Advertisements

Monday, March 2, 2015

KONYAGI NI NENO LA KIHAYA JITIRIRISHE NA HII KUPATA UKWELI

David Mgwassa: 
Konyagi ni neno la Kihaya
Konyagi bila kula vizuri hili hapa ndiyo jibu.
JINA la kinywaji cha Konyagi ni maarufu kuliko jina la kampuni inayotengeneza kinywaji hicho,  Tanzania Distilleries (DTL). Baada ya umaarufu ambao kinywaji hicho kimejipatia hapa nchini, sasa kimejiingiza katika utengenezaji wa vinywaji vya aina nyingine kama vile mvinyo kwa ajili ya kukidhi soko la ndani na lile la kimataifa.
Mkurugenzi Mtendaji wa DTL, David Mgassa (DM), amezungumza na jarida la The Guardian (TG) la Uingereza hivi karibuni kuhusu mabadiliko yanayoendelea ndani ya kampuni hiyo ambayo ni mtoto wa Uhuru wa Tanganyika. Tafsiri ya Kiswahili ni ya gazeti hili. Endelea

TG: Ni nini siri ya mafanikio ya kinywaji cha Konyagi?

DM: Wakati anapozungumzia vinywaji vikali, mtu anaweza kuzungumzia vile vya aina ya whisky au brandy. Huwezi kuiweka Konyagi katika kundi hilo. Konyagi haina ukali wa vinywaji kama hivyo. Iko kipekee sana. Kwa kawaida, vinywaji vikali vina kilevi cha asilimia 40 lakini Konyagi kilevi chake ni asilimia 35 tu.

Ndiyo maana wanaokunywa Konyagi wanapata ladha ya kipeekee sana. Ukitaka kufaidi kinywaji hiki unatakiwa kuchanganya na vinywaji vyenye ladha ya ndimu au limao.

TG: Neno Konyagi lina maana gani?

DM: Konyagi ni neno lenye asili ya kabila la Wahaya na lina maana ya “ Njooni tupate kinywaji). Wahaya ni mojawapo ya makabila ya asili ya Tanzania linapokana katika eneo la Ukanda wa Ziwa Victoria.

TG: Kama alama maarufu ya biashara, tueleze Konyagi inafanya vizuri katika soko la Tanzania?

DM: Konyagi ina umri wa zaidi ya miaka 42. Huu ni muda mrefu kwa bidhaa kuwa sokoni na kitu kizuri ni kwamba hii ni bidhaa ambayo imetokana na Watanzania wenyewe. Ni bidhaa ya nyumbani.

Katika kipindi hicho, Konyagi imekuwa ikikua kila kukicha. Ukuaji huo umeongezeka kasi katika kipindi cha miaka minne hadi mitano iliyopita. Kama ukiangalia kiwango cha uzalishaji leo, ni mara kumi ya kiwango kilichokuwa kikizalishwa miaka mitano iliyopita.

Tulichokifanya ni kutengeneza kinywaji cha kipekee sokoni. Tumetengeza kinywaji ambacho kiko katikati ya vinywaji vikali kabisa kama Johnny Walker na pombe kali za kienyeji kama vile gongo. Konyagi si kama gongo na wala si kama Walker. Iko katikati ya vinywaji hivyo viwili.

TG: Zaidi ya Konyagi, kuna vinywaji vingine ambavyo vinazalishwa na TDL, je mauzo ya Konyagi ni sawa na asilimia ngapi ya mauzo ya vinywaji vyote mnavyotengeneza?

DM: Konyagi inachangia asilimia 65 ya mauzo yetu kwa sasa ingawa tuna bidhaa nyingine sokoni ambazo sasa ukuaji wake ni mzuri zaidi ya ule wa Konyagi. Sasa tumeanza kuuza mvinyo. Katika siku za nyuma, mvinyo uliokuwa ukiuzwa ni ule wa bei ya juu, hakukuwa na mvinyo ambao watu wengi wangeweza kumudu bei yake. Tumeingia pia kwenye soko la vinywaji jamii ya maziwa. Maarufu zaidi kwa sasa ni kile kinachojulikana kwa jina la Zanzi.

Huwezi kuifananisha na kinywaji kama Amarula au Baileys ambavyo vinajulikana zaidi lakini hiki ni kinywaji ambacho kinagusa soko la walio wengi. Hii ni kwa sababu bei zake zinaendana na hali halisi ya kipato cha walio wengi. Ndiyo maana utakuta mauzo yake yamekuwa yakipanda sana.

Mojawapo ya mafanikio haya ya kutazama nini soko linahitaji na kuzalisha ni kwamba sasa tunafanya vizuri hata katika mauzo ya nje ya nchi. Mwaka jana pekee, tuliuza zaidi ya lita 850,000 za vinywaji vyetu nje ya nchi na nadhani ilitufanya tuwe wauzaji nje wa bidhaa namba sita au saba kwa mwaka uliopita.

TG: Ni nchi zipi ambako mnauza zaidi bidhaa zenu zaidi ya Tanzania?

DM: Kenya, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Sudan Kusini, Rwanda, Zambia na Msumbiji. Mkakati wetu ni kuhakikisha kwamba soko la walio wengi linakidhiwa mahitaji yake. Kwa sasa tunaona ongezeko la asilimia 10 la ukuaji wa biashara zetu katika masoko yetu ya nje.

TG: Je, mna mpango wowote wa kuona Konyagi inauzwa duniani kote na si Afrika pekee?

DM: Kabla ya kufika huko, tunahitaji kwanza kufanya mabadiliko ya mambo ambayo ingawa soko letu la sasa halijali sana, kwenye masoko ya kimataifa linaangaliwa sana. Masuala kama ya usindikaji (packaging) na chapa (branding).

Miongoni mwa mambo ambayo tunayaona kama tunaweza kuyafanya katika siku za mbele ni kutoa leseni kwa makampuni yaliyo nje ya Tanzania kuweza kutengeneza Konyagi hukohuko waliko.

Kwa mfano, kama tukiona kuwa Konyagi ina wateja wengi Uingereza au Australia, tunaweza kuipa leseni mojawapo ya kampuni ya huko ili izalishe na kuuza Konyagi huko ilipo. Unajua kwa wenzetu wanaweza wakaacha tu kununua bidhaa yako kwa sababu inatoka Afrika au Tanzania. Ikitengenezwa kwao wanakuwa na imani nayo zaidi. Hii ni kwa sababu ya unyanyapaa tu wa bidhaa kutoka katika nchi zinazoendelea.

TG: Mauzo ya bidhaa zenu nje ya nchi ni kiasi gani cha mauzo yenu yote?

DM: Asilimia nane. Kwangu, hiki ni kiwango kizuri kizuri kwa kampuni ambayo inataka kufanya biashara zake vizuri. Si vizuri kwa kampuni kutegemea zaidi soko la nje kuliko la ndani kwa sababu huko nje kunaweza kutokea mtikisiko wa aina yoyote na ukapata matatizo. Kwa aina ya biashara zetu ni vizuri kuwa na soko la uhakika zaidi ndani kuliko nje.

Huwezi kutegemea sana soko la nje lakini pia si vema kuwa na fursa nzuri nje ya nchi ambayo umeshindwa kuitumia.

TG: Mmejiandaa kuongeza uzalishaji wenu ili kukidhi mahitaji ya soko yanayoonekana kuwa yataongezeka katika siku zijazo?

DM: Ndiyo. Tayari tumeongeza eneo letu mara mbili zaidi hapa. Pia tumefungua kiwanda kingine mkoani Mwanza ambao pia ni mji mwingine unaokua vizuri. Kwa sasa, mkakati ni kujenga kiwanda kingine Kusini mwa Tanzania.

TG: Mnafikiri kuanzisha bidhaa nyingine yoyote mpya katika siku za karibuni?

DM: Katika siku za karibuni, tumeanza kuona vijana wakipenda sana vinywaji vikali vyenye mchanganyiko wa divai (kokteli). Tumeanza kujaribu kutengeneza kinywaji cha Konyagi chenye mchanganyiko huo. Inaweza kuitwa Konyagi Mix

TG: Mnashirikiana vipi na makampuni ya kigeni kuhakikisha kwamba wanaleta vinywaji vya viwango vya juu nchini Tanzania?

DM: OMojawapo ya wabia wetu muhimu ni makampuni ya Distell Group, kutoka nchini Afrika Kusini ambayo ni mojawapo ya makampuni makubwa ya kutengeneza vinywaji vikali na mvinyo barani Afrika. Ingawa tunazalisha vinywaji vyetu, lakini pia huwa tunatengeneza vinywaji vyao kwa ajili ya kuviuza kwenye eneo letu hili la Afrika Mashariki.

Miongoni mwa vinywaji hivyo ni mvinyo wa Overmeer ambao tunatengeneza kwa kutumia zabibu ya Tanzania na pia bidhaa nyingine kutoka Afrika Kusini. Zaidi ya hapo, pia sisi huagiza vinywaji vingine kutoka nje kama vile Amarula.

TG: Unauonaje mustakabali wa soko la sekta ya mvinyo nchini kwako?

DM: Kuna kipindi soko la mvinyo hapa Tanzania lilikufa kabisa. Kimsingi, ni sisi ndiyo ambao tulilifufua miaka saba iliyopita. Nchini kwetu zabibu hailimwi kama inavyolimwa kwingineko kama Ufaransa ambapo wakulima ni wale wenye mashamba makubwa.

Hapa kwetu wakulima ni wale watu wenye mashamba yenye ukubwa wa ekari mbili hadi tatu. Hiki ni kilimo cha kujitosheleza tu na huwezi kusema kwamba ni cha kibiashara kabisakabisa. Kwa hiyo hata mvinyo unaozalishwa ni ule kidogo tu wa kujitosheleza. Hiki si kitu kibaya sana kwa vile kinatupa sisi fursa ya kutumia zao hili na wakulima hawa kama njia mojawapo ya kusaidiana na serikali katika kupambana na umasikini.

Kama wakulima hawa watahakikishiwa soko la kudumu la bidhaa zao watalima zaidi, wengi zaidi na matokeo yake watajikwamua kutoka katika umasikini walionao sasa.

Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, viwanda viwili vya kuzalisha mvinyo vimeanzishwa mkoani Dodoma na sisi tuko mbioni kuanzisha cha kwetu katika siku za usoni. Kuna changamoto nyingi kwenye hili lakini hilo ni jambo la kawaida kokote.

TG: Mnauza mvinyo nje ya nchi?

DM: Ndiyo. Tunauza katika nchi za Rwanda na Kenya.

TG: Mnakumbana na changamoto katika ufanyaji wa shughuli zenu nchini Tanzania?

DM: Tanzania, kama zilivyo nchi nyingi zinazoendelea, ina changamoto nyingi kibiashara. Kama utachunguza kwa makini, utabaini kwamba sekta isiyo rasmi ni kubwa kuliko ile isiyo rasmi.

Mojawapo ya changamoto kubwa, kwa upande wa serikali, zinahusu namna bora ya kuongeza wigo wa ukusanyaji kodi kutoka katika mazingira ya namna hiyo. Hili ni mojawapo ya matatizo ambayo yanaikumba Tanzania na serikali inashindwa kutanua wigo huo.

Hii maana yake ni kwamba yale makampuni machache yaliyo katika sekta rasmi yanalazimika kubeba mzigo mkubwa wa kulipa kodi kwa sababu serikali haina mahali kwingine kwa kwenda.

Tunapambana sana kuishawishi serikali kuhusu hili hasa kwenye maeneo ya ulipaji wa kodi za kawaida, Kodi ya Ongezeko la Thamani na Ushuru.

TG: Kama kampuni, unadhani TDL ina maono gani ya kukua katika siku zijazo?

DM: Maono yetu ni kuwa kiwanda bora cha utoneshaji (distillery) katika eneo letu la Afrika. Tunataka uwepo wetu uonekane kuanzia Tanzania hadi Angola. Hii maana yake ni kwamba Zambia, Zimbabwe, Msumbiji, DRC, Congo-Brazzaville, Sudan, Sudan Kusini, Kenya na Uganda ndiyo yanatakiwa kuwa masoko yetu ya msingi.

Tukikamilisha hilo, tutaanza sasa kufikiria namna ya kulishika soko la kimataifa. Wenzetu wanaofanya biashara kama yetu wameanza zamani. Kama ukiangalia vinywaji kutoka Scotland, vingine vina umri wa zaidi ya miaka 200.

Kama ukilinganisha na wenzetu kama hao, utaona kwamba sisi bado ni wachanga sana katika uzalishaji wa vinywaji vikali na mvinyo. Hata hivyo, tutakua taratibu na mwisho tutakuwa wakubwa pia.

TG: Katika kipindi cha miaka kumi ijayo, unaonaje mustakabali wa Konyagi na TDL?

DM: Nitafurahi sana kuona Konyagi ikizalishwa katika walau nchi nne duniani na hivyo kujihalalisha kama kinywaji cha walio wengi barani Afrika. Kama utaangalia takwimu za ukuaji wa uchumi katika nchi nyingi za Afrika, utaona kwamba nyingi zinakua kwa kiwango cha kuanzia asilimia tano na zaidi.

Hii ni ishara kwamba kada ya watu wenye kipato cha kati itazidi kukua katika miaka inayokuja. Hawa ndiyo watakuwa wateja wakuu wa bidhaa zetu na ni muhimu kwetu kuhakikisha kundi hili kubwa linapata linachohitaji. Nafikiri kwamba huko tuendako biashara itakuwa nzuri kuliko ilivyo sasa

1 comment:

Anonymous said...

misifa ya kihaya imeshaanza kabila hili kwa kupenda misifa wee na kujiona na wenye dharau ya hali ya juu na kujifanya wanajua kila kitu wao na wana roho mbaya sana hawa.mwaaafyuu eti konyangi ni jina la kihaya mwaaafyuuuuuuuuuuuuuuuuu.

pelekeni misifa yenu kwingineko.