Tuesday, June 14, 2016

WAVUVI WATATU WAFA ZIWA VICTORIA

Watu watatu wamekufa maji baada ya boti yao ya uvuvi kuzama ndani ya Ziwa Victoria kutokana na dhoruba kali lililowapiga katika eneo la Nyamkazi Manispaa ya Bukoba, mkoani Kagera.
Mwenyekiti wa mtaa wa Nyamukazi lilipotokea tukio hilo, Andason Lazaro amesema wavuvi hao waligundulika kuzama maji baada ya kutoonekana tangu Juni 9, mwaka huu.
“Baada ya kutowaona kwa muda mrefu, juhudi za kuwatafuta zilianza na miili yao kubainika wakiwa tayari wamefariki dunia,” amesema Lazaro.
Waliofariki katika ajali hiyo wametambuliwa kwa jina moja moja la Audax na Seperatus, wakati mtu wa tatu hajatambulika.
Diwani wa Kata ya Miembeni, Richard Gasper amesema ofisi yake imepokea taarifa za ajali na vifo hivyo na kuwataka wavuvi kuzingatia kanuni na taratibu za usalama ikiwemo kuvaa mavazi maalumu ya kuelea juu ya maji wakati ajali inapotokea.

No comments: