Advertisements

Saturday, August 30, 2014

Uraia pacha waota mbawa Serikali yauzima, yazua hofu

MATUMAINI ya Watanzania waishio nje ya nchi kupata uraia pacha yameota mbawa baada ya serikali kuweka bayana kuna athari kubwa za kiusalama.
Licha ya sababu hiyo ya serikali kutotaka liwemo kwenye Katiba mpya, suala hilo limewagawa wajumbe wengi wa Bunge Maalum kwa misingi ya kisiasa na kiuchumi.

Mgawanyiko huo ulijitokeza zaidi katika kamati mbalimbali zilizokuwa zikijadili Rasimu ya Katiba, kiasi cha kumfanya Mwenyekiti wa Bunge Maalum, Samuel Sitta, kuunda kamati ya watu 10 kulishughulikia.

Sitta, pia aliagiza watalaamu wa Uhamiaji, watoe semina kwa wajumbe ambayo ilifanyika jana na kuzusha mgawanyiko mkubwa.

Katika semina hiyo, watoa mada walikuwa ni Katibu Mtendaji, Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango, Dk. Philip Mpango na mtendaji mwandamizi kutoka Idara ya Uhamiaji, waliyopinga Watanzania wenye uraia pacha kushiriki siasa.

Wataalamu wa uhamiaji, walisema kama Tanzania itaridhia suala hilo litaondoa uzalendo na litahatarisha amani.

Hata hivyo, katika kile kilichowashangaza wajumbe wengi, serikali haikuwaleta wataalamu wanaohusika na uraia pacha wanaofanya kazi katika Idara ya Uhamiaji.

Inadaiwa kuwa, hofu ya serikali ni kuwa Mtanzania atakapopewa uraia pacha, anaweza kufanya uhalifu hapa nchini na kukimbilia nchi nyingine aliko na uraia wake na hivyo kuweka mazingira magumu ya kumkamata.

Hofu nyingine iliyotolewa na wajumbe wengi hasa wa Zanzibar, ni kuwa baadhi ya watu waliokimbia hapa nchini wakati wa Mapinduzi mwaka 1964, wanaweza kurejea na kuchukua uongozi kama uraia pacha utaruhusiwa.

Hata hivyo, Mjumbe wa Bunge hilo anayewakilisha Watanzania walio nje ya nchi, Kadari Singo, alisema suala la uraia pacha limeshakwama.

Singo, alisema kauli za Makamishna wa Uhamiaji waliotoa mada kwa wajumbe, inaonyesha serikali haitaki Watanzania kuwa na uraia zaidi ya nchi moja.

Alisema sababu za kuwa Watanzania walio nje ya nchi wakipewa uraia pacha hawatakuwa na uzalendo na watahatarisha usalama wa nchi ni nyepesi.

Singo, alisema msimamo huo wa serikali ni mwiba kwa Watanzania waishio nje ya nchi wapatao milioni moja, waliyotegemea uraia pacha utaingizwa kwenye Katiba mpya.

Alisema serikali ilifanya hila za kuwatumia makamishna wa Uhamiaji, kwa kueleza hasara za uria pacha bila kueleza faida zake.

“Nimesikitishwa sana na dhamira ya serikali, kwani imetoa mada yenye mlengo mmoja tu hivyo kuwanyima fursa wajumbe kujua faida za uraia pacha,” alisema.

Alisema uraia pacha una faida kubwa na nchi nyingi zinanufaika na utaratibu huo, ambapo fedha zinatoka nje na kuendeleza nchi husika.

Singo, alisema kutokana na hatua hiyo, Watanzania wengi watanyimwa fursa ya kushiriki kuinua uchumi wa nchi yao kikamilifu, kutokana na kutotambuliwa kisheria.

Alifafanua kwamba katika nchi za Kenya, Uganda na Rwanda, zinanufaika na utaratibu huo, ambako raia wake wanaingiza fedha nyingi nchini mwao kwa ajili ya maendeleo.

Singo, alisema uraia pacha unafungua njia kwa kurejesha rasilimali kwa wingi nchini na kulikomboa Taifa na tatizo la ajira.

Aliongeza kuwa, utafiti usio rasmi unaonyesha Watanzania walio nje wanarejesha nchini kati ya dola milioni 10 na 37 za Marekani.

Alitaja mfano wa manufaa katika nchi nyingine ni China inayonufaika na dola bilioni 60 za Marekani kutoka nje kila mwaka, Nigeria dola bilioni 20, Kenya inavuna dola bilioni 1.7.

Hata hivyo, alikiri kuwepo utata wa takwimu za Watanzania wanaoishi nje ya nchi kutofautiana, na kulingana na vyanzo vyake, alifafanua kwamba Benki ya Dunia inataja wako milioni 3, mwenyewe Singo, alikadiria kati ya milioni 1 na milioni 1.5.

Aliongeza kuwa Tanzania ni kati ya nchi nane pekee za barani Afrika ambazo hazijaingia katika mfumo wa uraia pacha, lakini inaathirika kupitia kuwapa uraia watu kutoka nchi nyingine zenye mfumo huo, akitoa mfano wa Rwanda.

Alisema kama ni dhana ya uzalendo iwapo inapatikana kwenye tabia binafsi ya mtu au mahali atokapo, akieleza imani yake ni kwamba tabia binafsi inatathimini uzalendo na si vinginevyo.

Singo, alishauri pamoja na kuwepo mifumo mingi ya uraia pacha, Tanzania bado inaweza kubuni mfumo unaoendana na mazingira yake ili kuwa na unaoendana na mazingira yake.
CREDIT:MTANZANIA

7 comments:

Anonymous said...

Sasa kwa nini mnafungua matawi ya CCM ughaibuni? It's westing our time .

Anonymous said...

What is next??. Pengine hao mawaziri na wabunge wana uraia wa nchi nyengine.

Anonymous said...

Its because some politicians don't want us back and take over. Chuki tuu that's all.

Anonymous said...

Hata hivyo .....kuna usalaama sasa ?

Anonymous said...

Hivi mnaotaka dual citizenship kitu gani sana kinawafanya mng'ang'anie sana hiyo issue?
Unang'ang'ania uraia pacha kwani yule aliyeko nje amekosa nini hasa? Na sisi washamba wa bongo wenye akili ya kiafrika tumekosa nini toka kwenu? Naangalia chapisho hapa mpaka nacheka. Kumbe kuna watanzania zaidi ya milioni tatu wanaoishi nje ya nchi. Andiko linasema mwaka 2013 hawa watanzania waliingiza kama dola milioni 75 tu (Tuseme walikosea, labda ni dola milioni 750). Wenzetu waKenya waliingiza dola bilioni 1.4, na Waganda wakaingiza dola bilion 1. Sasa huoni hata aibu. Ina maana kila mtanzania aliyeko nje aliingiza dola 25 (kama ilikosewa basi tuseme 250). Ni kiasi kidogo sana mpaka muombe kuwa special.
Sasa ninyi kipi chawazuia kuleta pesa zenu hapa Tanzania? Kenya kabla haijawa na dual citizenship ilikuwa inaingiza hadi dola bilion 2. Sasa sijui imeshuka baada ya watu kupata dual citizenship au la, lakini unaona pesa wanayoingiza inaweza endesha wizara moja.
Kwa ufupi watu wetu walioko nje hawana chochote kile. Halafu msijifanye ninyi tu ndio mmeishi nje. Sisi pia tumesoma huko miaka na miaka. Na tunaenda tukipata nafasi. Tunajua tofauti kubwa kati ya mtanzania na mataifa mengine. Watanzania wengi waliopo nje si intellectuals wala si wafanyabiashara. Walipaswa kuwa peasants.Ni wanafiki sana na ni wabangaizaji tu waliokimbia maisha bongo wakidhani nje ni mteremko.
Watanzania waache wapige mapicha New York, London, kwenye parties, show za diamonds na ku post facebook na Instagram. Lakini suala la kusaidia uchumi ni zero. Hata kutetea hoja tu ya uraia pacha hawawezi.
Uraia pacha hauna umuhimu kwa taifa la sasa. Hela mnayoingiza ni sawa na mapato ya mfanyabiashara mmoja. Haina athari katika uchumi wetu. Hebu tupisheni hapa.

Anonymous said...

Hahaha mshkaki umemaindi sana naona unaua tu umaonesha ww ni mkereketwa lakini kumbuka intelectual or not hao unaowakandia wanaprovide kwa families zao kiasi kikubwa wakaweza kucreate businesses ..kitu ambacho government imeshindwa kufanya..usiwe narrow minded mshkaji.

Anonymous said...

ni vizuri pia ujue ni wakenya wangapi au waganda wangapi wako enje ya nchi zao,watanzania walio nje hawafikii hata robo moja ya hayo mataifa uliyoyataja,sio tu ukimbilie bilion zao