Advertisements

Monday, August 24, 2015

CHUO KIKUU DODOMA KUMUENZI JK

Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Profesa Idris Kikula akimkabidhi Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Tuvako Manongi nakala ya kitambu kinachoelezea kwa kina historia ya Chuo Kikuu cha Dodoma. Katika Maelezo yake, Prof. Kikula amesema UDOM imeamua kuweka katika maandishi historia nzima ya Chuo hili ili kuepusha upotoshaji na upindishaji wa ukweli na kwamba UDOM inapanga kumuenzi Mhe. Rais Jakaya Kikwete ikiwa ni kutambua mchango wake katika kuanzishwa na hatimaye ujenzi wa UDOM. wengine katika picha kutoka kushoto ni Naibu Mkuu wa Chuo Prof. Shaaban Mlacha anayesimamia masuala ya mipango, fedha na utawala, Naibu Mwakilishi wa Kudumu Balozi Ramadhan Mwinyi na Bi. Christina Silvester, Katibu wa Baraza.
Makamu Mkuu wa UDOM Prof. Kikula akimkabidhi nakala ya kitambu cha historia ya UDOM, Prof. Estomih Mtui, M.D anayefanya kazi Weill Cornel Medical Collage, Prof. Mtui ni moja kati ya wana-Diaspora ambaye amekuwa kiungo kikubwa katika utafutaji na upatikanaji wa vifaa tiba ,vitabu na wataalam wa fani mbalimbali kwaajili ya kusaidia nchini Tanzania. baadhi ya vifaa na vitabu ambavyo Ujumbe wa Makamu Mkuu wa UDOM wamevikagua vimepatikana kwa juhudi za Prof. Mtui

Na Mwandishi Maalum, New York
Chuo Kikuu cha Dodoma ( UDOM), kinatarajia kufanya hafla ya  aina yake ya kumuenzi Rais  wa Jamhuri ya  Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete kama sehemu ya kutambua mchango wake wa hali na mali uliopelekea kuanzishwa kwa Chuo   Kikuu hicho cha aina yake Tanzania na nje ya Tanzania.
Taarifa ya kusudio la  Chuo hicho kumuenzi Mh. Rais Kikwete imetolewa mwishoni mwa wiki na Makamu Mkuu wa  UDOM, Prof. Idris Kikula wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na   Mabalozi na Maafisa wa Uwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa.
Profesa Kikula   na ujumbe wake   yuko  katika ziara ya kikazi nchini Marekani,  ziara iliyomfikisha  Jijini New York, ambapo   ujumbe ulipata fursa ya kukagua vifaa tiba na vitabu  vya kiada na ziada ambavyo vimetolewa na  wadau mbalimbali wenye mapenzi mema na Tanzania.
 Baada ya  kukagua vifaa na vitabu hivyo na kijiridhisha,  Makamu Mkuu wa UDOM ameushukuru Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania kwa kuwapatia fursa hiyo ya kujionea  wenyewe aina ya vifaa tiba na vitabu ambayo amesema  vitakuwa msaada mkubwa kwa  Kitivo cha Sayansi ya Afya cha  Chuo hicho.

“Waheshimiwa Mabalozi, mimi na ujumbe wangu napenda kwa moyo wa dhati kabisa kutoa shukrani zetu  kwa kutuonyesha vifaa na vitabu ambavyo kupitia kwenu wafadhili wamevitoa kuwasaidia watanzania nanyi  mkaona bora kutushirikisha na kuona namba gani  Chuo chetu kinaweza kunufaika na misaada ya aina hii” akasema Pofesa Kikula
Na kuongeza kwamba Kitivo cha Sayansi ya Afya na ambacho pia kina Zahanati kinahitaji sana misaada ya  kila aina ili kiweze kutimiza lengo lake kuu la kuwaandaa  madaktari na wataalam mbalimbali lakini pia kutoa huduma  uchunguzi na  matibabu siyo tu kwa wanafunzi na wafanyakazi wa UDOM bali pia kwa watanzania wote.
“ Uongozi wangu unapenda kutambua   juhudi zenu hizi za kushirikiana na wadau mbalimbali  kusaidia  siyo tu vyuo vikuu vyetu lakini na watanzania.Mmedhihirisha kwa  kwa vitendo na si maneno na  hii imetupa faraja sana na kudhihirisha namna gani tunaweza kushirikiana kwa karibu Zaidi.
Akasema  kuanzishwa  kwa   Chuo Kikuu cha Dodoma ni ndoto na hatimaye mbegu iliyopandwa na Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete ,  ndoto uliyoanzia kwenye kampeni yake ya  urais mwaka 2005.
“ilianza kama ahadi ya kampeni, ahadi ambayo haikuishia katika maneno matupu ya ahadi bali aliitekeleza ahadi ile na leo hii tunaiona mbegu aliyoipanda ikichanua na mavuno yanaonekana”. Akasema Prof.Kikula kwa  msisitizo wa aina yake.
Anasema  haikuwa rahisi kuifanikisiha ndoto ile ya Rais kutokana na pingamizi  mbalimbali  kutoka nje na ndani ya serikali.
Anaongeza kuwa shauku ya ujenzi na hatimaye uwepo wa UDOM haukuishia kwa watanzania tu  bali hata baadhi ya  Mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao  nchini Tanzania ambazo walikuwa wakimfuata na  kutaka kujua  tajiri ngani aliyekuwa anafadhiri mradi huu mkubwa.
Profesa anasema mara zote alikuwa akiwajibu Mabalozi hao kuwa mradi ule ulikuwa ukijengwa na kufadhiliwa na watanzania wenyewe na serikali yao.
“Nisema kwamba haikuwa kazi rahisi, tulipata  wakati mgumu  na pingamizi  hata kutoka  ndani ya serikali.  Wapo  baadhi ya viongozi ambao hawakutaka   Chuo Kikuu hiki kijengwe  Dodoma. Mimi binafsi   nilimuuliza Mhe. Rais kwa nini alikuwa anataka  Chuo Kijengwe Dodoma.
Mhe. Rais alinijibu. “Ninataka  kijengwe  Dodoma na si kwingine, kwa sababu kwanza, ya umaskini wa  Mkoa wa Dodoma na pili Dodoma ni Makao Makuu ya Nchi”.
Profesa Kikula  anaeleza kuwa  Mhe.  Kikwete aliamini kwamba kwa kujenga chuo Kikuu chenye  ukubwa na uwezo wa kudahili wanafunzi wengi Zaidi,   pamoja na kuongeza udahili wa wanafunzi wengi na kuwapa fursa  vijana wengi wa kitanzania kupata elimu ya juu, lakini pia kungefungua milango ya  kiuchumi na maendeleo ya kijamii,  na hivyo kuwapunguzia  umaskini wananchi wa Mkoa wa Dodoma.
Kwa mijibu wa Makamu Mkuu wa UDOM anasema, maono hayo ya Rais ya kuongeza udahili wa wanafunzi na kufungua  milango ya uchumi na kupunguza umaskini   kwa wakazi wa mkoa wa  Dodoma yamefanikiwa kwa kiasi kikubwa.
Ni kwa sababu hiyo, Profesa Kikula anasema,  watanzania   hawanabudi kujivunia  mafanikio yanayotokana na  utekelezaji wa  ahadi na vipambaumbele vinavyowekwa na serikali yao.
“watanzania ni vema tukajijengea utamaduni wa kujivunia mafanikio yetu, penye ukweli lazima tusema,  sisi wa Chuo Kikuu  cha Dodoma tuna kila sababu ya kujivunia mafanikio  ya Chuo  hiki, na  ndio maana  tumeandika kijitabu kinachoelezea  historia ya  UDOM na mchango mkubwa wa Mhe. Rais.  tumeweka kwa maandishi ili kuepusha upindishwaji ukweli  na upotoshaji wa historia ya UDOM”.
Akasema kuwa tayari kijitabu hicho amekabidhiwa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma  Rais Mstaafu wa awamu ya Tatu Mhe. Benjamin William Mkapa kwaajili ya hatua za kuangalia   taratibu za kumuenzi Mhe. Rais Jakaya Mrisho Kikwete.
Kwa upande wake, Balozi Tuvako Manongi,  Mwakilishi wakudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa,  ameushuku uongoziwa  UDOM kwa kuitikia  wito wa   Uwakilishi wa  kutumia ziara yao ya kikazi,  kujionea kukagua vifaa na vitabu ambavyo  vimepatika kwa ushirikiano wa  Uwakilishi  na wadau  mbalimbali.
Akasema kuwa Uwakilishi utaendelea na  juhudi za kutafuta wadau  wanaoweza kusaidia katika maeneo  mbalimbali, kutokana kwamba wapo watu wanaopenda sana kuisaidia Tanzania, akasisitiza haja na umuhimu waufuatiliaji na wepesi wa kujibu barua au mapendekezo  Uwakilishi unapeleka kwa Taasisi  mbalimbali zikiwa  Vyuo vya elimu ya Juu.



No comments: