Advertisements

Wednesday, August 17, 2016

MTOTO AJINYONGWA KWA CHANDARUA



Na Yeremias Ngerangera-Namtumbo



Mtoto Zawadi Hasani (14) wa kitongoji cha Majengo katika kijiji cha Mkongo wilayani Namtumbo Mkoani Ruvuma amejinyonga kwa kutumia chandarua chake akiwa chumbani kwake baada ya kuchoshwa na kauli zisizo na staha kutoka kwa mama yake.



Tukio hilo limetokea hivi karibuni ,ambapo mwili wa marehemu ulikutwa chumbani kwake asubuhi siku ya ijumaa baada ya mama yake mzazi kumtaka aamke na ndipo jitihada zake za kumtaka aamke kwa kumwita mlangoni zilipogonga mwamba aliamua kufungua mlango na kuukuta mwili wa mwanae ukiwa juu ukining’inia.



Mtendaji wa kata ya Mkongo Whclif Mlinda alifika katika eneo la tukio na kuthibitisha kifo cha kijana huyo kilichosababishwa na kujinyonga kwa kutumia chandarua kutokana na kauli zisizo na staha kutoka kwa mama yake mzazi huyo marehemu.



Kwa mujibu wa bwana Mtinda amesema kuwa kabla ya kwenda kulala marehemu alikuwa anadai hela yake kutoka kwa mama yake ambazo alimpa mama yake huyo amwekee na alipozihitaji kuzichukua kauli zisizo na staha zilitolewa na mama huyo kwa mwanae na kuibuka sintofahamu kati yao.



Malumbano ya mama huyo na mwanae yaliendelea usiku huo hatua iliyofikia mama huyo kumtaka mwanae aondoke na aende akaishi na baba yake mzazi kwa kuwa baba ya marehemu na mama huyo waliachana na marehemu aliamua kwenda kuishi na mama yake huyo.



Aidha kitendo cha mama huyo kumweleza mtoto wake aende akaishi kwa baba yake na kumnyima fedha yake aliyoiweka kwake ndicho kilichomkasirisha kijana huyo na kisha kuamua kujinyonga alisema bwana Mtinda.



Marehemu amezikwa kijiji cha Mkongo na kumwacha mama yake katika hali ya kutoamini kilichotokea kwa madai kuwa uamuzi aliouchukua mwanae wa kujinyonga unamwumiza moyoni na utaendelea kumwumiza moyoni alisema mama huyo.

No comments: