Advertisements

Monday, November 24, 2014

MINOTI YA ESCROW INAUMA SANA!

Stori: Ojuku Abraham wa GPL
THIS is not fair (Hii siyo sawa)! Tunaweza kufumba macho na kuacha kusema kinachoendelea katika baadhi ya ‘madudu’ serikalini, lakini linapokuja suala la uchotwaji wa Sh. bilioni 306 za umma kutoka Akaunti ya Tegeta Escrow, tuache masihara, minoti hiyo iliyoibwa na wajanja wachache, inauma sana, Ijumaa Wikienda
linakudadavulia zaidi.

KWANZA ESCROW NI NINI?
Tunajua wengi wanafahamu kinachoendelea kuhusu Escrow ambapo sasa limekuwa gumzo ndani ya bunge na kwenye mijadala mbalimbali ya wananchi wa kada tofauti lakini si vibaya tukaijua zaidi kwani inadaiwa sakata hilo linampa wakati mgumu Rais Jakaya Mrisho Kikwete.

Akaunti ya Tegeta Escrow ilifunguliwa na serikali ili kuhifadhi fedha za umma baada ya Shirika la Ugavi wa Umeme Tanzania (Tanesco) kuingia mkataba wa kununua nishati ya umeme kutoka Kampuni ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL) mapema miaka ya 2000.
Baadaye Tanesco iligundua kwamba, bei ya umeme wanayouziwa na kampuni hiyo ni kubwa, hivyo walikwenda kuipinga katika mahakama ya kibiashara.

ILIVYOFUNGULIWA SASA

Wakati mvutano huo ukianza, ndipo serikali ilifungua akaunti hiyo kwenye Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ambako Tanesco iliweka fedha ilizokuwa ikizilalamikia kwa ajili ya kuilipa IPTL kama tozo ya umeme (capacity charges) hadi hapo mahakama itakapotoa uamuzi juu ya kama kweli bei hiyo ilikuwa halali kwa Tanesco au la!

WAJANJA WAZICHOTA
Lakini wakati shauri hilo likitua kwenye Mahakama ya Kimataifa ya Utatuzi wa Migogoro ya Kibiashara (UCSID) na uamuzi ukiwa bado haujatolewa, inadaiwa Wizara ya Nishati na Madini iliidhinisha fedha hizo zitolewe BoT na kulipwa Kampuni ya PAP ambayo ilishainunua IPTL, wizara ilidaiwa kuamini Tanesco wangeshindwa kesi hiyo.
Hukumu ilipotoka, Tanesco waliibuka na ushindi na kutakiwa kulipwa fedha kibao lakini walipokwenda kuchungulia kwenye akaunti walikuta hakuna kitu, sakata likaanzia hapo sasa.

NI FEDHA NYINGI KIASI GANI?
Kwa utafiti uliofanywa na gazeti hili, shilingi bilioni 306 ni fedha nyingi kiasi kwamba kama zikipangwa katika chumba chenye ukubwa wa futi 10 kwa 10, vitahitajika vyumba viwili vilivyojaa kuanzia chini hadi juu pasipo na pangaboi.

INAUMA JAMANI

Kama hiyo haitoshi, hesabu zinaonesha, endapo kijana mwenye umri wa miaka 18 sasa, aliyemaliza elimu ya kidato cha nne na yupo tayari kuanza maisha, akipewa sehemu ndogo tu ya fedha hizo halafu akafanya matumizi ya kufuru bila kufanya kazi wala biashara yoyote, ataweza kufa akiwa na miaka 75 huku akibakisha chenji kubwa.
Kwamba, endapo kijana huyo atatumia shilingi laki tano (500,000) kila siku (watumishi wengi wa serikali wanalipwa chini ya kiwango hiki) kwa mwaka mzima wenye siku 365, atakuwa ametumia shilingi milioni 182.5 tu!

UFAFANUZI WAKE
Maana yake ni kwamba hadi atakapofikisha umri wa miaka 75, ikiwa ni miaka 57 tangu aanze kutumbua fedha hizo akiwa na miaka 18, atatumia shilingi bilioni 10.4 tu, sawa na asilimia chini ya sifuri ya mabilioni hayo ambayo baadhi ya wakubwa ‘wamejisevia’. Kweli inauma sana!

WABUNGE WALIOICHARUKIA

Kashfa hiyo imeshikiwa bango na wabunge karibu wote wa kambi ya upinzani na baadhi kutoka Chama cha Mapinduzi (CCM), ingawa wanaoonekana kuwa vinara ni pamoja na Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila ambaye ndiye aliyeibua kashfa hiyo.
Kafulila, ambaye Jumamosi iliyopita alifunga ndoa nyumbani kwao Kigoma, alisababisha purukushani kubwa ndani ya bunge alipoibua sakata hilo kiasi cha kutaka kupigwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema.

KINA NANI KIKAANGONI?

Sakati hili limewakalia vibaya baadhi ya vigogo serikalini, akiwemo Waziri Mkuu, Mizengo Pinda anayedaiwa kutumika ili kuifunika ripoti ya CAG isijadiliwe bungeni, Waziri wa Nishati na Madini, Sospeter Muhongo, Katibu Mkuu wake, Eliakim Maswi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Frederick Werema, Gavana wa Benki Kuu, Benno Ndullu na Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi, Anna Tibaijuka.
Wengine wanaohusishwa na kashfa hiyo baada ya kubainika kupewa mgao wao kupitia kwa mmoja wa watuhumiwa ni pamoja na waziri wa zamani wa Nishati na Madini, William Ngeleja na Mwanasheria Mkuu wa serikali wa zamani, Andrew Chenge.

KITAELEWEKA KESHOKUTWA
Hatima ya vigogo wanaotuhumiwa kuchota mabilioni hayo ya fedha inatarajiwa kujulikana Novemba 26, mwaka huu (keshokutwa) wakati ripoti ya uchunguzi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) itakapopiga hodi bungeni na waheshimiwa kuanza kuijadili.

No comments: