Advertisements

Saturday, May 30, 2015

UMOJA WA MATAIFA WA WAENZI WALINDA WA AMANI WALIOPOTEZA MAISHA 2014

 
Maura Mwingira, Charge d' affaires a.i wa Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, akipokea kutoka kwa Mkuu wa Idara ya Operesheni za Ulinzi wa Amani za Umoja wa Mataifa ( DPKO ) Bw. Harves Ladsous, Medali Maalum ya Dag Hammarskjold ambazo wametunukiwa Mashujaa wanne walinda Amani kutoka JWTZ ambao walipoteza maisha mwaka 2014 wakati wakitekeleza majukumu yao. Umoja wa Mataifa umeitenga Mei 29 kama siku ya Kimataifa ya kuwakumbuka na kuwaenzi walinda amani ambao walipoteza maisha katika misheni mbalimbali za Umoja wa Mataifa. Jumla ya walinda amani 126 walipoteza maisha mwaka jana . Medali hizo zitawasilishwa kwa Familia za Mashujaa hao.
Maura Mwingira wa Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, akiandika katika kitabu maalum, baada ya kupokea kwa niaba ya familia za mashujaa wanne wa JWTZ waliopoteza maisha wakati wakihudumu katika misheni za kulinda amani mwaka jana. Medali hiyo maalum ya Dag Hammarskjold ilitokwa siku ya ijumaa kama ishara ya kuwaenzi, kutambua na kuthamini mchango mkubwa wa mashujaa hao.

Katibu Mkuu Ban Ki Moon, akiwa na Naibu Katibu Mkuu, Jan Eliasson, na Viongozi wakuu wa Idara ya Operesheni za Ulinzi wa Amani ( DPKO) muda mfupi kabla ya utoaji wa medali maalum kwa mashujaa 126 walinda amani ambao walipoteza maisha mwaka jana. katika salamu zake Katibu Mkuu alieleza kwamba katika maadhimisho yote yanayofanyika katika Umoja wa Mataifa, adhimisho la kuwakumbuka na kuwaenzi walinda amani ni adhimisho lenye kutia simanzi na gumu.

Mpiga Buluji akiimba wimbo maalum wa maombolezo kama ishara ya kuwakumbuka mashujaa 126 walinda amani waliopoteza maisha mwaka jana. shughuli za utoaji wa medali maalum zilitanguliwa na uwekaji wa shada maalum la maua katika eneo ambalo limetengwa katika viunga vya Umoja wa Mataifa .Pichani anaonekana Katibu Mkuu Ban Ki Moon akitoa salamu za heshima kwa wahanga hao anaonekana pia Naibu Katibu Mkuu Jan Eliasson

Na MwandishiMaalum, New York
Mashujaa Private Ally Salum Jumanne, Private Mohamed John Mbizi, Private Vasco Adrian Msigala na Sajent Hamis Juma Nyange kutoka Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) ni miongoni mwa mashujaa 126 ambao siku ya Ijumaa, Umoja wa Mataifa uliwatunuku medali ya Dag Hammarskjold
Ijumaa ya Mei 29 ya kila mwaka Umoja wa Mataifa umeitenga kama siku
maalum ya kutambua na kuenzi mchango wa walinda Amani ambao wamepoteza maisha wakati wa kitekeleza majukumu ya ulinzi wa Amani kupitia operesheni za Umoja wa Mataifa.


Katika adhimisho
hilo na ambalo lilihudhuriwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa mataifa, Ban ki moon, Naibu wake Jan Eliasson, na Wakuu wa Idara za Ulinzi za Umoja wa Mataifa, jumla ya mashujaa 126 kutoka nchi 38 waliopoteza maisha mwaka jana (2014) walienziwa kwa kutunukiwa medali maalum ya Dag Hammarskjold.

Adhimisho hilo lilitanguliwa na uwekaji wa shada la maua kwa heshima ya mashujaa hao, shada liliwekwa na Katibu Mkuu Ban Ki Moon katika sehemu maalum ambayo imeandaliwa kwa ajili ya kumbukumbu hiyo.
Akizungumza kwa masikitiko makubwa wakati wa hafla hiyo, Katibu Mkuu, Ban Ki Moon, amesema, katika maadhimisho yote yanayofanyika katika Umoja wa Mataifa, hakuna adhimisho lenye kutiasimanzi na ngumu kama hili la kuwakumbuka na kuwaenzi walinda amani ambao wamepoteza maisha yao wakati wa kitoa ulinzi kwa watu wengine.

“ Ninasikitika kusema kwamba, hii ni mara ya saba mfululizo ambapo zaidi ya walinda amani 100 wamepoteza maisha katika kipindi cha mwaka mmoja.
Hatari wanayokumbana nayo walinda amani wetu inazidi kuongezeka kwa kasi kubwa, kutokana kushambuliwa na makundi ya wahafidhina na makundi ya wanamgambo wenye silaha mpaka hatari ya magonjwa ambukizi kama vile Ebola” amesema KatibuMkuu.

Mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa akaendelea kusema.
“ Tumekusanyika hapa kuwaenzi mashujaa wetu waume kwa wake ambao wamepoteza maisha yao wakati wakiwalinda wananchi katika maeneo hatari duniani. Kujitoa kwao muhanga na namna walivyo ishi maisha yao, wanatufanya sisi tujisikie fahari na kututia shime ya kufanyakazi kwa bidii zaidi ili kudhihirisha kwamba maisha yao hayakupote abure.
Ban Ki Moon, awaeleza wawakilishi kutoka nchi ambazo zimepoteza mashuja wake kwamba, operesheni za ulinzi wa amani chini ya Umoja wa Mataifa zitaendelea kuwa zenye changamoto na hatari kubwa, na cha kusikitisha ni kwamba adhimisho lililofanyika ijumaa la kuwaenzi mashujaa hao halitakuwa la mwisho
“Walinda amani wetu wanabeba jukumu zito kwa ajili yetu sote.
Natoa heshima zangu kwa mashujaa na salamu zangu za pole kwa familia za mashujaa hawa” akasisitiza Katibu Mkuu.

Walinda amani hao 126 naraia 19 wamepoteza maisha wakati
wakihudumia katika misheni zilizopo, Afghanistan, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Ivory Coast, Cyprus, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Haiti, Mali, Mashariki ya Kati, Liberia, Sudan na Sudan ya Kusini
Pamoja na Tanzania nchi nyingine ambazo zimepoteza mashujaa wake katika misheni mbalimbali za kulinda Amani katika mwaka uliopita ni Senegal, Afrika ya Kusini, Uhispania, Togo, Rwanda, Benin, Burkina Faso, Bangladesh,na Burundi.

Nyingine ni Cambodia, Chad, El Salvador, Ethiopia, Fiji, France, Ghana, India, Indonesia, kenya , Malawi, Niger, Pakistan, Philippines, Tunisia na Zimbabwe.

Pamoja na mashujaa hao ambao ni wanajeshi, wapo pia raia 19 wakiwamo pia polisi, Madaktari, watumishi na watoa misaada ya kibinadamu ambao wamepoteza maisha wakati wa kitoa misaada kwa binadamu wenzao.

Wakati Umoja wa Mataifa ukiwaenzi mashujaa hao waliopoteza maisha mwaka jana. Tayari mwaka huu wa 2015 mashujaa wapatao 49 wamekwisha poteza maisha wakitekeleza majukumu yao ya kuleta Amani ,utulivu na ulinzi wa raia wasiona hatia katika nchi zenye migogoro. Kati ya mashujaa 49 hao wapo watanzania wawili.

Jumla ya walinzi wa Amani 3,300 wamekwisha kupoteza maisha tangu kuanzishwa kwa Operesheni za Ulinzi wa Amani chini ya Umoja wa Mataifa mwaka 1948

No comments: