Advertisements

Friday, October 20, 2017

NECTA YATANGAZA MATOKEO YA DARASA LA SABA

Baraza la Mitihani la Tanzania (Necta) limetangaza matokeo ya mtihani wa darasa la saba leo Oktoba 20,2017.
Katibu Mtendaji wa Necta, Dk Charles Msonde amesema watahiniwa 662,035 kati ya 909,950 waliofanya mtihani huo wamefaulu kwa kupata alama 100 au zaidi kati ya alama 250 wanazopaswa kupata.
Dk Msonde amesema kati ya waliofaulu, wasichana ni 341,020 ambao ni sawa na asilimia 70.93 na wavulana ni 321,015 sawa na asilimia 74.80 .
Amesema idadi ya watahiniwa waliofaulu ni sawa na asilimia 72.76.
Dk Msonde amesema mwaka 2016 watahiniwa waliofaulu walikuwa asilimia 70.36, hivyo kuna ongezeko la ufaulu kwa asilimia 2.40.
Katibu Mtendaji huyo amesema ufaulu katika masomo ya Kiswahili, Kiingereza na Hisabati umepanda kwa asilimia kati ya 4.25 na asilimia 10.05 kulinganishwa na mwaka 2016.
"Kwa masomo ya Sayansi na maarifa ya jamii ufaulu umeshuka kwa asilimia kati ya 3.56 na asilimia 13.97 kulinganisha na mwaka 2016.
"Watahiniwa wamefaulu zaidi katika somo la Kiswahili ambalo ufaulu ni asilimia 86.86 na somo walilofaulu kwa kiwango cha chini zaidi ni Kiingereza, lenye ufaulu wa asilimia 40.30," amesema Dk Msonde.
Katibu Mtendaji, Dk Msonde amezitaja shule 10 bora kitaifa kuwa ni St Peter iliyopo Kagera, St Severine (Kagera), Alliance (Mwanza), Sir John (Tanga), Palikas (Shinyanga), Mwanga (Kagera), Hazina (Dar es Salaam), St Anne Marie (Dar es Salaam), Rweikiza (Kagera) na Martin Luther (Dodoma).
Amezitaja shule 10 ambazo hazikufanya vizuri kuwa ni Nyahaa ya Singida, Bosha (Tanga), Ntalasha (Tabora), Kishangazi (Tanga), Mntamba (Singida), Ikolo (Singida), Kamwala (Songwe), Kibutuka (Lindi), Mkulumuzi (Tanga) na Kitwai A (Manyara).
Aliitaja mikoa iliyoongoza kitaifa kuwa ni Dar es Salaam, Geita, Kagera, Iringa, Kilimanjaro, Njombe, Arusha, Mwanza, Katavi na Tabora.
Dk Msonde amesema mikoa iliyofanya vibaya ni Singida, Tanga, Tabora, Songwe, Lindi na Manyara.

No comments: