1 324.6 10.4


B. 4.5% Msaada wa kibajeti (GBS) 39.9 40.0 0.3


C. Dhamana za Hazina/Hati Fungan 15.8 25.0 58.2


D. Kodi Mapato kwa w/kazi wa SMT 0.0 26.0


E. Bakaa ya bajeti 2012/13 5.9 5.0 -15.3


F. Msamaha wa Madeni (MDRI) 2.5


G. Mikopo na Ruzuku 293.2 235.4 -19.7


Jumla ya Mapato 648.9 658.5 1.5


MATUMIZI


Matumizi ya Kawaida 307.8 353.1 14.7
i) Mishahara (Mawizara) 139.6 155.5 11.39

ii) Mishahara (ruzuku) 17.7 20.8 17.5

iii) Matumz mengineyo (Wizara) 71.1 80.6 13.3

iv) Matumizi mengineyo (ruzuku) 26.6 31.2 16.9

v) Mfuko Mkuu wa Serikali (CFS) 52.8 65.0 23.1

Matumizi ya Maendeleo 341.1 305.4 -10.5

i) Mchango wa Serikali 47.9 70.0 46.1

ii) Washirika wa Maendeleo 293.2 235.4 -19.7

Jumla ya Matumizi 648.9 658.5 1.5

Chanzo: Idara ya Bajeti - ORFUMM




75. Mheshimiwa Spika, sura hiyo ya Bajeti ndiyo inayokusudiwa kutekeleza Mpango wa Maendeleo na kuendesha kazi za kawaida kwa mwaka ujao wa Fedha. Inatarajiwa kuwa utekelezaji wa Bajeti hiyo utupeleke karibu zaidi na kufikia malengo ya Mipango yetu Mikuu ya Maendeleo ikiwemo Dira ya 2020, MKUZA II, Mkakati wa Kukuza Uchumi na Malengo ya Kimataifa yakiwemo Malengo ya Maendeleo ya Milenia.


SHUKURANI


76. Mheshimiwa Spika, makadirio haya yasingeweza kuwasilishwa leo hii hapa bila ya mchango wa watu na Taasisi mbalimbali. Naomba niwashukuru wachache kwa niaba ya wengi waliochangia mafanikio ya hatua hii muhimu. Mosi, naomba nianze kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, ambae pia anaisimamia Ofisi yake hii ya Fedha, Uchumi na Mipango ya Maendeleo, Makamo wa Kwanza na wa Pili wa Rais, Wajumbe wote wa Baraza la Mapinduzi ambao ni Mawaziri na Manaibu Mawaziri wote kwa kuipitia na kuitolea Muongozo Rasimu ya Bajeti hii. Shukrani pia kwa Wajumbe wa Tume ya Mipango kwa kazi kubwa ya kuzingatia na kuridhia mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa mwaka ujao wa fedha.


77. Mheshimiwa Spika, pili, naomba kukushukuru wewe Mheshimiwa Spika, kwa uongozi wako mahiri na wa busara kwa Baraza hili. Ni kwa busara, uvumilivu na uongozi wako ndio tumeweza kuhakikisha utulivu hapa Barazani na baina ya Baraza na mihimili mingine ya Dola. Nakushukuru sana Mheshimiwa Spika. Pili, naomba nimshukuru Mwenyekiti wa Kamati ya Wenyeviti wa Kamati za Kudumu za Baraza lako, Mheshimiwa Hamza Hassan Juma kwa mchango na muongozo wa Kamati yake. Nawashukuru pia Waheshimiwa Wenyeviti wa Kamati zote za Kudumu na Wajumbe wao kwa kukaa na Wizara zote na kupitia Mapendekezo ya Bajeti zao na kuyatolea muongozo unaofaa. Kwa hakika, Mheshimiwa Spika, nalishukuru sana Baraza lako lote kwa mchango wake katika maandalizi ya Bajeti hii.


78. Mheshimiwa Spika, nje ya Baraza Mheshimiwa Spika, naomba kuwashukuru Makatibu Wakuu na Watendaji wengine wote wa Wizara na Taasisi zinazojitegemea, Mikoa, Manispaa na Halmashauri za Wilaya. Nathamini na kuushukuru pia mchango wa Sekta binafsi na Asasi zisizo za kiserikali katika maandalizi ya Bajeti hii. Vikao vingi vimefanyika na ushauri wao umesaidia sana kufikisha Bajeti katika muundo wake wa sasa.


79. Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee naomba kuwashukuru watendaji wa Ofisi ya Rais – Fedha, Uchumi na Mipango ya Maendeleo. Nawashukuru sana Katibu Mkuu ndugu Khamis Mussa Omar, Katibu Mtendaji Bi. Amina Khamis Shaaban, na Naibu Katibu Mkuu ndugu Juma Ameir Hafidh. Nawashukuru pia Kamishna wa Bajeti, Mhasibu Mkuu wa Serikali, Kamishna wa Mipango ya Kitaifa, Sera za Kisekta na Kupunguza Umaskini, Kamishna wa Ukuzaji Uchumi, Kamishna wa Fedha za Nje na Wakuu wa Idara na Watendaji wote wa Ofisi yangu kwa kazi kubwa waliyoifanya kwa umahiri na kujitolea hadi kufikia hatua hii. Ninapowasilisha Mapendekezo haya leo hii nafarijika kujua kuwa Mapendekezo haya ni matokeo ya kazi kubwa, ya umakini na ya juhudi ya pamoja ya Wasaidizi mahiri wanaofanya kazi kwa mashirikiano makubwa na kulitumikia Taifa letu kwa nguvu na uwezo wao wote.

80. Mheshimiwa Spika, naomba kuwashukuru sana Washirika wetu wa Maendeleo, nchi marafiki na Mashirika ya Kimataifa, kwa mchango wao mkubwa kwa juhudi zetu za kuwaletea maisha bora wananchi wenzetu. Kwa niaba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Wazanzibari wote, naomba kuzishukuru sana nchi zote zilizosaidia na zinazoendelea kutusaidia ili nasi tupige hatua za maendeleo. Miongozi mwa nchi hizo ni Canada, China, Cuba, Denmark, Finland, India, Ireland, Japan, Korea, Kuwait, Marekani, Misri, Norway, Oman, Sweden, Ubelgiji, Uholanzi, Uingereza, Ujerumani, Umoja wa Falme za Kiarabu na Uturuki.

81. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Mashirika ya Kimataifa, naomba kuyashukuru sana ACBF, ACRA, AfDB, AGRA, BADEA, CARE INTERNATIONAL, CDC, CHAI, CIDA, DANIDA, DFID, EGH, EU, EXIM BANK ya CHINA, EXIM BANK ya KOREA, FAO, FHI, GAVI, GEF, GLOBAL FUND, IAEA, ICAP, IDB, IFAD, ILO, IMW, IPEC, JICA, JSDF, KOICA, KUWAITI FUND, MCC, NORAD, OFID, ORIO-Netherlands, PRAP, SAUDI FUND, SAVE THE CHILDREN, SIDA, UN AIDS, UNDP, UNESCO, UNFPA, UN-HABITAT, UNICEF, UNIDO, USAID, WB, WHO, WSPA.


82. Mheshimiwa Spika, mwisho, na kwa namna maalum, naomba kwa dhati kabisa kuwashukuru sana Wananchi wote wa Zanzibar kwa imani yao kwa serikali na Watendaji wake na Baraza lako hili. Bila ya imani ya Wananchi, leo hii kazi zetu zingeweza kufanyika, bila ya utulivu wao sote tusingeweza kuwa makini na bila ya ridhaa yao, sote tusingekuwepo. Kwa mara nyengine tena, nawaomba Wananchi wote waendelee kushirikiana nasi waliotutuma kuwatumikia ili kwa pamoja tuweze kuleta maendeleo ya nchi yetu na sisi wenyewe na kizazi chetu.


HITIMISHO


83. Mheshimiwa Spika, tunaendelea kupata mafanikio katika ukuzaji wa uchumi wetu na uimarishaji wa huduma mbalimbali za jamii. Hata hivyo, lazima tubaini kuwa kazi iliyo mbele yetu ya kuleta maendeleo kwa nchi yetu na jamii yake ni kubwa sana. Tunahitaji kujituma kwa jitihada na maarifa zaidi, sote kwa pamoja, serikalini na sekta binafsi.


84. Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo, sasa naomba kwa heshima na taadhima, Baraza lako tukufu lipokee, kujadili na hatimae kuidhinisha Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo na Bajeti kwa mwaka 2013/14 kwa kuzingatia Mwelekeo wa Hali ya Uchumi. Kama nilivyosema, Bajeti ya mwaka ujao wa fedha ni Bajeti ya Huduma za Jamii kwa Wananchi wa Zanzibar. Serikali inapendekeza mbele ya Baraza lako tukufu kukusanya mapato ya Shilingi mia sita na hamsini na nane bilioni na mia tano milioni (TZS 658.5 bilioni). Serikali pia inapendekeza kutumia kiasi hicho cha Shilingi mia sita na hamsini na nane bilioni na mia tano milioni (TZS 658.5 bilioni) ikiwemo Shilingi mia tatu na hamsini bilioni na mia moja milioni (TZS 353.1 bilioni) kwa kazi za kawaida na Shilingi mia tatu na tano bilioni na mia nne milioni (TZS 305.4 bilioni) kwa kazi za maendeleo.

JUNI 12, 2013

3 comments:

Anonymous said...

Ndugu mwombaji,

i ni Bw James BILLINGS binafsi mkopo Taasisi, anayetoa mkopo katika kiwango cha chini sana riba ya 3% sisi kutoa kila aina ya mkopo kama.

Elimu ya mkopo, mkopo Biashara, mkopo nyumbani, mkopo wa Kilimo, mkopo binafsi, mkopo auto na nyingine nzuri Sababu, mimi pia kutoa mikopo

kutoka mbalimbali ya $ 5,000 USD-$ 800,000.00 USD katika kiwango cha 3% riba. Muda wa 1 - miaka 50 kulingana na kiasi unahitaji kama loan.contact nasi kupitia barua pepe:

onlinesloanservice412@outlook.com

Kindly JAZA MAOMBI YETU MFUMO NA GET BACK Marekani haraka iwezekanavyo

MAELEZO YA KWANZA'S zinahitajika NI:

1. Kamili majina:

2. anwani:

3. nchi:

4. jimbo:

5. Jinsia:

6. umri:

7. Hali ya ndoa:

8. kazi:

9. Namba ya simu:

10. Kiasi zinazohitajika:

11. Duration:

12. Madhumuni ya mkopo:

13. barua pepe:

Anonymous said...

shukrani kwa Mwenyezi Mungu kwa wema wake na wema juu ya maisha yangu nini i wamefanya kama si kwa Bibi Kate Lisa ambaye i daima kuona kama Mungu alimtuma mwanamke ambaye Mungu wamechagua kuwasaidia watu walio katika haja ya fedha kama mimi maskini mjane ambaye alikuwa short waliotajwa, na short wa fedha mwanamke ambao wana watoto wawili na ana majukumu mengi mwanamke ambaye alipoteza mume wake na ina kulipa bili yenye kodi ya nyumba na umeme bili zote mbili na ilikuwa scammed Jumla ya $ 4,000 uSD i kamwe kuamini kwamba bado kuna legit mkopo kampuni online ambao bado wanaamini kwamba watu ni katika tatizo la kifedha na tayari kusaidia baada ya kuwa scammed $ 450,000 uSD i kamwe kuamini kwamba bado kuna legit mkopo kampuni ya mpaka i alimkuta baada ya kuwa alikuwa posted na moja Bibi Luis juu ya jukwaa hiyo yeye alielezea jinsi yeye alipata mkopo wake kutoka Bibi Kate Lisa ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji Bibi Kate Lisa nyumbani mkopo na kisha i mara baada ya hakuna chaguo zaidi kuliko kujaribu bahati yangu kwa wakati wa tatu ili kuepuka kupoteza nyumba yangu (malazi ) ili i kufikiri juu yake i alikuja na hitimisho kwamba i unapaswa kujaribu tena hivyo i kuwasiliana Bibi Kate Lisa kupitia barua pepe wao walihudhuria kwangu katika chini ya 10mins i kutumika kwa ajili ya mkopo jumla ya $ 95,000,00 dola mkopo kupitishwa na ya chini kiwango cha riba na baada ya usindikaji i got mkopo wangu katika akaunti ya benki yangu jana hivyo i unataka haraka kutumia kati ya ushauri yoyote mtafuta mkopo huko nje kuwasiliana na Bibi Kate Lisa email mrskatelisaloanhome1@gmail.com yeye dhahiri kukupa mkopo unahitaji bila matatizo yoyote kwa mara nyingine tena , shukrani kwa Mungu kwa huruma yake juu ya maisha yangu. i itakuwa kuangalia mbele na kusikia ushuhuda wako mwenyewe tu kama yangu.

Bibi Sarah .

Unknown said...

Siku njema Mimi ni Mheshimiwa Alimin Muhammad muslin mkopo Taasisi, mimi ni
Mkurugenzi Mtendaji wa ALIMIN MUHAMMAD MKOPO KAMPUNI sisi kutoa mikopo binafsi na biashara kwa wale ambao mahitaji mkopo salama na hakuna kuchelewa
Yetu ni 100% kuhakikisha matatizo ya bure katika kiwango cha riba ya 3% wasiliana nasi kupitia aliminmuhammadloancompany@gmail.com
Na kupata mkopo wako leo bila matatizo yoyote
wasiliana nasi leo saa
aliminmuhammadloancompany@gmail.com