Advertisements

Wednesday, May 8, 2013

Pinda aagiza vyuma vinavyotolewa kwa waathirika wa bomu visitupwe



Waziri Mkuu Mizengo Pinda, ameagiza madaktari wanaofanya upasuaji kwa majeruhi wa bomu lililolipuka katika Kanisa la Mtakatifu Josef Mfanyakazi, Parokia ya Olasiti, kuweka vizuri vipande vya vyuma wanavyovikuta na kukabidhi kwa wataalam serikalini.Amesema hiyo itasaidia kubaini kama bomu hilo lilitengenezwa kienyeji ama viwandani.

Pinda aliyasema baada ya kuwatembelea majeruhi wa tukio hilo katika Hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mount Meru jana.

Pinda, alikuwa amefuatana na Waziri Mkuu mstaafu, Edward Lowassa, Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Goodluck Madeye na baadhi ya wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).


Aidha, alimwagiza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Frida Mokiti, kuwasiliana na Ofisi ya Hifadhi za Taifa (Tanapa) na wadau wengine kushirikiana kwa pamoja kujenga wodi ya daraja la kwanza.Pia alimwagiza Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, kuhakikisha anafikisha agizo hilo kwa Tanapa ili ujenzi ufanyike na Kitengo cha Uangalizi Maalum (ICU) cha kisasa.

Aidha, Pinda, aliipongeza Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kuchukua hatua za haraka za kutoa msaada wa dawa na vifaa vyote vinavyotakiwa vyenye thamani ya Sh. milioni 23.3.Kadhalika, Waziri Mkuu, alivipongeza vyombo vya habari kwa kutangaza tukio hilo kwa uhakika bila kupotosha na kuwezesha umma kufahamu ukweli.

Kwa upande wake, Waziri Mkuu mstaafu, Lowassa, alipongeza pia vyombo vya habari kwa kutangaza tukio hilo bila kupotosha na kuipongeza serikali na Jeshi la Polisi kwa kufanya uchunguzi kwa haraka  na kuliomba liendelee ili ukweli ubainike na uwekwe wazi.

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Nyalandu,
alikabidhi msaada wa dawa na vifaa mbalimbali vya kuhudumia majeriuhi hao.Pia aliahidi kukutana na wadau wa utalii wakiwamo wafanyabaishara, ili waone msaada gani zaidi watautoa kwa majeruhi hao.

Naye Mkuu wa Mkoa Arusha, Magesa Mulongo, alisema kati ya majeruhi 66 waliokuwa wamelazwa hospitalini hapo, 24 wameruhusiwa kurejea majumbani baada ya kupata nafuu na
41 bado wanaendelea na matibabu.
 
CHANZO: NIPASHE

2 comments:

Anonymous said...

Mimi siasa za bongo zinanipa tabu kidogo - sasa na hili nalo linasubiri Waziri Mkuu atoe maagizo? Si vyombo vya usalama na wataalamu wa uchunguzi wa uhalifu wa jinai walitakiwa kuwa wameliweka katika 'to do list' yao? Au ni ile tu ionekane na WM ametoa agizo!!??

Anonymous said...

kasheshe bongo land kasheshe watu wanajua wakifanyacho msiwaone wajinga hawa