Advertisements

Friday, April 9, 2021

MHE GEKUL AOMBA USHIRIKIANO BAINA YA VIONGOZI WAKUU WA WIZARA,WATENDAJI NA WATUMISHI

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
Mhe.Innocent Bashungwa (katikati mwenye tai nyekundu) akiwa na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt Hassan
Abbasi (mwenye tai ya bluu) wakimkaribisha Naibu Waziri, Mhe. Pauline Gekul
alipowasili rasmi kwenye Ofisi yake mpya iliyopo eneo la Mji wa Serikali
–Mtumba jijini Dodoma leo, baada ya kuapishwa
na Mhe.Rais Samia Suluhu Hassan Aprili 01,2021 Ikulu ya Chamwino kushika wadhifa huo.
Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
Pauline Gekul akipokea maua kutoka kwa
wafanyakazi wa Wizara hiyo kama ishara
ya kumkaribisha rasmi kwenye Ofisi yake mpya iliyopo eneo la Mji wa Serikali –Mtumba jijini Dodoma
leo, baada ya kuapishwa na Mhe.Rais
Samia Suluhu Hassan Aprili 01,2021 Ikulu ya Chamwino kushika wadhifa huo
Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na
Michezo Pauline Gekul akisaini
kitabu cha wageni mara baada ya
kuingia kwenye Ofisi yake mpya iliyopo eneo la Mji wa Serikali –Mtumba
jijini Dodoma leo, baada ya kuapishwa na
Mhe.Rais Samia Suluhu Hassan Aprili 01,2021 Ikulu ya Chamwino kushika wadhifa huo.

Na John Mapepele, Dodoma


Naibu
Waziri wa Habari Utamaduni na Sanaa na Michezo Mhe. Pauline Philipo Gekul ameomba ushirikiano baina Viongozi Wakuu wa Wizara, Watendaji na Watumishi wote wa Wizara ili kutekeleza majukumu ya Wizara hiyo kimamilifu kulingana na Miongozo ya Serikali, Maelekezo ya Mheshimiwa
Rais na Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) hatimaye matarajio ya wananchi yaweze kufikiwa.

Mhe.Gekul ameyasema haya alipowasili rasmi leo kwenye Ofisi yake mpya eneo la Mji wa Serikali- Mtumba jijini Dodoma mara baada ya kuteuliwa na Mheshimiwa Rais kwenye nafasi hiyo hivi karibuni akitokea Wizara ya Mifugo na Uvuvi ambako alikuwa akihudumu kwa nafasi hiyohiyo.

“Mheshimiwa Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara, madaraka haya tuliyopewa ni sawa na makoti ya kuazima hivyo tuna kila sababu ya kumtanguliza Mungu na kuimarisha ushirikiano ili kuleta matokeo tarajiwa kwa wananchi wetu wakati tunatekeleza majukumu yetu ya kila
siku” amesisitiza Mhe. Gekul

Amemshukuru Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kumwamini na kumrejesha tena kwenye nafasi hiyo pamoja na viongozi wote Wakuu wa
Wizara hiyo ambapo ameongeza kuwa hali hiyo itarahisisha utekelezaji wa majukumu ya Wizara kwa ufanisi kwa kuwa watendaji wote wamerejeshwa na wanauzoefu wa kutosha.

Amemhakikishia Waziri Bashungwa kufanya kazi kwa bidii ya kumshauri na kumsaidia kwa kadiri ya uwezo wake wote kama msaidizi wake.

Kwa upande wake, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Innocent Bashungwa amesema Watumishi wote kuwa na mshikamano wa hali ya juu ambapo amesisitiza watumishi
wasisubiri kusukumwa na Katibu Mkuu na badala yake wachape kazi ili kukidhi dhamira ya Mhe. Rais ya kuwatumikiwa wananchi kikamilifu.

“Napenda kusema tukigundua mahali popote kwenye Wizara yetu hakuna ushirikiano
tutachukua hatua mara moja maana hiyo itakuwa ni hujuma kwa taifa”amefafanua Mhe. Bashungwa

Amemshukuru Mhe. Rais Samia kwa kumwamini na kumteua tena kuendelea kusimamia Sekta zilizo chini ya Wizara hiyo pia kumteua Mhe. Gekul kuja kuongeza nguvu katika kutekeleza
na kumuahidi kuendelea kufanya kazi kwa bidii na weledi ili kutekeleza Ilani ya CCM na hotuba aliyoitoa awali kama mwongozo kwa Watendaji wote wa Serikali.

Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. Hassan Abbasi amemshukuru Mhe.Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwa kumwamini na kumteua kwa mara nyingine kuwa Katibu Mkuu na kumwahidi kushirikiana na Viongozi na Watumishi wote kutekeleza majukumu ya Wizara kwa weledi
na kuzingatia taaluma.

Akizungumza kwenye Kikao cha Menejimenti ya Wizara hiyo mara baada ya kupokea maelekezo ya Waziri Bashungwa, Dkt. Abbasi amesisitiza watendaji wa Wizara kutoka na kuwa jirani na wadau
wa sekta zilizochini ya Wizara hiyo kwa kuwa wanahitaji kulelewa kwa karibu.

Amesema jukumu la Wizara ni kuzisimamia sekta zilizo chini ya wizara hiyo kikamilifu kwa weledi ili kupata matokeo chanya kwa kuwa nchi yetu imebahatika kuwa na wasanioi wenye vipaji na vipawa
vingi kinachotakiwa ni usimamizi madhubuti.

No comments: