Advertisements

Tuesday, July 4, 2017

KUNASWA KWA WANAFUNZI 11 KWA SOO LA UFUSKA DAR, WAZAZI WASHTUSHWA

Tukio la Jeshi la Polisi kuwakamata watoto wa kike na kiume 11 walio chini ya miaka 18 wakifanya vitendo vya ufuska kwenye Ufukwe wa Coco jijini hapa, wazazi maeneo mbalimbali wameshitushwa na tukio hilo.

Watoto hao ambao wana umri wa miaka 15 hadi 17, wote ni wanafunzi wa shule za sekondari tatu tofauti za Temeke, walin-aswa majira ya usiku na Jeshi la Polisi Mkoa wa Kipolisi Temeke chini ya Kamanda, SACP Gilles Muroto wakiwa nusu uchi huku wakiwa wamebeba vilevi mbalimbali na ikaelezwa kuwa walikutwa wakifanya mambo yasiyofaa kufanywa na watoto huko walikokamatiwa.

Kufuatia tukio hilo Mkuu wa Wilaya wa Temeke, Felix Lyaniwa aliamuru jeshi la polisi kuwashikilia ili wafikishwe mahakamani watoto na wazazi wao kwa kosa la kuvunja maadilia ya Mtanzania, huku akiwaagiza wakuu wa shule zote kuhakikisha wanawafuatilia kwa makini wanafunzi wenye tabia za utukutu mashuleni mwao.

Wakizungumza na Gazeti la Uwazi, baadhi ya wazazi walisema kwa tukio hilo ni kama wamezibuliwa masikio na watakuwa makini katika malezi ya watoto wao kwa kuepuka kudhalilika.
“Tukio lile ni kama limenifumbua macho kwa kweli, kwa sababu ni watoto wadogo sana kukamatwa usiku na katika mazingira tatanishi ya ufuska. Wazazi tunajisahau sana katika malezi ya watoto wetu, pamoja na ugumu wa maisha lakini bado tuna wajibu wa kuhakikisha watoto wetu wanakuwa katika malezi ya kimaadili na ya kumpendeza Mungu,” alisema Justine John wa Makumbusho.

Naye mzazi wa watoto wawili mkazi wa Tegeta, Ramadhani alisema: “Kuna udhaifu mkubwa sana kwa baadhi ya wazazi, lakini kwa tukio hilo litakuwa limewafungua macho na masikio wazazi wengiki.”

Watoto wengi wamekuwa wakionekana waungwana wanapokuwa maeneo ya nyumbani kwao lakini wanapokuwa mbali, wengi wamekuwa wakijihusisha na uvutaji wa bangi, dawa za kulevya, ulevi, ngono, uporaji, usagaji na mambo mengine yasiyofaa kwenye jamii.

Imefahamika pia kwamba watoto wengi hutoka majumbani kwao wakiwa na nguo za ‘kihasarahasara’ ambazo huzitumia wakifika kwenye maeneo ya starehe hivyo wazazi wamepewa muongozo wa kuwa makini sana na watoto wao wawapo nyumbani na hata nje ya makwao ili kuepuka aibu.

“Mimi pia ni mzazi lakini ninawashauri wenzangu tuwe makini sana na watoto wetu, kila wanapotoka tujue wamekwenda wapi, na nani, kufanya nini, wakiwa wamevaaje ili kuepukana na aibu kama hizi walizopata wenzetu,” alishauri mama Zaina wa Sinza, Dar.

No comments: