Advertisements

Monday, January 26, 2015

SEHEMU YA MPANGO WA KUENDELEZA MICHEZO WA MAKAMBA, HUU HAPA

Mbunge wa Bumbuli na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Habari na Masoko ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) ambaye hivi karibuni ametangaza nia ya kugombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa January Makamba, ameweka wazi shauku yake ya kuinua kiwango cha michezo nchini.
Makamba ambaye ni miongoni mwa wanasiasa wenye mvuto mkubwa kwa vijana nchini, aliweka wazi nia yake hiyo katika mazungumzo yake na Padre Privatus Karugendo ambayo yamechapishwa katika kitabu ambacho gazeti hili limepata nakala yake.
Mbunge huyo amesema anataka kujenga vituo vya michezo vya kanda vyenye hadhi ya olimpiki.
“Inafedhehesha sana kuona kwamba asilimia 79 ya Watanzania walikuwa hawajazaliwa mara ya mwisho tumeshiriki katika fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika.
“Mwaka huohuo wa 1980, ndiyo ilikuwa mara ya kwanza na ya mwisho tuliweza kushinda medali za Olimpiki. Rafiki yangu mzee Suleiman Nyambui na mzee wetu Filbert Bayi ndiyo walitutoa kimasomaso kipindi kile. Ni muhimu kurekebisha hili,” alisema Makamba katika kitabu hicho.
Kama mgombea wa kwanza kutangaza nia yake ya kugombea urais katika uchaguzi mkuu wa Oktoba, mwaka huu, Makamba anaungwa mkono na vijana wengi kutokana na kuendesha siasa zake kisasa, kibunifu na kuepuka malumbano ya jukwaani.
Makamba anakuwa mgombea wa kwanza wa urais kuweka bayana mipango yake ya Tanzania Mpya katika maandishi.
“Tufikie wakati ambapo timu za taifa za miaka 10 ijayo ziwe zinaandaliwa kuanzia sasa na serikali itenge bajeti kila mwaka kwa timu hizo ili kuziwezesha kukaa kambini, kufanya mechi za majaribio na kuziwezesha kushiriki kikamilifu katika mashindano ya kimataifa,” alimalizia Makamba alipokuwa akigusia mpango wake wa kuinua michezo nchini. 
Source Saleh Jembe

No comments: