Advertisements

Wednesday, November 25, 2015

SHUKRANI ZA DHATI

UBALOZI WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
 
SHUKRANI ZA DHATI
Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hapa Marekani, Mhe. Wilson M. Masilingi anatoa shukrani za dhati kabisa kwa watu wote walioshirikiana na Ubalozi wakati wa kuomboleza kifo cha Mtumishi wa Ubalozi, Marehemu Bi. Nyamiti Ivan Lusinde aliyeaga dunia tarehe 17 Novemba, 2015 akiwa likizo nchini Tanzania.

Shukrani za dhati kabisa ziende kwanza kwa Uongozi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa kwa Ushirikiano Mkubwa wa hali na mali walioutoa tangu Marehemu akiwa hospitalini hadi alipopumzishwa kwenye nyumba yake ya milele huko nyumbani kwao Dodoma, Tanzania.

Shukrani za kipekee ziende pia kwa Baba Paroko wa Parokia ya Mt. Edward – Baltimore, Padre Honest Munishi aliyewezesha kwa kiwango kikubwa mafanikio ya Misa Takatifu ya kumwombea Marehemu iliyofanyika Parokiani hapo tarehe 22 Novemba, 2015. Kwa uzito huo huo, Mhe. Balozi anatoa shukrani kwa Padre Lehandry Kimario na Brother James Watson ambao waliungana na Baba Paroko kuadhimisha Misa hiyo.

Aidha, anatoa shukrani za kipekee pia kwa jumuiya ya Watanzania wote wa DMV, Ndugu, Jamaa na Marafiki kutoka nchi mbalimbali walioungana nasi katika kuadhimisha Misa hiyo Takatifu ya kumwombea marehemu. Salamu za rambirambi na misaada mbalimbali mliyoitoa kwa moyo mkunjufu hadi kufanikisha maombolezo na Misa hiyo kwa ujumla, vimekuwa faraja kubwa kwetu na familia ya Marehemu.

Vilevile, Mama wa Marehemu Bi. Agnes Ivan Lusinde na familia nzima wanashukuru sana kwa upendo wenu mliouonesha katika kipindi hiki kigumu walichonacho.

Mwisho, Mhe. Balozi Masilingi anatoa wito kuwa ushirikiano uliooneshwa, uendelezwe wakati wa shida na raha kila vinapotokea kwenye jamii yetu.

Mwenyezi Mungu aipumzishe Roho ya Marehemu Bi. Nyamiti Ivan Lusinde mahali pema peponi, Amina.

No comments: