Advertisements

Friday, September 23, 2016

IPTL YAGEUZIWA KIBAO SAKATA LA ESCROW, YATAKIWA KUIREJESHEA TANESCO BILIONI 216

Kampuni  ya Kufua Umeme ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL) imegeuziwa kibao katika suala la Escrow, imefahamika.

Kampuni hiyo imetakiwa kurejesha zaidi ya Dola za Marekani milioni 100   (Sh bilioni 216.2 ) kwa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco)  zikiwa fedha za  ziada ambazo  ililipwa kabla ya hesabu kufanywa upya.

Hatua hiyo inatokana na uamuzi wa Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi wa Biashara uliotolewa Septemba 12 mwaka huu unaoitaka Tanesco kuilipa Chartered ya Hong Kong (SCB-HK) Dola za Marekani milioni 148.

Mahakama hiyo ilitoa uamuzi huo kutokana na kesi iliyofunguliwa na Benki ya Standard Chartered ya Hong Kong (SCB-HK) dhidi ya Tanesco ikidai kulipwa Dola za Marekani milioni 369.

Kwa mujibu wa Wakili wa Tanesco, Richard Rweyongeza, amesema walichokuwa wanabishania mahakamani si Tanesco kulipa bali walikuwa wanabishania shirika hilo litalipa kiasi gani na linamlipa nani.


“Kabla hatujaingia katika kutetea kesi hiyo, mwaka 2014 mahakama hiyo ilisema inayo madaraka na ikaamuru Tanesco kuilipa  SCB-HK.

“Sisi tuliingia kutetea baada ya uamuzi huo,  Mei, 2014 tukaomba hesabu zifanyike upya kwa malekezo yaliyotolewa na mahakama hiyo  kujua deni halisi.

“Hesabu zilipofanyika kwa mtaji wa mwekezaji, walichukua mkopo wakahesabu kuwa ni mtaji, hatua hiyo ilikataliwa na mahakama.

“Kabla ya hesabu kufanyika ndipo likaingia suala la akaunti ya Tegeta Escrow. Fedha zilipochukuliwa katika akaunti hiyo, SCB-HK wakabadilika wakasema hakuna haja ya kufanya hesabu upya kwa sababu Tanesco wamekubali viwango hivyo ndiyo sababu waliwalipa IPTL.

“Tulibishania hoja hiyo ya kulipa kwa viwango vya zamani ikaamuriwa hesabu zifanyike upya, mahakama ilikubali hesabu ifanyike kwa kutumia mkopo wa wana hisa.

“Baada ya kuamuru hivyo, deni likashuka kutoka walichokuwa wakidai Dola za Marekani milioni 369 hadi kuamuriwa kulipa Dola za Marekani milioni 148,”anasema Wakili Rweyongeza.

Alisema IPTL walilipwa Dola za Marekani milioni 246 kwa kutumia viwango vya zamani na kwamba uamuzi uliotolewa unaanza kutumika katika kipindi chote ambacho Tanesco ilikuwa inadaiwa mpaka mwaka 2015.

“Kutokana na hesabu hizo gharama ilikuwa chini, IPTL ililipwa zaidi hivyo inatakiwa kurejesha Dola za Marekani zaidi ya milioni 100 kwa Tanesco,”alisema.

Rweyongeza alisema walipendekeza SCB-HK wadai fedha zao kwa IPTL lakini mahakama hiyo ilikataa na kuamuru Tanesco ndiyo walipe hivyo kwa mtazamo wa kawaida IPTL inatakiwa kurejesha fedha kwa shirika hilo.

Katika kuhitimisha, mahakama hiyo ilisema pande zote mbili zinazopingana zilishinda katika maeneo muhimu waliyokuwa wakibishania lakini zilipoteza katika hoja nyingine.

Baada ya kumaliza kusikiliza kesi hiyo mahakama iliamuru pande hizo mbili kulipa gharama za usuluhishi na nyingine kwa viwango sawa.

Malipo hayo na anayelipwa katika mabano ni Dola za Marekani 254,775.02 (Profesa MC Rae), Dola 171,278.36 (Profesa Douglas) na Dola 370,126.76 kwa ajili ya Profesa Stem.

Gharama nyingine zilizokadiriwa moja kwa moja ni Dola za Marekani 157,336.26 na gharama za utawala kwa mahakama hiyo Dola za Marekani 180,000 ambako jumla ya gharama zote wanazotakiwa kulipa Tanesco na SCB-HK ni Dola za Marekani 1,133,516.42.

Hata hivyo Rweyongeza alisema pamoja na ushindi huo hawakuridhishwa na uamuzi huo kwa sababu katika uamuzi wa kwanza, mahakama hiyo ilikataa hesabu kupigwa kwa kutumia kiwango cha 22.31 lakini bado katika uamuzi huu walitumia kiwango hicho kufanya hesabu hivyo walikosea kufanya hivyo.

Hoja ya pili, alisema SCB-HK si mwekezaji hivyo hakustahili kupeleka kesi hiyo mahakamani na kwamba hapakuwa na hoja.

“Sababu nyingine ya kutoridhishwa na uamuzi huo ni kwamba hatukupewa nafasi ya kujibu hoja mpya zilizowasilishwa kuhusu Tanesco kwamba ilidanganya, tulipaswa kujibu kwa maelezo ya mashahidi si mawakili.

“Tuliwasilisha hoja kwa maandishi, zilipotokea hoja mpya tulitakiwa kuzijibu kwa kuleta mashahidi, tunapinga pia uamuzi ulioitambua SCB-HK kuwa ilistahili kisheria,”alisena Rweyongeza.

Suala hilo limeibuka ikiwa imepita miaka mitatu tangu Serikali kupitia Mwanasheria Mkuu wa Serikali na viongozi wa Wizara ya Nishati na Madini kuruhusu kufanyika kwa malipo ya Dola za Marekani milioni 200 (zaidi ya Sh bilioni 300) kutoka katika Akaunti ya Tegeta Escrow iliyokuwa imefunguliwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Fedha hizo zilitolewa na kwenda kwa mmiliki wa Kampuni ya Pan Africa Power Solutions Tanzania Limited (PAP), Harbindar Singh Sethi mwenye makazi yake nchini na Afrika Kusini.

Katika kesi hiyo Tanesco ilikuwa inawakilishwa na mawakili wa kampuni za R.K Rweyongeza & Advocates na Crax Law Partners.

Chanzo cha Escrow
Mwanzoni mwa miaka ya 1990  nchi ilikuwa na upungufu wa umeme kutokana na upungufu wa maji kwenye mabwawa, ambapo 1994 serikali ilitoa kazi ya uwekezaji kwa IPTL ilikuwa iliyokuwa ikimilikiwa na VIP ya Tanzania iliyokuwa na asilimia 30 na Mechmar ya Malaysia yenye asilimia 70.

Tanesco na IPTL walisainiana mkataba wa miaka 20, hata hivyo uzalishaji haukuanza mara moja kutokana na mgogoro ulioibuka baina yao (Tanesco na IPTL) .

Mwaka 2002  IPTL ilianza kuzalisha umeme na mkataba ukaanza kuhesabiwa hapo, lakini kutokana na mgogoro ikafunguliwa akaunti ya Escrow na mwaka 2004 Tanesco ilifungua shauri kupinga tozo la Capacity Charge

Uwiano wa mtaji ni 70 kwa 30 na uamuzi haujabadilishwa na mahakama yoyote. Mwaka 2004 Kampuni ya Mkono &  CO advocates iliishauri Tanesco iendelee kupinga Capacity Charge London.

Inaelezwa kuwa Agosti 2005, benki ya SCB-HK ilinunua kwa bei ya punguzo ya dola za Marekani 76.1 kutoka Benki ya Malaysia ya Danaharta baada ya kushindwa kurejesha deni la muda mrefu kutoka IPTL.

Bei halisi ya deni hilo ilikuwa ni dola milioni 101.7 kwa mujibu wa ushahidi uliopo ambako IPTL ilikopa dola milioni 100 mwaka 1998 kutoka kwa mbia wa benki ya Malaysia ili kujenga mtambo wa kufua umeme wa megawati 100 wa Tegeta.

Kwa mujibu wa  makubaliano hayo, SCB-HK ilipewa kandarasi kadhaa ikiwamo haki ya kulipwa deni la 1997, ambako mkataba wa utekelezaji na hatia ya makubaliano ya dhamana iliyosainiwa  kati ya IPTL na Serikali.

Fedha zilivyotolewa
Akaunti ya Tegeta Escrow ilifunguliwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kwa kuhifadhi fedha za malipo ya tozo ya ufuaji umeme baada ya Tanesco kuingia kwenye mgogoro na Kampuni ya IPTL  na  suala hilo lilipelekwa mahakamani.

Kwa mujibu wa masharti ya uendeshaji wa akaunti ya Escrow, fedha zilitakiwa zitolewe baada ya Mahakama kutoa uamuzi wa mgogoro huo, lakini wakati ilitaka pande hizo mbili zikutane na kukokotoa viwango vya tozo, fedha hizo zilitolewa na kulipwa mmiliki wa Kampuni ya Pan Africa Power Solution (PAP) jambo lililosababisha kuibuka  kashfa hiyo.

Ilivyotua bungeni
Aliyekuwa wa kwanza kulifikisha bungeni suala hilo ni aliyekuwa Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila, ambaye aliwalipua baadhi ya mawaziri wa Serikali ya awamu ya nne kuhusika na mpango huo.

Hatua hiyo ilisababisha Spika wa Bunge la 10 kuagiza uchunguzi wa vyombo vya dola  kuweza kuchimbua kwa undani wizi huo.

Baada ya kukamilika ilikabidhiwa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAP) chini ya aliyekuwa Mwenyekiti wake Zitto Kabwe na Makamu wake, marehemu Deo Filikunjombe.

Novemba 28 mwaka  2014, Bunge la 10 lilitoa maazimio manane kuhusu suala  hilo huku Harbinder Singh Sethi, James Rugemalira  wa (VIP), aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Umeme wa Umeme Tanzania (TANESCO) walionekana kuhusika kwa namna moja au nyingine katika kufanikisha kufanyika miamala haramu ya fedha za Akaunti ya Escrow ya Tegeta kwenda Pan African Power Solutions Ltd (PAP) na VIP.

Bunge pia liliazimia mawaziri wa wakati huo wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo,  Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Fredrick Werema, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini wa kati huo, Eliachim Maswi na wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa TANESCO wawajibishwe kwa kuishauri mamlaka yao ya uteuzi kutengua uteuzi wao.

Mawaziri hao walipoteza nyadhifa zao huku Profesa Muhongo akijiuzulu na Tibaijuka uteuzi wake ukifutwa na Rais wa awamu ya nne, Jakaya Kikwete.

Credit: Mtanzania

No comments: