Friday, August 31, 2012

Mamia wamuaga Askofu Katoliki

Mapadri wakiteremsha kutoka kwenye ndege mwili wa MarehemuMhashamu Askofu  Pascal William Kikoti wa Mpanda  wakati ulipowasili kwenye uwanja wa ndege  wa Mpanda, Agust 30, 2012. 
(Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).
MHASHAMU Askofu wa Jimbo Kuu la Mwanza Yuda Thadei Ruwaichi, jana aliwaongoza waumini wa madhehebu  ya Kikristo katika misa ya kumuaga marehemu Askofu Paschal Kikoti wa Jimbo la Mpanda iliyofanyika katika Kanisa Kuu la Epiphania jimbo la Bugando.
 
Akiongea katika ibada hiyo,Askofu Ruwaichi aliwataka waumini wa dini na wale wasiokuwa waumini kuishi katika uaminifu na kutokuwafanyia watu wengine mambo mabaya.
 
Alisema uaminifu huo usiwe kivuli cha kukinga maovu ambayo mtu anayafanya, na kuongeza kuwa  mungu yupo na anaona kila kitu ambacho binadamua anakifanya duniani.
 
Kadhalika Askofu Ruwaichi aliwataka waumini wa dini hiyo kujiuliza maswali ambayo yatatoa tafakari ya maana ya maisha yao,  hasa kwa mkristo na kuwataka kuwa tayari kwa sababu hawajui siku wala saa ambayo mauti itawakuta.
 
“Mungu ana siri kubwa kwa wanadamu, na huwa inajidhihirisha kidogo kidogo katika mtiririko wa matukio ambayo yanawakuta binadamu,  kwa mtazamo huo binadamua tunatakiwa kuishi kwa ushuhuda na kufanya matendo yaliyo mema”alisema Askofu Ruwaichi.
 
Aliwataka waumini hao kuwaombea maaskofu kwa sababu wanabeba mzigo mkubwa wenye mateso ili wasiweze kukata tamaa ya kuwatumikia.
 
Alisema  maaskofu wanahitaji ushirikiano mkubwa kwa waumini wao kutokuna na kazi kubwa wanayoifanya ya kuhumia kanisa pamoja na watu wake.
 
Marehemu Paschal Kikoti alifariki usiku wa kuamkia juzi akiwa na umri wa miaka (55)  katika Hospitali  ya Rufaa ya Bugando alipokuwa amelazwa kwa ugonjwa wa shinikizo la damu.
 
Taarifa za awali kutoka  hospitali hiyo  zilidai  marehemu askofu alifikishwa hospitalini hapo usiku saa mbili siku ya Jumapili akitokea jimboni kwake ambapo alikuwa akitumikia.
 
Kwa mujibu wa taarifa hizo, ugonjwa huo wa shinikizo la damu ulisababisha askofu kuanguka bafuni wakati akioga na hatimaye kumsababishia ugonjwa wa kiharusi.

No comments: