Advertisements

Friday, August 12, 2016

FAINI YA SHILINGI MILIONI 128 YAISUBILI YANGA

Ofisa Habari wa TFF, Alfred Lucas
Ofisa Habari wa TFF, Alfred Lucas

KLABU ya Yanga inakabiliwa na faini ya Sh milioni 128 kwa uzembe wa kuchelewa kufanya usajili wake kwenye mtandao wa kimataifa (TMS).

Yanga ambayo tayari utetezi wake umetua Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), iwapo utakubaliwa klabu hiyo ya mtaa wa Jangwani italazimika kumlipia kila mchezaji dola za Marekani 500 na klabu hiyo ina wachezaji 27 ambao italazimika kuwalipia dola za Marekani 13500 ( sawa na Sh milioni 128).

Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Alfred Lucas aliiambia HabariLeo jana kuwa kwa mujibu wa kanuni ya 60 (12) inayozungumzia masuala ya usajili, iwapo Fifa na CAF (Shirikisho la Soka Afrika) zitaridhia utetezi wa Yanga basi adhabu ya faini haiepukiki.

Mbali na Yanga, timu nyingine ambayo inakabiliwa na adhabu hiyo ni Coastal Union ya Tanga ambayo ipo kwenye hatari ya kushushwa daraja hadi wilayani.

“Iwapo watakubaliwa utetezi wao ili kuwafungulia usajili timu za Ligi Kuu zitalazimika kumlipia kila mchezaji dola 500 na pia kwa zile timu ambazo hazikukamilisha usajili wake vizuri zinakabiliwa na faini ya Sh milioni tatu”.

“Kwa timu za daraja la kwanza na la pili ambazo usajili wake ulikuwa na kasoro zinaweza kukumbwa na faini ya Sh 300,000 mpaka milioni tatu 3,” alisema.

Timu ambazo usajili wake ulikuwa na kasoro ni African Lyon, Kiluvya United, Mashujaa, Friends Rangers, Abajalo, Kitayosa na Mvuvuma. Dirisha la usajili wa Ligi Kuu Bara lilifungwa Agosti 6 saa sita kamili usiku, huku Yanga na Coastal Union zikiwa ni timu pekee ambazo hazijawasilisha usajili wake.

Timu ambayo imeshindwa kutuma usajili wake TMS moja kwa moja inakuwa imeondolewa kwenye ligi.

“Utetezi inabidi ukubaliwe na FIFA ndiyo dirisha lifunguliwe, ukikataliwa hiyo timu inateremka hadi daraja ambalo halimo kwenye usajili wa mfumo wa TMS, ambalo huku kwetu ni la tatu,” alisema Lucas.

Lucas alisema mwaka jana pia TFF ilichelewa kukamilisha usajili, ikaomba FIFA iwafungulie dirisha baada ya ufafanuzi mzito, lakini bado walitozwa faini.

HABARI LEO

No comments: