Advertisements

Thursday, March 23, 2017

RC SHINYANGA APIGA MARUFUKU KUFANYA SHUGHULI ZA KIBINADAMU KANDO YA VYANZO VYA MAJI

 Katibu Tawala Wilaya ya Kishapu, Shadrack Kangese akisoma hotuba kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack wakati wa kilele cha maadhimisho ya Wiki ya Maji kimkoa
 Katibu Tawala Wilaya ya Kishapu, Shadrack Kangese akipanda mti wakati wa kilele cha maadhimisho ya Wiki ya Maji kimkoa.
 Katibu Tawala Wilaya ya Kishapu, Shadrack Kangese (katikati) akiongozwa na Kaimu Mhandisi wa Maji, Wilaya, Bernad Bwire (wa pili kushoto) kutembelea bwawa la maji na kupanda miti katika kilele cha Wiki ya Maji. Wengine pichani kushoto ni mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, Mohamed Mlewa (kushoto) na Kaimu Mkuu wa Idara ya Elimu Sekondari, Steven Cleophace (kulia).
 Kaimu Mhandisi wa Maji, Wilaya, Bernad Bwire (katikati) akitoa maelezo kwa Katibu Tawala Wilaya ya Kishapu, Shadrack Kangese na viongozi kuhusu mradi wa maji ya bwawa la Sekeididi.
 Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, Mohamed Mlewa akizungumza wakati wa kilele cha maadhimisho ya Wiki ya Maji kimkoa.
 Wananchi wa kijiji cha Sekeididi Kata ya Sekebugoro wakifuatilia maadhimisho ya Wiki ya Maji kimkoa yaliyofanyika kijijini hapo.
Baadhi ya wakuu wa idara katika Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu wakielekea katika eneo lililotengwa kwa ajili ya zoezi la upandaji miti.

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack ameagiza wakurugenzi wa mamlaka za Serikali za Mitaa na Maji kuhakikisha hakuna mtu anayefanya shughuli za kibinadamu kwenye vyanzo vya maji.
Telack alitoa agizo hilo juzi wilayani hapa katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Katibu Tawala Wilaya ya Kishapu, Shadrack Kangese wakati wa kilele cha maadhimisho Wiki ya Maji yaliyofanyika kijiji cha  Sekeididi.
Aliagiza wakurugenzi hao kuhakikisha vyanzo hivyo vinapandwa miti ili kutunza uoto wa asili ambao mara nyingi huathiriwa na ukame kutokana na kukosekana kwa miti.
Mkuu huyo wa mkoa aliwataka viongozi hao wasimamie utekelezaji wa sheria ya utunzaji wa mazingira ili kunusuru vyanzo vya maji, kwani Serikali inatumia fedha nyingi katika utekelezaji wa miradi ya maji.
“Utunzaji wa vyazo vya maji ni jambo muhimu katika upatikanaji wa maji na hivyo ni jukumu la kila mmoja wetu kutunza vyanzo vya maji kwa kupanda miti eneo linalozunguka vyanzo.
“Kwa mujibu wa Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004, kifungu cha 57, kifungu kidogo cha 1 kinakataza mtu yeyote kufanya shughuli za kibinadamu ndani ya mita 60 kwenye vyanzo vya maji,” alisema.
Maadhimisho hayo yaliambatana na zoezi la upandaji miti kwenye bwawa la Sekeididi ambalo litakuwa likitoa huduma ya maji kwa wananchi wa maeneo hayo.
Telack aliwataka wananachi kuiunga mkono Serikali katika jitihada zake za kuboresha huduma ya upatikanaji wa maji safi na salama katika maeneo yao.
Alisema miradi hiyo imeibuliwa na wananchi wenyewe kupitia vikao vyao na hivyo wanapaswa kuendeleza jitihada zao ili kunufaika nayo kwa kuwa wasimamizi wake.
Awali akizungumzia mradi wa ujenzi wa bwawa la maji kijijini hapo, Kaimu Mhandisi wa Maji Wilaya, Bernad Bwire alisema kuwa lina uwezo wa kuhifadhi lita milioni 119.8 za maji.
Alisema bwawa hilo linalojengwa kwa gharama ya sh. milioni 662.4 linatarajiwa kuhudumia wananchi 16,627 wa vijiji vinne vya Bugoro, Ngwashinong’ela na Mwagalankulu katika kata ya Sekebugoro.
Mhandishi Bwire alisema ili kulifanya bwawa lidumu wananchi wamejipanga kuhifadhi mazingira yanayolizunguka kwa kuzuia mifugo kuingia katika eneo la bwawa.
Aliongeza kuwa katika kipindi cha Wiki ya Maji jumla ya miti 230 imeshapandwa na kuwa wanatarajia kupanda mingine 800 zaidi katika eneo la kuzunguka bwawa hilo.

No comments: