Advertisements

Wednesday, January 2, 2019

Wakazi wa Dodoma watakiwa kuchangamkia fursa ujenzi wa Mji wa Serikali

 Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Dkt Hamisi Mwinyimvua (aliyenyoosha mkono) akiangalia jinsi kazi za ujenzi wa jengo la Wizara ya Nishati unavyoendelea katika Mji wa Serikali jijini Dodoma. Wa pili kushoto ni Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga na kushoto kwa Katibu Mkuu ni Mkurugenzi wa Sera na Mipango, Wizara ya Nishati, Haji Janabi.
 Kazi za ujenzi wa jengo la Wizara ya Nishati zikiendelea katika Mji wa Serikali, Ihumwa jijini Dodoma.
Mhandisi Peter Mwaisabula kutoka Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) (wa kwanza kushoto), akitoa maelezo kuhusu ujenzi wa jengo la Wizara ya Nishati unaoendelea jijini Dodoma . Wanaosikiliza ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Dkt Hamisi Mwinyimvua (wa pili kushoto) na Wajumbe wa Kamati ya Ujenzi ya Wizara ya Nishati.



Na Teresia Mhagama, Dodoma
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Dkt Hamisi Mwinyimvua amewaasa wakazi wa Mkoa wa Dodoma kuchangamkia fursa za kazi za ujenzi zinazoendelea katika Mji wa Serikali uliopo Ihumwa jijini Dodoma.

Katibu Mkuu ameyasema hayo leo jijini Dodoma baada ya kukagua kazi ya ujenzi wa jengo la Wizara ya Nishati ambapo aliambatana na Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga, Mkurugenzi wa Sera na Mipango, Wizara ya Nishati, Haji Janabi pamoja na wajumbe wa Kamati ya ujenzi huo wakiongozwa na Katibu wa Kamati, Maseke Mabiki.

Akiwa katika eneo hilo la ujenzi, Mhandisi Peter Mwaisabula kutoka Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) amemweleza Katibu Mkuu kuwa, kazi za ujenzi zinaendelea usiku na mchana lakini kumekuwa na changamoto ya upatikanaji wa vibarua wa kutosha watakaoweza kuf anya kazi muda wote.

Ameeleza kuwa, ili kuweza kumaliza ujenzi wa jengo hilo ndani ya wakati wameagiza vibarua wengine kutoka Dar es Salaam na Arusha ili kuongeza nguvu kazi.

Kuhusu suala hilo, Dkt. Mwinyimvua  pamoja na kutoa wito kwa wakazi wa Dodoma kuchangamkia fursa hizo, ameeleza kuwa atawasiliana na Mamlaka mbalimbali ili kuweza kufanya jitihada za uhamasishaji.


Kuhusu ujenzi wa jengo hilo la Wizara, ameeleza kuwa ameridhishwa na kazi za ujenzi zinazoendelea ambapo kwa sasa NHC wamefunga taa zinazowawezesha kufanya kazi kwa masaa 24.    

No comments: