Advertisements

Wednesday, March 3, 2021

DC NTEMO -WADAU WA ELIMU WASIKAE NYUMA KUUNGA NGUVU ZAO KUTATUA CHANGAMOTO ZA ELIMU


NA MWAMVUA MWINYI,KIBAHA

MKUU wa wilaya ya Kibaha ,mkoani Pwani ,mhandisi Martin Ntemo amewataka wadau wa elimu na maendeleo wilayani humo, kuunga mkono juhudi za Serikali za kutatua changamoto za sekta ya elimu ikiwemo kuondoa upungufu wa madawati na majengo ya madarasa ,ili hali kuweka mazingira bora kwa wanafunzi.

Aidha amewaasa walimu, kufanyia ukarabati madawati yanayoharibika kwenye shule zao ili kukabiliana na upungufu wa madawati.

Akizungumza na walimu na wanafunzi wa shule za msingi Maendeleo na Maili Moja wakati wa kukabidhi madawati 250 yaliyotolewa na Halmashauri ya Mji wa Kibaha kwa shule hizo ,Ntemo alisema huu sio wakati wa kuiachia serikali pekee kutatua changamoto za elimu.

Ntemo alisema ,serikali inaendelea na mpango wa kukabiliana na changamoto za elimu ili kuhakikisha wanafunzi wanasoma kwenye mazingira magumu.

“Tunaishukuru halmashauri kwa kutoa madawati hayo ambayo yatasaidia kukabili changamoto ya baadhi ya wanafunzi kukaa chini lakini pia hakikisheni mnafanya ukarabati pale madawati yanapoharibika ili kupunguza changamoto hii,” alisema Ntemo.

Naye mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha Jenifa Omolo alieleza, halmashauri ina upungufu wa madawati 2,000 kwa shule za msingi ambapo kwenye karakana ya Iramba Furniture wametengeneza madawati 500 na karakana ya mtaji wa maskini ni nguvu zake mwenyewe wanatengeneza madawati 200.

Omolo alisema kuwa madawati yaliyosalia watayatengeneza kabla ya mwaka wa fedha kwisha Julai mwaka huu.

Kwa upande wake mwalimu mkuu wa shule ya msingi Maendeleo Mariam Mkama aliishukuru Halmashauri kwa kuwapatia madawati hayo kwani itasaidia kupunguza upungufu wa madawati hayo.

Wanafunzi wa shule hizo walishukuru msaada huo kwani madawati hayo yatasaidia kusoma vizuri na kuwa na mwandiko mzuri

No comments: