Advertisements

Monday, October 16, 2017

VYAKULA UNAVYOTAKIWA KUEPUKA KULA KAMA UNATAKA KUPUNGUZA UZITO WA MWILI

Na Jumia Travel Tanzania

Leo siku ya Oktoba 16 dunia inaadhimisha Siku ya Chakula Duniani ambapo Shirika la Chakula Duniani (FAO) kila mwaka huadhimisha kwa shughuli na kauli mbiu mbalimbali. Kwa mwaka huu kauli mbiu ni ‘Badili Hali ya Uhamiaji ya Baadaye: Wekeza Katika Usalama wa Chakula na Maendeleo ya Vijijini.’ Kwa mujibu wa FAO, dunia inapitia mabadiliko kadha wa kadha kila kukicha. Watu wengi wamelazimika kuhama makazi yao kutokana na sababu tofauti kama vile kuongezeka kwa migogoro na kutokuwepo usalama wa kisiasa. Lakini njaa, umasikini, na kuongezeka kwa matukio ya hali ya hewa yanayochangiwa na mabadiliko ya hali ya hewa ni sababu zingine za muhimu zinazochangia katika kupelekea watu kuhama.   
Miongoni mwa changamoto kubwa inayowakumba watu siku za hivi karibuni ni katika upatikanaji wa chakula, matumizi yake na namna ya kudhibiti ili kutoleta athari katika mwili. Kwa kuwa leo ni maadhimisho ya ‘Siku ya Chakula Duniani,’ Jumia Travel ingependa kukushirikisha aina za vyakula vya kupunguza au kuacha kula kabisa kama unataka kupunguza uzito wa mwili wako.


Chipsi. Kwa wakazi wengi wa sehemu za mijini kama vile jiji la Dar es Salaam, chipsi ni mojawapo ya chakula kinachotumiwa na idadi kubwa ya watu. Na hii ni kutokana na upatikanaji wake kwa urahisi karibu kwenye kila maeneo wanapoishi. Kwa mujibu wa tafiti, chakula hiki kinaongeza uzito mwilini kutokana na kuwa na kalori nyingi ndani yake na ni rahisi kuzila nyingi zaidi kwa mpigo. Tafiti pia zinaendelea kwa kuelezea kuwa chipsi pengine ndiyo chakula kinachochangia kuongeza uzito kuliko chakula chochote. Hivyo basi, kwa afya yako unashauriwa kuvichemsha kwa maji na kula badala ya kukaanga.  

Vinywaji vyenye sukari nyingi. Vinywaji vinavyotengenezwa na kuongezewa sukari ili kuwa vitamu vinatajwa kuwa ni mojawawapo vyakula hatari zaidi kiafya duniani. Vinahusishwa kwa kiasi kikubwa na kuongezeka kwa uzito na vinaweza kuwa na madhara zaidi mwilini endapo vitatumiwa kwa kiasi kikubwa. Ingawa vyakula hivi huwa na kalori nyingi lakini ubongo wako hauvitambui kama ni vyakula vigumu. Kwa hiyo, kama una nia ya dhati kabisa ya kupungua uzito ni vema ukaachana na vinywaji vya aina hii.

Chokoleti. Inafahamika watu wengi hupendela chokoleti kutokana na utamu wake lakini ni hatari sana kiafya. Hutengenezwa kwa kuongezewa sukari nyingi zaidi, mafuta na unga uliosafishwa zaidi kiwandani kwa kiasi fulani. Chokoleti zina kalori nyingi huku virutubisho vikiwa ni vichache. Kipande cha kawaida cha chokoleti kina kadiriwa kuwa kalori takribani 200-300, huku vipande vikubwa zaidi vinaweza kuwa nazo nyingi zaidi. Lakini kwa bahati mbaya unaweza kukutana na chokoleti karibu kila mahala tena zikiwa zimewekwa kwa kutamanisha zaidi ili kukushawishi kununua. Inashauriwa kama unataka kula chakula kidogo cha kawaida badala yake kula kipande cha tunda au karanga angalau.

Juisi za viwandani. Juisi nyingi za matunda unazoziona madukani zinakuwa na virutubisho vidogo sana ukilinganisha na tunda halisi. Nyingi huwa zinatengenezwa viwandani na kuongezewa sukari. Kiukweli, huwa na sukari nyingi na kalori sawa na soda, tena inawezekana vikazidi. Kwa kuongezea juisi za viwandani hazina nyuzinyuzi ambazo unaweza kuzipata kwenye matunda halisi. Hivyo basi unashauriwa ni vema ukala tunda kamili badala ya juisi kwani faida zake haziwezi katu kulingana kama wengi tunavyoamini.   

Mikate, biskuti na keki. Vyakula hivi huongezewa na virutubisho vingi ambavyo havina faida kwa mwili. Tena wakati mwingine huongezewa mafuta hatarishi ambayo yanahusishwa kuwa chanzo cha magonjwa tofauti. Kwa kawaida vyakula hivi havishibishi hivyo utatamani kuvitumia zaidi na hivyo kupelekea kula sumu zaidi.

Baadhi ya vileo (hususani bia). Kwa kiasi kikubwa pombe hutuongezea kalori nyingi kuliko wanga na protini mwilini mwetu. Hata hivyo, suala la kunywa pombe na kuongezeka uzito bado halijadhibitishwa moja kwa moja. Unywaji wa pombe wa kawaida unaweza kuwa hauna matatizo na wakati mwingine huhusishwa na kupunguza uzito. Lakini kwa upande mwingine, unywaji wa kupindukia hupelekea kuongezeka kwa uzito wa mwili. Aina ya kileo unachokunywa pia ni kitu cha kuzingatiwa. Kwa mfano, unywaji wa bia unawdza kupelekea kuongezeka uzito, huku unywaji wa divai (wine) unaweza kuwa na faida kwa afya ya mwili.

Aiskrimu. Chakula hiki ni kitamu sana lakini ni hatari kwa afya ya mwili wako. Kwani kina kalori nyingi na huongezewa sukari nyingi kwenye utengenezaji wake. Matumizi kwa kiasi kidogo hayana madhara lakini ni vigumu sana kujizuia kutokutumia kiasi kikubwa kwa wakati mmoja. Unaweza kutengeneza wewe mwenyewe nyumbani ili kuweka virutubisho vingi zaidi lakini pia kujizuia kutumia nyingi zaidi, tenga kiasi kidogo na kingine kifiche ili kujizuia zaidi.  

Pizza. Chakula hiki ni maarufu sana maeneo ya mijini kutokana na upatikanaji wake wa haraka lakini sio vizuri kiafya kabisa. Huwa na kalori nyingi na kutengenezwa kwa kuongezewa virutubisho hatari kwa afya kama vile unga na nyama zinazochakatwa viwandani.

Kutokana na makala haya unaweza kuwa umegundua kwamba vyakula vingi huwa vinatengenezwa viwandani na kuwekewa kemikali nyingi ili kuongezewa ladha na kutumika kwa muda mrefu zaidi. Jumia Travel ingepependa kukushauri kula vyakula vya asili zaidi au kupika mwenyewe kwani kwa kufanya hivyo utakuwa unajitengenezea fursa ya kuepuka magonjwa mengi zaidi sasa na siku za usoni.


No comments: