Advertisements

Monday, October 5, 2015

BALOZI SEIF AWANADI WAGOMBEA UBUNGE NA UWAKILISHI JIMBO LA KIEMBE SAMAKI

Baadhi ya Wanachama wa CCM wa Majimbo ya Kiembe Samaki na Chukwani wakiwa katika mkutano wa Kampeni wa Kuwanadi Wagombea nafasi za Ubunge, Uwakilishi na Udiwani wa Majimbo hayo uliohutubiwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Kampeni ya CCM Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi.
 Balozi Seif akimnadi Mgombea wa nafasi ya Ubunge wa Jimbo la Kiembe Samaki kupitia Chama cha Mapinduzi Nd. Ibrahin Raza kwenye uwanja wa michezo hapo Kiembe Samaki Wilaya ya Magharibi “B”.

Balozi Seif akimnadi Mgombea nafasi ya Ujumbe wa Baraza la Wawakilishi kupitia Chama cha Mapinduzi Jimbo la Kiembe Samaki Mh. Mahmoud Thabit Kombo.
Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa Balozi Seif akimuombea kura Bibi Mwanaasha Khamis Juma anayewania nafasi ya Uwakilishi kwa tiketi ya CCM Jimbo la Chukwani Bibi Mwanaasha Khamis Juma kwenye Mkutano wa Kampeni zinazoendelea ndani ya Majimbo hayo.
Balozi Seif akiwanadi wagombe wa nafasi za Udiwani katika wadi zote zilizomo ndani ya Majimbo la Kiembe Samaki na Chukwani hapo Uwanja wa Michezo wa Kiembe Samaki.


Wagombea nafasi hizo za Udiwani wa kwanza kulia ya Balozi Seif ni Nd. Maabada Ali Wadi ya Mbweni, Ndugu Maulidi Mwinyi Mzee Wadi ya Mombasa, Nd. Suleiman Muusa Wadi ya Shakani na Nd. Khamis Abdillah Wadi ya Kisauni. Picha na –OMPR – ZNZ.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kampeni ya Uchaguzi ya CCM Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema kwamba endapo CCM itaendelea kushinda tena kwenye uchaguzi Mkuu wa mwaka huu Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itahakikisha kwamba inafuta waraka zote za umiliki wa ardhi zilizochukuliwa kihadaa kwa sura ya uwekezaji.

Alisema wapo baadhi ya watu waliopewa dhamana na Serikali katika kusimamia masuala ya ardhi na wakaamua kutumia vibaya madaraka yao kwa kujilimbikizia maeneo ya ardhi kwa maslahi yao binafsi.

Balozi Seif Ali Iddi alitoa Kauli hiyo wakati akiwanadi wagombea nafasi mbali mbali za Uongozi katika Majimbo Mawili ya Kiembe Samaki na Chukwani kwenye Mkutano wa Kampeni zinazowendelea Nchini uliofanyika katika uwanja wa michezo wa Kiembe Samaki Wilaya ya Magharibi “ B ”.

Alisema tamaa ya watu hao kujilimbikizia maeneo makubwa ya ardhi imechangia kuikosesha mapato Serikali kuu kwa kipindi kirefu jambo ambalo upo uwezekano wa maeneo hayo kupewa wawekezaji wenye nia thabiti ya kutaka kuisaidia Nchi Kiuchumi. 

Akizungumzia siasa za Kampeni zinazoendelea Balozi Seif ambae pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa alisema uwezo wa upinzani wa kudhania kwamba utaking’oa madarakani Chama cha Mapinduzi ni wa kujifurahisha na hatma yake itaishia kuwadanganya wanachama pamoja na wafuasi wao.

Alisema Upinzani utawezaje kuliongoza Taifa wakati viongozi wake wamo ndani ya maamuzi yanayofanywa na Serikali katika Vikao vya Baraza la Wawakilishi na Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania tokea kuanza kwa mfumo wa Vyama vingi vya Siasa Nchini Tanzania kwa takriban Miaka 25 sasa.

Alisema nguvu za Chama cha Mapinduzi katika kutekeleza Sera na Ilani yake iliyofikia zaidi ya asilimia 90% katika kipindi cha Mwaka 2010 hadi 2015 ndio kigezo sahihi kinachotoa ishara kwamba Chama hicho kitaendelea kuungwa mkono na Wananchi walio wengi Tanzania Bara na Zanzibar.

Balozi Seif alijinasibu kwa kuelezea kuwa tabia ya Viongozi na wafuasi wa vyama vya upinzani kuendelea kumlalamikia kila mara hasa kwenye mikutano yao ni dalili za wafuasi hao kuiogopa CCM kutokana na jitihada zake za kuzisimamia Serikali zote mbili katika utekelezaji wa Ilani na sera zake.

Akisisitiza umuhimu wa suala la Amani Nchini hasa katika kipindi hichi cha mpito kuelekea uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika baadae mwezi huu Balozi Seif amnbae pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alisema Serikali kamwe haitokubali kuona Nchi inaelekezwa katika kutiwa kwenye matatizo.

Balozi Seif alitahadharisha na kuwashauri wale watu waliozoea shari, fujo na mchafuko ni vyema wakafanya utaratibu wa kuelekea kwenye nchi zenye vitendo hivyo na sio haa Zanzibar.

Mapema Muasisi wa Jimbo la Chukwani Mzee Ali Hassan Khamis aliwanasihi Wanasiasa hasa wale wa vyama vya upinzani kuacha kutengeneza fitna mbaya na shari kwa kuwahusisha vijana wa Jimbo hilo ambayo kuachiliwa kupaliliwa kwake inaweza kuleta hatari kwa hatma ya vizazi hivyo.

Mzee Ali Hassan alisema Wazee na Wananchi wa Jimbo la Chukwani hawana nia mbaya na viongozi wa Upinzani lakini tabia ya wanasiasa wake ya kupita nyumba hadi nyumba kushawishi pamoja na kuhonga watu ni mwanmzo wa ishara mbaya ya kutaka kuleta fujo na vurugu.

Naye Mbunge Mstaafu wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki Mh. Ummy Aley aliitanabahisha jamii kuwa na hadhari dhidi ya Viongozi wa Vyama vya Upinzani walioamua tumia fedha za Umma kujinufaisha wao binafsi.

Mh. Ummy alisema Wabunge wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na Wale wa Baraza la Wawakilishi wa Chama cha Wananchi CUF wametumia karibu shilingi Bilioni 25 katika kipindi cha miaka Mitano na Shilingi Bilioni Mia 100 katika kipindi cha miaka 20 tokea kuanza kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa.

Katika Mkutano huo ulishirikisha Wanachama vindakindaki wa Majimbo ya Kiembe Samaki na Chukwani Balozi Seif aliwaombea kura kwa Wananchi na Wana CCM wagombea wote wa chama cha Mapinduzi wakati utakapowadia.

Wagombea hao ni Ibrahim Raza Hassananali Ubunge Jimbo la Kiembe Samaki, Mahomud Thabit Kombo Uwakilishi Jimbo hilo la Kiembe Samaki, Bibi Mwanaasha Khamis Juma Ujumbe wa Baraza la Wawakilishi Jimbo la Chukwani, Nd. Maabad Ali Udiwani Wadi ya Mbweni, Nd. Maulid Mwinyi Wadi ya Mombasa, Suleiman Mussa Wadi ua Shakani na Nd. Khamis Abdillah Wadi ya Kisauni.

Othman Khamis Ame


Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar 

No comments: