Advertisements

Friday, June 8, 2018

Menejimenti ya BOT yahojiwa na PAC, Ripoti Kukabidhiwa kwa Spika Jumatatu

Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) imemaliza kazi ya kuwahoji Bodi na Menejimenti ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) juu ya tuhuma zinazowakabili za kutumia bima binafsi ya afya badala ya Bima ya Taifa ya Afya (NHIF).

Bodi na Menejimenti ya BoT wamefika mbele ya kamati ya PAC kujibu tuhuma hizo ambazo ziliibuliwa bungeni Juni 4 na Mbunge wa Ulanga (CCM), Goodluck Mlinga.

Mwenyekiti wa PAC, Naghenjwa Kaboyoka amesema, wameshazungumza na Bodi na Menejimenti ya BoT pamoja na NHIF.

“Kwa kuwa ni agizo la Mheshimiwa Spika (Job Ndugai), tunakamilisha kuandaa taarifa na Jumatatu (Juni 11, 2018) tutamkabidhi,” ameongeza Kaboyoka ambaye pia ni Mbunge wa Same Mashariki (Chadema).

Bodi na Menejimenti ya BoT ikiongozwa na Gavana wa Benki hiyo, Profesa Florens Luoga pia wamehudhuria kikao cha 47, Mkutano wa 11 leo na kutambulishwa na Mwenyekiti wa Bunge, Andrew Chenge.

No comments: