Advertisements

Wednesday, June 7, 2017

JWTZ yatoa onyo kwa matapeli wa ajira

Jeshi la Wananchi (JWTZ) limetoa tahadhari kwa umma juu ya matapeli wanaowalaghai wananchi kwamba watawapa ajira katika jeshi hilo na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).
Akitoa tahadhari hiyo, Mkuu wa Utumishi wa JWTZ, Meja Jenerali Harrison Masebo amesema wamepokea malalamiko mengi ya wananchi kuhusu utapeli huo na kusisitiza kwamba jeshi lina utaratibu wake wa kuajiri na siyo kuwatumia watu wengine kufanya kazi hiyo.
Masebo amesema wanawatafuta watu hao kwa sababu wanalichafua jeshi kwa kujiita maofisa wa JWTZ na kujenga dhana kwa wananchi kwamba wametapeliwa na jeshi.
"Tunaomba ushirikiano wa wananchi ili tuweze kuwakamata watu hao. Mtu akikwambia anataka kukupa kazi JKT au JWTZ wewe msikilize lakini tuletee taarifa kabla hukampa chochote, sisi tutamkamata,"amesema Masebo.
Mkuu huyo wa utumishi jeshini amesema ajira zote zinazotelewa na JKT lazima zitangazwe kwenye vyombo vya habari na mchakato wake uko wazi.
Amewataka wananchi wasiwape chochote matapeli hao badala yake watoe taarifa jeshini.

No comments: