Advertisements

Monday, October 17, 2016

Waliotorosha makontena 100 bandari kusakwa

Serikali yawataka wafanyakazi TBS kujisalimisha

Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam

SIKU chache baada ya kuripotiwa kupitishwa bila kukaguliwa makontena 100 katika Banadari ya Dar es Salaam, Serikali imesema inaendesha msako mkali kuwabaini wafanyakazi waliohusika na mpango huo.

Vilevile imewataka baadhi ya wafanyakazi wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS) walioshirikiana na wenzao wa Mamlaka ya Mapato (TRA) kupitisha makontena hayo bila kukaguliwa, wajisalimisha haraka.

Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage, alitoa agizo hilo Dar es Salaam juzi katika uzinduzi wa Baraza la Wafanyakazi wa Shirika la ViwangoTanzania (TBS).

Alisema tayari ameanza kukusanya orodha ya majina ya watu waliosaidia kupitisha makontena hayo kinyume cha sheria.

“Nimeanza kukusanya orodha ya majina ya watu waliosaidia kupitisha makontena haya na nikija nayo hawatapona,” alisema.

Aliwataka wote wanaojijua kuhusika, kujisalimisha mapema na kutubu ili wasamehewe kabla hatua kali za sheria hazijachukuliwa dhidi yao.

Makontena hayo yalipitishwa katika bandari ya Dar es Salaam hivi karibuni bila ya kuthibitishwa na shirika hilo hali iliyozua taharuki huku kila upande ukitupia lawama wenzake.

Waziri Mwijage, aliitaka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuacha kutoa makontena bila ya shirika hilo kuthibitisha au kukagua ubora wa bidhaa zinazoingizwa nchini kwa sababu mwenye mamlaka hiyo ni TBS.

Alisema watakaotubu kuwa walishiriki waseme walishiriki vipi na lini, walishirikiana na nani na wataje sehemu yalikopelekwa makontena hayo serikali iweze kusaidia kukomesha hali hiyo.

Mwijage alisema anaamini waliofanya hivyo katika mamlaka hiyo walifanya kwa utashi wao bila ya ushiriki wa viongozi wao na sasa wakati umefika wa kukomesha tabia hiyo.

Akizungumzia Baraza la Wafanyakazi, Mwijage alilitaka baraza hilo kushirikiana na menejimenti kuhakikisha matatizo yanayojitokeza yanapatiwa ufumbuzi kwa masilahi ya nchi na Serikali itahakikisha inaongeza vitendea kazi na watumishi ili kufikia malengo ya shirika.

Awali, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Dk. Egid Mubofu, alisema baraza hilo lina wajumbe 48 wanaotoka katika vitengo mbalimbali.

Alisema wafanyakazi wanatakiwa kufanya kazi kwa weledi na uadilifu katika majukumu yao ya kila siku.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi (TBS), Profesa Mekanya Maboko, alilitaka baraza hilo kufanya kazi kwa kushirikiana na menejimenti na bodi kuhakikisha shughuli za udhibiti wa ubora zinafanyika kwa ufanisi.

MTANZANIA

No comments: