Advertisements

Monday, July 18, 2016

SIFA ZA MFUNGWA WA PAROLE NA UAMUZI WA BODI ZA PAROLE UNAVYOFANYIKA HAPA NCHINI



Na, Lucas Mboje - Jeshi la Magereza,
SIFA ZA MFUNGWA WA PAROLE
Sheria ya Bodi za Parole Sura 400 ya mwaka 2002 na Kanuni zake za mwaka 1997 inaainisha kuwa mfungwa anayetumikia kifungo cha kuanzia miaka minne (4) na kuendelea anastahili kunufaika na mpango wa Parole kama atakuwa na sifa zifuatazo:-
i) Asiwe amehukumiwa kifungo cha maisha;
ii) Asiwe ni mfungwa anayetumikia kifungo kwa makosa ya unyang’anyi wa kutumia silaha, madawa ya kulevya na makosa yanayohusiana na kujamiiana;
iii) Asiwe ni mfungwa ambaye kifungo chake kimebatilishwa kutoka kwenye kifungo cha kunyongwa;
iv) Awe anatumikia kifungo kisichopungua miaka minne (4) au zaidi na awe ametumikia 1/3 ya kifungo chake;
v) Awe ameonesha tabia na mwenendo mzuri kwa muda wote aliokaa gerezani na;
vi) Asiwe na pingamizi la kimahakama la kukataliwa kunufaika na utaratibu wa Parole chini ya Kifungu cha 67 cha Sheria ya makosa ya Jinai.

UAMUZI WA BODI ZA PAROLE UNAVYOFANYIKA HAPA NCHINI

Kimsingi mfungwa anapoingia gerezani kwa mara ya kwanza hujulishwa kuhusu haki zake ikiwemo haki ya kuingizwa kwenye mpango wa Parole kama ana sifa kulingana na kosa lake na muda wa kifungo chake gerezani.

Mfungwa mwenye sifa ya kuingizwa kwenye mchakato wa Parole anapotimiza 1/3 ya kifungo chake, Afisa Parole hukusanya taarifa mbalimbali zinazomuwezesha kujadiliwa katika Bodi za Parole; Taarifa hizo ni maoni kutoka kwa wazazi/ndugu zake, maoni ya mwathirika wa uhalifu, nakala ya hukumu, hati ya kifungo, maoni kutoka uongozi wa kijiji anachotarajia kwenda kuishi na maoni/taarifa kutoka Kituo cha Polisi kilichomkamata na pia matokeo ya uchunguzi wa alama zake za vidole kuhusu kumbukumbu zake za uhalifu. Taarifa hizi zote huwa ni kwa ajili ya kudumisha usalama wa jamii na wa mfungwa mwenyewe anufaikapo kwa Parole.

Baada ya Taarifa hizi zote kukamilika kila mfungwa anayependekezwa kunufaika na Parole hufunguliwa jalada (Prison Form. 64) kwa ajili ya kutunza kumbukumbu zake pamoja na taarifa za tabia na mwenendo wa mfungwa. Mchakato wa kumjadili mfungwa huanzia katika Kamati za Urekebishaji ya Gereza. Kamati hiyo hupitia taarifa hizo na kutoa maoni na mapendekezo kwenda Bodi ya Parole ya Mkoa. Bodi ya Parole ya Mkoa hupitia maoni na mapendekezo hayo na baada ya uchambuzi wa kina, hutoa mapendekezo yake kwa Bodi ya Taifa ya Parole kupitia kwa Sekretarieti ya Bodi ya Taifa ya Parole.

Sekretarieti ya Taifa ya Parole ina jukumu la kuratibu shughuli zote za Bodi. Hivyo hupokea taarifa za wafungwa waliopendekezwa au kutopendekezwa kunufaika na Parole kutoka katika Bodi za mikoa. Huchambua taarifa hizo na kuandaa taarifa ya kila mfungwa kwa ajili kujadiliwa na Bodi ya Taifa ya Parole.

Bodi hiyo kwa kutumia taaluma mbalimbali walizonazo wajumbe wake na nyadhifa zao hufanya uchambuzi wa kina wa mawasilisho hayo na kutoa uamuzi wa mfungwa anufaike au asinufaike na Parole. Uamuzi wa Bodi ya Taifa ya Parole huwasilishwa kwa Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi kwa uamuzi wa mwisho kwa mujibu wa Kifungu cha 6(4) cha Sheria ya Bodi za Parole Na. 25 ya mwaka 1994 (Sura ya 400 R. E 2002).

Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi hupitia taarifa za kila mfungwa na kutoa uamuzi wa mwisho wa kukubaliwa au kukataliwa kunufaika kwa mpango wa parole. Uamuzi huo huwasilishwa kwa Katibu wa Bodi ya Taifa ya Parole ambaye ni Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza Tanzania. Itaendelea...... !.


MWANDISHI WA MAKALA HII NI AFISA NGAZI YA JUU WA JESHI LA MAGEREZA, KWA MAONI NA USHAURI - 0754 871084, lucasmboje@yahoo.co.uk or mbojelucus@gmail.com

No comments: