Tuesday, May 3, 2011

Kamanda wa Polisi mkoani Kilimanjaro, Lucas Ng`hoboko

Mkazi wa Sanya Juu, Wilaya ya Siha, mkoani Kilimanjaro, Narcis Massawe (43), amejiua kwa kujichanachana na vipande vya wembe baada ya kukuta nyumba yake ya biashara imewekwa alama ya X ikimaanisha imejengwa mahali pasipotakiwa na inatakiwa kubomolewa.

Tukio hilo lilitokea usiku wa kuamkia Aprili 30, mwaka huu, eneo la
Sanya Juu mjini, ambapo mfanyabiashara huyo anaemiliki nyumba yenye zaidi ya vyumba 10. Vyumba sita ndivyo vilivyowekewa alama hiyo.
Taarifa kutoka eneo la tukio zilizothibitishwa na Kamanda wa Polisi mkoani Kilimanjaro, Lucas Ng’hoboko, zilisema kuwa mtu huyo alikuwa safarini kwa muda mrefu na kwamba alifika kwenye nyumba yake Aprili 29, mwaka huu.
Ng’hoboko alisema baada ya kufika alikuta vyumba sita vimewekewa alama hiyo na maofisa wa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) Mkoa wa Kilimanjaro, ambao walipita eneo hilo kati ya Aprili 23 na 24, mwaka huu.
Taarifa hizo zilieleza kuwa awali eneo la baraza la nyumba hiyo ndilo liliwekewa alama hiyo, lakini baada ya siku kadhaa maofisa wa Tanroads walirudi tena na kuweka alama kwenye vyumba hivyo kwa madai kuwa imejengwa katika eneo la hifadhi ya barabara.
CHANZO: NIPASHE

No comments: