Advertisements

Sunday, February 14, 2016

WATAKAOTAKA KUHUJUMU MARUDIO YA UCHAGUZI MKUU ZANZIBAR KUKIONA CHA MOTO, ASEMA BALOZI SEIF

Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM Balozi Seif Ali Iddi akiwa na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Nd. Vuai Ali Vuai wakifika Tawi la CCM Kengeja kuangalia hali halisi ya Jengo la Tawi hilo lililotiwa moto na Watu wasiojuilikana usiku wa kuamkia Tarehe 10 mwezi huu.
Balozi Seif na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Nd. Vuai wakilikagua jengo la Tawi la CCM Kengeja lililotiwa moto na watu wasiofahamika usiku wa kuamkia Tarehe 10 Febuari.

Balozi Seif akijionea hali halisi ya baadhi ya sehemu za Tawi la CCM Kengeja ambazo zimeathirika kutokana na moto uliotiwa na watu wasiofahamika.
Baadhi ya Wanachama wa Chama cha Mapinduzi na Wananchi wakimsikiliza Balozi Seif hayupo pichani wakati akiwapa pole baada ya jingo la Ofisi ya Tawi la Kijiji hicho kuuunguzwa moto na watu wasiofahamika. Picha na – OMPR – ZNZ.

Na Othman Khamis, OMPR
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeonya vikali kwamba vyombo vya Dola havitakuwa tayari kuona watu wachache wanatumia hila na vishawishi vya kutaka kuharibu uchaguzi wa marejeo unaotarajiwa kufanyika Mwezi ujao.

Onyo hilo limetolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi wakati akizungumza na anachama wa CCM na wananchi wa Kijiji cha Kengeja mara baada ya kulikagua Tawi la CCM la Kijiji hicho
lililochomwa moto na watu wasiojuilikanausiku wa kuamkia Tarehe 10 mwezi huu.

Balozi Seif alisema alitahadharisha kwamba fujo zozote zitakazotokea kabla na baada ya uchaguzi huo wakukamatwa mwanzo na kupelekewa kwenye vyombo vya Dolan a Kiongozi atakayehusika na kuandaa vurugu hizo.

Aliwaonya watu walioandaliwa kujihusisha na vitendo vya vurugu ikiwemo kufanya hujuma dhidi ya mali na vifaa vya Wananchi yakiwemo majengo ya Kisiasa kuacha mara moja tabia hiyo ambayo hatma yake itapelekea kuwatia hatiani na baadaye kupelekwa kwenye mkondo wa sheria.

Balozi Seif alisema vitendo vya hujuma vinavyoonekana kuibuka nyakati hizi ni vibaya kwa vile vinaathiri maisha ya jamii kutokana na athari za hujuma hizo kuharibu miradi ya wananchi kama mashamba, Majengo ya Skuli nay ale ya Raia pamoja na huduma za Maji safi na salama.

“ Tumeshuhudia miradi inayohujumiwa na baadhi ya watu wakorofi kama mashamba, Skuli, Maji safi na majengo ya Raia athari yake pia huwapata wakorofi hao ”. Alisema Balozi Seif.

Balozi Seif ambae pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi aliwaomba wanachama hao wa Tawi la CCM Kengeja kuwa wastahamilivu kutokana na mkasa uliowakumba wa kutiliwa
Moto Jengo la Tawi lao.

Alisema Vyombo vya Dola bado vinaendelea kufanya uchunguzi wa kuwabaini watu waliohusika na vitendo hivyo wakiwemo wale watu wanaoendeleza kauli za chuki, hujuma na na kutaka kuleta vurugu hapa Nchini.

Balozi Seif aliwahakikishia Wanachama na Wananchi hao kwamba Serikali itajizatiti kuongeza ulinzi wa kutosha utakaoleta faraja kwa Umma hasa katika kipindi cha mpito kuelekea kwenye uchaguzi wa marudio wa mwezi
ujao wa machi.

Alisema uhuru wa Jamii utalindwa ili kumpa fursa kila Mwananchi kuitumia haki yake ya Kidemokrasia kumchagua Kiongozi anayestahiki amtumikie katika uchaguzi huo wa marejeo.


Mapema Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Nd. Vuai Ali Vuai amnbae alikuwepo kushuhudia athari ya kuungua kwa Tawi hilo la CCM Kengeja alisema kilichopo kwa Wanachama wa CCM hivi sasa ni kusubiri kupiga

kura ya marejeo ifikapo Tarehe 20 mwezi ujao.

Nd. Vuai aliwataka wanachama hao wa Chama cha Mapinduzi kuzipa mgongo hila zilizozoeleka kufanywa na baadhi ya wanasiasa za kudanganya wananchi hali ya kisiasa inavyokwenda nchini ambazo tayari zimeshafikia ukingoni.

Alifahamisha kwamba CCM muda mwingi ilikuwa tayari kuridhia kila kitu katika kuiona nchi inaendelea kubakia salama na hatimae kufikia suluhu ya kuundwa kwa Serikali na Umoja wa Kitaifa Zanzibar lakini upande mwengine wa upinzani unashindwa kufahamika hasa unataka nini.

Naibu Katibu Mkuu huyo wa CCM Zanzibar alitoa wito kwa Wanachama na Viongozi wa chama cha Upinzani cha CUF kufikiri kwanza kabla ya kuamua mambo wanayotaka kuyatekeleza vyenginevyo maamuzi yao ya awali ndio
yanayowapelekea kwenye matatizo.

Akizungumzia kadhia iliyowakumba Wana CCM wa Tawi la Kengeja ya kuchomwa moto kwa Jengo lao la Ofisi ya Chama Nd. Vuai alisema watu waliofanya vitendo hivyo wanaonekana kutokuwa na huruma na Binaadamu

wenzao.

Alisema kitendo hicho kinaendelea kulaaniwa na Chama Cha Mapinduzi kwa vile athari ya janga hilo kulingana na mazingira ya eneo lililozunguuka jengo hilo ingekuwa inazungumzwa vyengine kutokana na ukaribu mkubwa wa majengo mengine ya Wananchi yaliyopembezoni mwa Tawi hilo.


Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Vuai aliviomba vyombo vya Dola kutosubiri kutokea maafa wakati watu wanaoashiria matamshi ya shari wanaeleweka katika maeneo mbali mbali Nchini.

Alieleza kwamba vyombo hivyo vina wajibu na haki ya kuwadhibiti watu wenye tabia hiyo. Hadi sasa athari ya gharama zilizotokea kutokana na janga hilo la moto ulioathiri baadhi ya sehemu za paa, mlango na Boriti katika Tawi hilola CCM Kengeja bado hazijafahamika.

2 comments:

Anonymous said...

mtatoka tu watanganyika Zanzibar in shaa Allah bi idhni laan.

utakioana wewe cha mtema kuni kwani wewe mungu.usijifanye jemedari jemedari Allah peke yake.

Anonymous said...

Kuchoma moto kunakusaidia nini wewe mdau wa hapo 5:39 PM? Siku moja wewe na wenzio mtashikwa na kujutia. Serikali ni kubwa kuliko nyie wahalifu, mtapata kichapo kama kile walichopewa waarabu mwaka 1964.