Advertisements

Monday, July 8, 2013

UMOJA WA MATAIFA WAJADILI PENGO KATI YA WALIONACHO NA WASIO NACHO

  Katibu Mkuu wa Umoja wa  Mataifa akifungua majadiliano ya siku moja kuhusu kukosekana kwa fursa sawa katika jamii na hivyo kufanya pengo kati ya walionacho na wasionacho kuongezeka hali ambayo amesema kama hujudi za makusudi  hazitachukuliwa  pengo hilo na tofauti  hizo katika jamii zinaweza kuwa chimbuko kubwa la  migogoro, machafuko, milipuko ya magonjwa uhalibifu wa mazingira na kudhoofu kwa maendeleo.
Sehamu ya wajumbe walioshiriki majadiliano ya siku moja kuhusu pengo kati ya walionacho na wasionacho majadiliano hayo yamefanyika siku ya jumatatu hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, New York. 
Na Mwandishi Maalum
Baraza  Kuu la Umoja wa  Mataifa jana  jumatatu lilikuwa na  majadiliano    juu ya kukosekana kwa usawa wa kiuchumi na kijamii  kati ya mtu na mtu,   na baina ya nchi na nchi na adhari zake kwa mstakabali  wa amani, usalama na maendeleo endelevu.
Majadiliano  hayo ya siku  moja  yaliandaliwa na Rais wa Baraza Kuu Bw Vuk Jeremic  na kufunguliwa na  Katibu Mkuu Ban Ki Moon, yaliwahusisha   baadhi ya mawaziri kutoka nchi kadhaa, wakuu wa Mashirika yaliyo chini ya Umoja wa Mataifa,  Jumuiya za  Kikanda  pamoja na  Asasi zisizo za kiserikali. 
Akifungua majadiliano hayo, Katibu Mkuu amesema,  licha ya kuwapo kwa mafanikio   kadhaa katika upatikanaji wa huduma  za kijamii, kama vile afya, elimu,  maji safi na  salama  kupitia utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo ya Millenia ( MDGs). Bado pengo kati ya walionacho  na wasio nacho ni kubwa na linaendelea kukua.

Kwa mfano, anasema, katika miaka michache  iliyopita jumuiya ya kimataifa imeshuhudia ongezeko la idadi ya  watoto wanaokwenda shule hasa watoto wa kike,  kupungua kwa vifo vya wanawake wajawazito na watoto wachanga, na  vita dhidi ya magonjwa  kama vile malaria,  maambukizi ya ukimwi na kifua kikuu.
Mafanikio mengine ni pamoja na  kuboresha maisha ya watu milioni 200 wanaoishi katika makazi duni  , huku watu milioni mia sita wakiondolewa kutoka katika umaskini  wa kupindukia.
Hata hivyo anasema  Ban Ki Moon. “ Lakini mafanikio haya na mengine mengi  hayana uwiano uliosawa   ndani ya mataifa mbalimbali na  baina ya taifa moja na jingine.  Mataifa  mengi, tajiri na maskini yanashuhudia ongezeko la ukosekanaji wa usawa wa  kiuchumi na kijamii”.
Akasisitiza kwa kusema   sura ya  pengo hilo la  usawa  katika maeneo kwa vile afya na elimu  inajionyesha  dhahiri   kati ya kaya za matajiri na maskini.
Ban Ki Moon anasema idadi kubwa ya watu  wanaoishi katika mazingira magumu wengi wao wana kiwango kidogo cha elimu, au elimu yao ni duni inayowakosesha ujuzi  na uwezo   wa kushindana katika soko la leo la ajira.
Kama hiyo haitoshi  Mkuu huyo wa Umoja wa Mataia, ameeleza pia kwamba,  pengo la ukosefu wa fursa za  kiuchumi na kijamii pia linaongezeka sana kati ya maeneo ya mijini  na yale ya vijijini. Akatoa mfano kwa kusema  zaidi ya watu 2.6 bilioni ambao hawana huduma za usafi wa mazingira na maji taka  wengi wao wanaishi maeneo ya vijijini.
Akatahadharisha kwa kusema,   kukosekana kwa usawa wa kiuchumi na  kijamii  kuna weza kuwa   chimbuko la    uhalifu, milipuko ya magonjwa, uharibifu wa mazingira na kudhoofisha ukuaji wa uchumi na maendeleo.
Ban Ki Moon  anasema   ndio maana  suala la usawa limekuwa moja ya  nguzo  muhimu katika majadiliano  yanayoendelea hivi sasa juu ya  mwelekeo wa ajenda ya maendeleo baada ya 2015.
Akasema  kunahitajika mikakati madhubuti na mageuzi makubwa ili kuikabili changamoto hii ya kupunguza pengo la ukosefu wa usawa.
 Anataja baadhi ya mabadiliko na mikakati hiyo kuwa   ni pamoja na   kutafuta ufumbuzi wa mgogoro wa kiuchumi na kifedha na kuendelea na juhudi za kutokomeza umaskini uliokidhiri na njaa.
Akasisitiza pia umuhimu wa kuongeza  uwekeza zaidi  katika afya elimu, ulinzi wa jamii, ajira za uhakika  hususani kwa vijana na  uwezeshwaji wa wanawake katika maeneo yote.
Kuhusu ajira Katibu Mkuu  anaeleza kuwa  zinahitajika ajira  mpya milioni 470  kati ya mwaka 2014 na 2030.
Baadhi ya washiriki wa majadiliano hayo akiwamo Rais wa Baraza Kuu, Bw. Vuk Jeremic walisisitiza  haja na umuhimu wa nchi kushirikiana katika kutafuta mbinu muafaka za kupunguza pengo kati ya walionacho na wasionacho. Washiriki hao pia  walielezea juhudi mbalimbali zinazochukuliwa na serikali zao katika kukabiliana na changamoto hiyo.

No comments: