Advertisements

Friday, February 20, 2015

Wapinga Makonda kuwa DC.

Wasomi, wanasiasa na wanaharakati nchini, wamepokea kwa hisia tofauti uteuzi alioufanya na Rais Jakaya Kikwete, wa wakuu wa wilaya wapya, huku baadhi wakikosoa uteuzi wa mkuu mpya wa wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda na wengine wakiunga mkono.

Juzi Rais Kikwete aliteua wakuu wa wilaya wapya 27, akiwamo Katibu wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Uhamasishaji na Chipukizi, Makonda, kuwang’oa 19 na kuwahamisha 64.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na NIPASHE jana, badhi walisema Rais Kikwete amefanya jambo la busara kuboresha utendaji kazi serikalini, lakini wakasema kumpa Makonda wadhifa huo kunaweza kudhoofisha utendaji wa kazi katika wilaya ya Kinondoni.

PRO. BAREGU
Aliyekuwa mjumbe wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Prof. Mwesiga Baregu, alisema Makonda alituhumiwa kumfanyia fujo aliyekuwa Mwenyekiti wa tume hiyo, Jaji Joseph Warioba, lakini hakuna hatua zozote zilizochukuliwa dhidi yake.

Kutokana na hali hiyo, alisema ni jambo la kushangaza kuona mtu mwenye tuhuma za kufanya fujo anateuliwa kuwa mkuu wa wilaya, ambaye atakuwa mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya.

“Hakuna uchunguzi wa polisi au kiusalama juu ya Makonda. Kutochukuliwa hatua kunadhihirisha mambo aliyoyafanya aliagizwa,” alisema Prof. Baregu.

Alisema uteuzi huo wa wakuu wa wilaya wapya unaweza ukawa kinga kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kujiimarisha katika uchaguzi mkuu na kura ya maoni za katiba inayopendekezwa.

MUKOBA
Rais wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Gratia Mukoba, alisema Rais Kikwete amefanya kitendo kizuri kuteua wakuu wa wilaya, lakini akasema kitendo cha kumpa Makonda ukuu wa wilaya ya Kinondoni siyo chema.

Alisema Makonda amepewa wilaya kubwa na hana uzoefu wowote wa kuongoza wilaya, kwani hajawahi hata kuongoza kata.

Mukoba alisema yawezekana Rais Kikwete amemteua Makonda kutokana na fujo anazozifanya, ikiwamo inayodaiwa kumfanyia Jaji Warioba.

“Sijawahi kumsikia akiongoza hata kata. Sana sana amewahi kuongoza Tahliso (Umoja wa Wanafunzi wa Vyuo vya Elimu ya Juu). Mtoto mdogo kama yule kumfanyia fujo mzee kama yule aliyeliletea sifa taifa na leo anakuwa mkuu wa wilaya ni jambo la kushangaza sana,” alisema Mukoba.

DK. BANA
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk. Benson Bana, alisema uteuzi wa wakuu wa wilaya ni mzuri, kwani rais ndiye mwenye mamlaka ya uteuzi.

Alisema japokuwa muda ni mdogo uliobaki wa kiutendaji wa kazi kwa wakuu hao wa wilaya wapya, changamoto kwao ni kuhakikisha mafanikio yanapatikana kwa wakati.

Dk. Bana alisema nafasi ya ukuu wa wilaya ni ya kisiasa zaidi, hivyo CCM wanajipanga kwa uchaguzi mkuu ujao.

KIJO-BISIMBA
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Hellen Kijo-Bisimba, alisema uteuzi huo wa wakuu wa wilaya wapya, CCM wanaweka makada wao mapema ili kujipanga na uchaguzi mkuu pamoja na kura ya maoni.

Alisema kulikuwa hakuna sababu ya Rais Kikwete kuweka wakuu wapya wa wilaya wakati muda wa kumaliza uongozi wake umebaki mdogo.

RAIS TLS
Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Charles Rwechengura, alisema Rais Kikwete anapaswa kupongezwa kwa uteuzi huo, kwani amefuata vigezo vya uteuzi wa wakuu wa wilaya, hivyo kumteua Makonda kuwa mkuu wa wilaya siyo kosa.

“Kisheria iko ivi, kama Makonda alifikishwa mahakamani akatuhumiwa kumfanyia fujo Jaji Warioba, basi ni makosa kuwa mkuu wa wilaya, lakini kama hakushitakiwa popote haina shida,” alisema Rwechengura

MNYIKA
Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Tanzania Bara, John Mnyika, amesema mabadiliko ya wakuu wa wilaya ni mkakati wa CCM kupitisha katiba inayopendekezwa kinyemela.

Mnyika, ambaye pia ni Mbunge wa Ubungo, alisema uamuzi wa Rais Kikwete kupangua safu hiyo una lengo la kuhujumu upinzani kuelekea uchaguzi mkuu zaidi kuliko ufanisi wa utendaji wa serikali.

Katika taatifa yake kwa vyombo vya habari jana, Mnyika alisema kuhamishwa vituo kwa wakuu wengi wa wilaya miezi michache kabla ya kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa na uchaguzi mkuu, ni mkakati wa wakuu hao ambao ni makada wa CCM kushinikiza Watanzania kupigia kura ya ndiyo katiba hiyo.

Alisema uteuzi huo unapaswa kuibua mjadala wa haja ya kufuta vyeo vya wakuu wa wilaya kwa Watanzania.

Alisema Watanzania wanatakiwa kutoshiriki kupiga kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa kwa sababu imeendeleza mianya ya nafasi hizo kutumika kwa siasa chafu za hujuma za CCM.

“Badala yake wananchi wajiandikishe kwa wingi kwa ajili ya uchaguzi mkuu kupiga kura kuiondoa CCM madarakani ili katiba mpya ikamilishwe na Rais mpya, serikali mpya, Bunge jipya na Bunge Maalumu jipya kwa kuzingatia maoni ya wananchi,” alisema Mnyika.

Alisema mpango huo ni wa kuendeleza mianya ya nafasi hizo kutumika kwa siasa chafu nchini.
CHANZO: NIPASHE

No comments: