Advertisements

Saturday, September 24, 2016

CHADEMA YALAANI DIWANI KUSWEKWA RUMANDE

Katibu wa CHADEMA jimbo la Arumeru Mashariki Elisa Stephen Mungure (Kulia) akiteta jambo na Diwani wa Kata ya Embaseny Gadieli Mwanda (kushoto) nje ya Mahakama ya Mwanzo ya Enaboishu jana mara baada ya kuwekwa rumande kwa saa 48 na mkuu wa wilaya ya Arumeru ambapo jana alifikishwa mahakamani na kupewa dhamana



      Na Woinde Shizza, Arusha 
Chama cha Demokrasia na Maendeleo Wilaya ya Arumeru Mashariki kimelaani vikali kitendo cha Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Alexender Mnyiti kumuweka rumande Diwani wa Kata ya Embaseny Gadieli Mwanda kwa saa 48 na kudai kuwa kitendo hicho ni matumizi mabaya ya madaraka. 

Katibu wa CHADEMA Wilaya ya Arumeru Elisa Stephen Mungure amesema kuwa kitendo hicho ni udhalilishaji dhidi ya viongozi wa upinzani ambao wamekua wakikamatwa mara kwa mara na kuwekwa rumande . 

Mungure alisema kuwa mbinu hiyo imekua ikitumika kwa hila ili kudhoofisha na kuua upinzani hivyo chama chake kimejipanga kukabiliana na hila hizo za kisiasa. 

“Diwani wa Kata ya Embaseny alitakiwa kuripoti katika kituo cha polisi cha Usariver septemba 20 mwaka huu ndipo alipokutana na Amri ya Mkuu wa Wilaya ya kuwekwa ndani kwa masaa 48 bila kuhojiwa ,jana alifikishwa mahakama ya Mwanzo ya Enaboishu na kutuhumiwa kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu kupitia mradi wa Kuku Kukua ambao Diwani huyo siyo muhusika ,tunamshukuru Mungu amepata Dhamana” Alisema Mungure 

Akizungumza baada ya kupata Dhamana katika mahakama hiyo Diwani huyo Gadiel Mwanda ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema jimbo la Arumeru Mashariki alisema kuwa Mkuu wa Wilaya alifanya ziara katika kata yake na kuzungumza na Wananchi ,baadhi ya watu ambao wanadaiwa kuwa ni wafuasi wa CCM walimshutumu kuwa anahusika na mradi huo alipotaka kujitetea alinyimwa nafasi hiyo na kuamriwa kufika kituo cha polisi asubuhi na mapema ndipo alipokutwa na masaibu hayo. 

Mwanda alisema kuwa misigano ya kisiasa inayotekea inalenga kuzorotesha juhudi za maendeleo ambazo amekua akizifanya kwa kushirikiana na wananchi jambo ambalo litawaathiri wananchi wengi hivyo amewataka wananchi kuendelea na juhudi hizo ikiwemo ujenzi wa zahanati ya kisasa. 

Kwa upande wao wananchi wa kata hiyo Ester Swai na Agnes Elia wamesema kuwa kukamatwa kwa viongozi kila mara kunazua hali ya taharuki miongoni mwa wananchi hivyo wamezitaka mamlaka husika kutimiza majukumu yao kwa kuzingatia misingi ya haki na usawa.

No comments: