Advertisements

Monday, August 3, 2015

CHAMA CHA MADEREVA KIMETANGAZA MGOMO WA MADEREVA NCHI NZIMA KUANZIA AGOSTI TISA MWAKA HUU.

Chama cha wafanyakazi madereva Tanzania-TADWU- kimetangaza mgomo wa madereva nchi nzima kuanzia Agosti tisa mwaka huu baada ya wamiliki wa mabasi, wakala wa usafiri wa nchi kavu na majini pamoja na wizara ya kazi kushindwa kutekeleza makubaliano yalifikiwa na tume iliyoundwa na waziri mkuu kutatua mgogoro wa madereva nchni.
Kauli hiyo imetolewa na naibu katibu mkuu wa TADWU, Bwana Rashidi Salehe wakati akizungumza na ITV ambapo amesema mgomo huo unarejea tena baada ya wamiliki wa mabasi kwa kushirikiana na wizara kazi pamoja na Sumatra kuendelea kutumia mikataba ya zamani katika kutoa leseni wakati makubaliano ya tume iliyoundwa na waziri mkuu yalitaka mikataba mipya ianze kutumika kuanzia julai mosi mwaka huu.


Wakizungumza na ITV baadhi ya madereva wamelalamikia wizara ya kazi na sumatra kwa kukaidi agizo la waziri mkuu na kuendelea kupokea mikataba ya zamani toka kwa wamiliki wa mabasi na kutoa leseni wakati makubaliano yalishafanyika na kusisitiza katika makubaliano hayo mishahara ya madereva wa malori yanayotoka nje ya nchi walikuwa wanatakiwa kulipwa mishahara ya shilingi milioni moja, huku madereva wa daladala shilingi laki tano pamoja na posho nyingine.

Akizungumza kwa simu na mmoja wa viongozi wa chama cha wamiliki wa mabasi nchni kwa masharti ya kutotajwa jina amewalalamikia madereva hao kwa kupanga mgomo badala ya kupeleka madai yao kwa tume ya kudumu iliyoundwa na waziri mkuu ili kupata ufumbuzi ambapo amesema kuna baadhi ya madereva wanatengeneza migomo ili kuleta usumbufu kwa wananchi na serikali kwa ujumla.

No comments: