Advertisements

Tuesday, June 28, 2016

WAGANGA WA TIBA ASILI NA TIBA MBADALA WATAKIWA KUJISAJILI ILI WATAMBULIKE KISHERIA

Na Lilian Lundo, MAELEZO – Dodoma 
Waganga wa tiba asili ambao wamekuwa wakitoa huduma ya tiba pasipo kujisajili wametakiwa kujisajili Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala ili waweze kutambulika kisheria. 

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Hamis Kigwangalla (pichani) ameyasema hayo leo, Bungeni Mjini Dodoma alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge Viti Maalum Mhe. Zainabu Mussa Bakar juu ya udanganyifu unaofanywa na waganga wa tiba asili wa kutoa dawa feki kwa wagonjwa. 

“Waganga wa tiba asili wapo kisheria, ni kweli wapo wanaotoa dawa feki, na wengi wao ni wale ambao hawajasajiliwa, hivyo tumewaagiza kujisajili ili tuweze kuwatambua na dawa zao ziweze kuhakikiwa na kusajiliwa kwa ajili ya matumizi ya binadamu,” alifanunua Mhe. Kigwangalla. 


Mhe. Kigwangalla amesema kuwa, mganga yoyote atakaye kiuka agizo hilo la kujisajili basi hatua kali zitachukuliwa dhidi yake. Aidha, amesema Wizara iko makini na ufuatiliaji wa dawa feki nchini kwani wanapopata fununu ya uwepo wa dawa feki hutuma kikosi kuchunguza na ikibainika kuwa dawa ni feki basi hatua kali huchukuliwa kwa muhusika. 

Aliendelea kwa kusema kuwa, ili kudhibiti uingizwaji wa dawa feki nchini Wizara hiyo hufanya uhakiki wa muda mrefu kuchunguza iwapo dawa inayopendekeza kuingia nchini siyo feki na inafaa kwa matumizi ya binadamu, ikiwa dawa haina madhara yoyote basi inasajiliwa kwa ajili ya kuingia sokoni. 

Vilevile Mhe. Kigwangalla amesema kuwa, Wizara imewaagiza waganga wa tiba asili kufunga dawa zao kwa kutumia vifungashio maalum vya madawa ambavyo vitasaidia dawa hizo kuendelea kuwa salama kwa mtumiaji kwa kipindi kilichopangwa kutumika.

No comments: