Advertisements

Wednesday, August 29, 2012

POLICE WAZUIA MIKUTANO YA CHADEMA IRINGA

 POLISI WAKIWA ENEO  LA KIWANJA AMBAKO ILITEGEMEWA KUFANYIAKA MKUTANO  WA CHADEMA
 VUTA nikuvute baina ya Polisi na Chadema imehamia Iringa, ambako jeshi hilo limezuia maandamano na mikutano yote ya chama hicho iliyokuwa imepangwa kufanyika kwa siku nane kuanzia jana.
Amri hiyo ya polisi imekuja siku moja baada ya kutokea vurugu kubwa mjini Morogoro, baina ya wafuasi wa chama hicho na polisi na kusababisha kifo cha mtu mmoja na wawili kujeruhiwa.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Michael Kamhanda alisema jana kuwa wameamua kuzuia maandamano na mikutano ya Chadema iliyopangwa kuanza jana kutokana na Sensa ya Watu na Makazi.
“Kutokana na hali halisi ya Sensa, tumeamua kuzuia maandamano na mikutano yote ya vyama vya kisiasa mkoani Iringa wakiwamo hawa watu wa Chadema,” alisema.
Alisema kabla ya kuwazuia, walikutana na viongozi wa chama hicho Wilaya ya Iringa na kuwataka wazuie mikutano yao, jambo ambalo alisema walilikubali kwa ‘mbinde’.

Dk Slaa: Wametuomba
Awali, akiwa Mjini Morogoro, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa alisema polisi wamekiomba chama hicho kusitisha maandamano na mikutano yake iliyopangwa kufanyika mkoani Iringa kupisha Sensa ya Watu na Makazi.
Alisema Chadema imekubali ombi hilo lililotolewa na Mkuu wa Polisi, IGP Said Mwema hivyo kuamua kusitisha mkutano wake uliopangwa kufanyika katika Viwanja vya Mwembetogwa, Iringa jana.
“Juzi Agosti 27, 1:00 usiku tulipata barua kutoka Jeshi la Polisi Iringa iliyokubali Chadema kufanya maandamano wakiwa ndani ya magari na si matembezi ya miguu, lakini baadaye saa 3:00 usiku, tulipigiwa simu na OCD wa Iringa akitujulisha kuwa maandamano yao yamebatilishwa na kutengua mambo yote tuliyoafikiana mwanzo,” alisema Dk Slaa na kuongeza:
“Asubuhi ya leo (jana) tulipigiwa simu na RPC (wa Iringa) na kudai kuwa wanataka kuonana na viongozi wa Chadema, huku wakiwa na hoja kuwa tuahirishe kufanya mkutano kutokana na Sensa.
Hoja nyingine ambayo mimi naona ni ya upuuzi ni ile ya kusema kwamba wananchi wa Iringa watakuwa wameathirika na kifo cha kijana aliyekufa Morogoro,” alisema Dk Slaa.
Alisema baada ya kutokubaliana na hoja hizo, alipigiwa simu na IGP Mwema akimwomba asitishe mkutano na maandamano ya mkoani Iringa kwa kuwa hiyo ni amri kwa vyama vyote vya siasa na si Chadema pekee.
“Nimeongea na IGP leo kwa dakika zaidi ya 40 akisema Dk Slaa sijawahi kukuomba hata siku moja, naomba nikuombe na usinikatalie kati ya siku nne hadi tano kuanzia sasa tumezuia vyama vya siasa kufanya mikutano ya hadhara kutokana na kuwapo kwa Sensa naomba tuelewane,” alisema Dk Slaa akimnukuu IGP Mwema.

No comments: