Advertisements

Saturday, November 18, 2017

RPC SIMON HAULE AFUNGA MAADHIMISHO YA WIKI YA NENDA KWA USALAMA BARABARANI MKOA WA SHINYANGA MWAKA 2017

Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga ACP Simon Haule amefunga wiki ya wiki ya nenda kwa usalama barabarani mkoa wa Shinyanga yaliyoanza siku ya Jumatatu Novemba 13,2017 katika viwanja vya jeshi la Zimamoto mjini Shinyanga.


Akizungumza leo Jumamosi Novemba 18,2017 wakati wa kufunga maadhimisho hayo, yenye kauli mbiu "Zuia ajali,Tii sheria,Okoa Maisha",Kamanda Haule aliwataka watumiaji wa barabara kuzingatia alama na michoro ya barabarani na watembea kwa miguu kuhakikisha wanapokuwa barabarani wanavuka katika maeneo yanayostahili ili kupunguza ajali zisizo za lazima.


“Watembea kwa miguu hakikisheni mnavuka katika maeneo yanayotakiwa,ajali nyingi zinatokea kutokana na uzembe wa watumiaji wa barabara,na ajali zinazoongoza Shinyanga ni za pikipiki na watembea kwa miguu”,alisema.

Katika hatua nyingine aliwataka wananchi kulinda miundombinu ya barabara kwa kushirikiana na serikali na kuhakikisha wanawakata baadhi ya watu wasio waaminifu wanaoiba miundombinu ya barabara.
“Naomba tushirikiane kuwafichua na kuwakamata watu wanaoiba miundombinu ya barabara,na tukiwakamata tuwafikishe katika vyombo vya sheria”,aliongeza Haule.
Aidha alitumia fursa hiyo kuwakumbusha akina mama kukaa mkao wa kiume wanapopanda pikipiki ama baiskeli badala ya kukaa upande upande ili kupunguza ajali za barabarani.
Naye Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani mkoa wa Shinyanga,Anthony Masanzu alisema katika wiki hiyo ya nenda kwa usalama,wamefanikiwa kutoa elimu ya usalama barabarani kwa waendesha bodaboda 184.
Alisema mbali na kutoa elimu kwa waendesha bodaboda na wananchi waliotembelea mabanda ya usalama barabarani pia walitembelea shule mbalimbali mjini Shinyanga ambazo zipo karibu na barabara.
“Tumetumia wiki hii kutoa elimu ya usalama barabarani kwa makundi mbalimbali ya watumiaji wa barabara ili kuhakikisha kuwa tunazuia ajali na kuokoa maisha yao”,aliongeza Masanzu.
Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga ACP Simon Haule akizungumza wakati wa kufunga wiki ya nenda kwa usalama barabarani mkoa wa Shinyanga mwaka 2017-Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog

No comments: