Advertisements

Tuesday, November 1, 2016

WAHARIRI WAMUANGUKIA RAIS MAGUFULI

Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) limemwomba Rais John Magufuli kumshughulikia Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, Peter Serukamba kwa maelezo kuwa ni ‘jipu’ ambalo limevuruga mjadala wa Muswada wa Huduma za Habari.

Hayo yalibainishwa jana Dar es Salaam wakati wahariri wa vyombo vya habari walipokuwa wakijadili vipengele vya Muswada huo ambavyo vinatakiwa kufanyiwa mabadiliko kabla ya kupitishwa kuwa sheria kwa kuwa si rafiki kwa tasnia ya habari nchini.

Mhariri Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya New Habari Limited, Absalom Kibanda alisema Serukamba ni ‘jipu’ na kumwomba Rais aamini hivyo, akibainisha kwamba kipindi cha aliyekuwa Waziri wa Habari, Fenella Mukangara walipeleka hati ya dharura kutaka Muswada huo ujadiliwe vizuri, lakini alikataa huku akiunga mkono kama ulivyo.

“Kuna sauti ilisikika ikitembea katika mitandao, nikajiuliza ameongea kama Waziri, Ofisa Habari wa Serikali au mtu binafsi?” Alihoji Kibanda.

Kibanda alimwomba Rais aangalie ni nani wasemao ukweli kati ya wadau wa habari (wahariri na waandishiwa habari) na mamlaka nyingine za Serikali kuhusu namna nzuri ambayo Muswada huo unaweza kujadiliwa na kuwa sheria kwa maslahi ya Taifa bila kukwaza upande.

Aidha, alibainisha kuwa kuna watendaji wa Serikali ambao wamekuwa wakimsukuma Waziri wa Habari, Utamaduni, Wasanii na Michezo, ili aridhie mahitaji yao kwa maslahi binafsi.

Alisema kwa sasa waandishi wa habari wanafananishwa na wahalifu na kusema hivi karibuni walichapisha habari kwenye gazeti lao na walikuja kuomba radhi baada ya kupokea vitisho.

Aliongeza kuwa Muswada huo ulitakiwa uwekwe vipengele vinavyowachukulia hatua watu wanaoingilia kazi za vyombo vya habari, kwa kuwa makosa mengi vinayotupiwa vyombo vya habari vyanzo huwa ni wanasiasa.

Mjumbe wa TEF, Jesse Kwayu alisema wana wasiwasi na msimamo wa Serukamba, kwa kuwa anashindwa kutimiza majukumu yake ya kuisimamia Serikali na badala yake anakuwa kama ni ofisa wa Serikali.

“Wakati akiusoma Muswada huu kwenye Kamati, akihitimisha alisema hakuna uhuru usio na mipaka,” alisema Kwayu.

Alibainisha kuwa Mwenyekiti wa Kamati hiyo aliyepita, alisikiliza vizuri mapendekezo ya wadau wa habari na kuyafikisha bungeni yajadiliwe tofauti na wa sasa ambaye si msikivu.

Alisema wakati wakiujadili hivi karibuni Dodoma ilifika mahali kukawa na mvutano mkali kati ya Serukamba na Zitto Kabwe kwa kuwa alikuwa hajaridhishwa na namna Muswada huo ulivyojadiliwa, kwa sababu wadau wa habari wahusika hawajahusishwa kikamilifu.

Alisema asilimia 80 ya waandishi wa habari wako mikoani ambako waandishi hao pia hawajajadili na kupata mwafaka wa Muswada huo.

Naibu Mhariri Mtendaji wa Jamhuri, Manyerere Jackton aliwataka Serukamba na Mkurugenzi wa Idara ya Habari, MAELEZO, Hassan Abbas wasijisahau na kupitisha Muswada huo eti kwa kuwa wako serikalini, bali wajue kuwa kuna wakati watarudi na kukabiliwa na sheria hiyo.

Mwenyekiti wa TEF, Theophil Makunga alisema Muswada huo usipobadilishwa vipengele hivyo na ukapitishwa kuwa sheria, waandishi wa habari watakuwa kwenye shida kubwa kwa kuwa watakuwa wakipambana na kitu kibaya sana.

No comments: