ANGALIA LIVE NEWS

Tuesday, August 4, 2015

Panga la urais CCM kuhamia kwa wabunge



Nape Nnauye, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM
By Exuper Kachenje na Suzan Mwillo, Mwananchi
Dar es Salaam. Chama cha Mapinduzi (CCM), kimesema kitatumia ‘panga’ lilelile lililotumika kumpata mgombea wake wa urais katika kuchuja wagombea ubunge na udiwani kupitia vikao vyake halali ili kupata wagombea safi.

Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnaye alisema hayo jana Dar es Salaam katika mkutano na waandishi wa habari, kuzungumzia mchakato wa vikao vya kamati za chama hicho ili kupata wagombea wa ubunge, uwakilishi na udiwani baada ya mchakato wa kura za maoni kukamilika.

Alisema mchakato huo utaanza kwa kikao cha Kamati Maalumu ya CCM Agosti 6 na 7 kuchuja na kupitisha wagombea ubunge na uwakilishi. Agosti 8 na 9, Sekretarieti itakutana ikifuatiwa na Kamati Kuu pia kwa siku mbili kabla ya Halmashauri Kuu kukutana Agosti 12 na 13 kuteua wagombea ubunge na uwakilishi.

“Kura za maoni siyo mwisho wa safari, ni hatua ya kwanza ya kuona ni nani anayekubalika… siyo kibali cha kupeperusha bendera ya CCM, kama kuna upungufu vikao vitachukua hatua. Kura ya maoni si kigezo… kama wamecheza rafu au kutumia rushwa, hata kama wameshinda kwa kura nyingi, ikithibitika wanaweza kuondolewa,” alisema Nape na kuongeza:

“Tutafanya kama ilivyokuwa kwa wagombea urais, kama maadili hayakufuatwa wanaweza kuondolewa siyo tu wa kwanza, hata wanne, hata kufuta matokeo. Tutachukua hatua kwenye ubunge, tutachukua hatua kwenye udiwani kwa wale watakaojihusisha na rushwa. Hawatapata nafasi ya uteuzi kwenye chama chetu. Hatuna muda wa kuanza kuosha watu na madodoki.”

Alikumbusha jinsi chama hicho kilivyomteua Dk Khamis Kigwangallah kuwania ubunge wa Nzega alikoteuliwa licha ya kushika nafasi ya tatu katika kura ya maoni.

Changamoto kura za maoni

Kuhusu changamoto kwenye upigaji kura za maoni ikiwamo vitendo vya rushwa, Nape alisema kwa takwimu walizonazo, changamoto zilizojitokeza ni kidogo ikilinganishwa na miaka ya nyuma... “Hii ni kwa sababu tumeboresha utaratibu tofauti na huko nyuma. Maeneo mengi yamemaliza na hata yale ambayo yamekuwa na kasoro za hapa na pale tumezitatua.

“…Kura za maoni katika chama chetu zimetoa demokrasia na bila shaka tumefundisha vyama vingine. Vyama vingi vinatoa wagombea mfukoni, lakini sisi tunawapeleka kwa wanachama wanapigiwa kura,” alisema Nape.

Vigogo kuanguka

Alisema kuwa kutokana na kukua kwa demokrasia katika chama hicho na kujenga mfumo mzuri zaidi wa upigaji kura za maoni, hata vigogo wasiofanya vizuri wameanguka katika kura za maoni.

Kauli hiyo ya Nape imekuja huku kukiwa na ripoti ya baadhi ya mawaziri na wabunge wanaomaliza muda wao kuanguka katika kura za maoni.

Vigogo kuhama CCM

Alipoulizwa kuhusu kuhama chama hicho kwa waziri mkuu wa zamani, Edward Lowassa na Mbunge wa Segerea, Dk Makongoro Mahanga na wanaCCM wengine, Nape alisema siyo jambo la ajabu na kwamba si wa kwanza na wala hawatakuwa wa mwisho. “Wapo wanaotoka CCM kwenda vyama vingine na wapo wanaotoka vyama vingine na kuja CCM. Lakini niseme tu kwamba wapo ambao wanataka uongozi na wapo ambao wanataka kwenda kuongoza watu:

“Anayetaka kuongoza watu ni mvumilivu, mtulivu na hufuata taratibu. Lakini wapo ambao lengo siyo kwenda kuongoza watu, lengo ni masilahi binafsi. Wakikosa uongozi huonyesha tabia zao waziwazi.”

3 comments:

Anonymous said...

WEWE MWENYEWE ULIKAMATWA KWA RUSHWA, NATEGEMEA UTAKATWA PIA. KUHUSU WAGOMBEA WA MIFUKONI MBONA NINYI CCM MLIKUWA NAO.....HAYO MAJINA MATANO MBONA YALITOKA MIFUKONI.....HIYO NDIYO DEMOKRASIA? AU MNATUFANYA WATANZANIA KUWA WEPESI WA KUSAHAU???

Anonymous said...

Mwaka huu lazima mshindwe uchaguzi, hakuna yeyote wa CCM aliyegombea bila rushwa ukiwemo wewe Nape. Ni wakati wa mabadiliko sasa.. Imetosha!

Anonymous said...

Kwa nini hilo panga Hali kukutafuta wewe, Nape? Kwanza CCM ina ukimwi sasa hivi, inauma rushea, mmeinunua CCM. Hata kama ni kweli wewe sio mla rushwa, Iweje wewe mfanyakazi wa chama uweze kupata milioni tatu ya kulipa wakala?