Tuesday, March 12, 2013

Mapya yaelezwa mauaji ya kinyama yalivyofanywa

Mtuhumiwa wa mauaji ya watu watatu na kuwajeruhi watu wanane kwa kuwacharanga mapanga Starnford Richard (30) akiwa chini ya ulinzi wa polisi baada ya kutolewa hospitali ya mkoa wa Kigoma ya Maweni jana.

Wakati Jeshi la Polisi mkoani Kigoma leo linatarajia kumfikisha mahakamani mkazi wa Kijiji cha Bitale, wilayani Kigoma, Stanford Richard (30), kwa tuhuma za kuwaua watu watatu kwa kuwacharanga mapanga na kuwajeruhi wengine wanane, ndugu na jamaa zake wamesimulia kilichotokea.

Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai wa Mkoa wa Kigoma, Dismas Kisusi, alisema leo mtuhumiwa huyo anayedaiwa kuwa na ugonjwa wa akili atafikishwa mahakamani na baada ya hapo wataomba kibali cha Mahakama kumpeleka Stanford hospitali kumfanyia uchunguzi kubaini kama ana ugonjwa wa akili ama la.Jana polisi walimpeleka mtuhumiwa huyo katika Hospitali ya Mkoa wa Kigoma Maweni kutibiwa majeraha aliyoyapata kutokana na kipigo cha wananchi baada kuua na kujeruhi.

MAMA MZAZI ASIMULIA
Mama mzazi wa mtuhumiwa, Ritha James (55), akizungumza na NIPASHE jana akiwa amelazwa katika Hospitali ya Maweni wodi namba tano alisema: “Mtoto wangu alimaliza kidato cha nne katika Shule ya Sekondari ya Mwandiga mjini Kigoma kisha mwaka 2002 alikwenda Tegeta, Dar es Salaam ndipo alipopata ugonjwa wa akili.

Nikamtuma mtoto wangu mkubwa Manase Richard kwenda kumchukua Dar es Salaam, alipokuja tulimpeleka kwa waganga na hali yake ikawa nzuri.”

Ritha alisema baada ya hapo mtuhumiwa huyo alikuwa anafanya biashara ya kuuza bidhaa katika kibanda kimojawapo kwenye soko la kijiji cha Bitale na kwamba siku ya tukio Machi 8, mwaka huu saa 2:30 usiku alimkata kwa mapanga mpangaji wao, Doto Issa kichwani.

“Ndipo mimi nikaenda kumsaidia na nikakatwa kichwani kwa panga, mume wangu Richard Manase naye akakatwa kichwani kisha mama mkwe wangu Rudia Mbaga akakatwa panga na kufariki dunia,” alieleza.

Alisema baada ya kushambuliwa na kujeruhiwa, wasamaria wema waliwachukua na kuwapeleka katika Hospitali ya Maweni ambako amelazwa wodi namba tano ma mumewe wodi namba saba.

KAKA WA MTUHUMIWA AELEZA
Kaka wa mtuhumiwa, Manase Richard (38), akizungumza na NIPASHE jana katika kijiji cha Bitale, alisema: “Mimi nilienda kumchukua mdogo wangu Dar es Salaam eneo la Tegeta ili nimlete huku Bitale kwa sababu alikuwa amechanganyikiwa, tulipofika huku nyumbani tulimpeleka kwa waganga akapona, akawa anafanya biashara yake kwenye kibanda cha duka sokoni Bitale.”

Richard alisema siku ya tukio tangu asubuhi mtuhumiwa alikuwa amelala, lakini ilipofika saa 2:30 usiku alichukua panga na nondo na kuanza kumkata kichwani mpangaji wao, Doto Issa na kwamba mama na baba yao walienda kumsaidia ndipo nao wakakatwa kwa panga na kupigwa nondo kichwani.

Alisema mtuhumiwa huyo alikuwa anavizia kwa sababu ya giza na kwamba ndiyo maana aliwaua watu watatu na kuwajeruhi wanane.

DIWANI WA AZUNGUMZA
Diwani wa kata ya Bitale, John Bwami, aliieleza NIPASHE jana kuwa tukio hilo limemshitua sana na limeleta majonzi na masikitiko makubwa.

“Naomba wananchi watulie, tusiwe na mtu wa kumlaumu, tuwe na subira na kila mtu kwa imani yake tuwaombee majeruhi ili wapone na kuendelea na kazi zao kama kawaida,” alisema Bwami wakati akizungumza kijijini hapo na kuongeza:

“Wananchi wawe makini, wakiona mtu yeyote ambaye ana matatizo ya akili watoe taarifa kwa viongozi wa kijiji ili lisitokee tena tukio kama la sasa.”

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Katubuka, Moses Bilantanye ambaye mama yake mzazi, Ezema Lazaro (70) aliuawa na mtuhumiwa kwa kukatwakatwa mapanga, alisema: “Mimi namuachia Mungu, lakini kila mwananchi akiona mtu mwenye matatizo ya akili, atoe taarifa kabla ya kutokea maafa kama haya, nimemzika mama yangu bila kutarajia kuwa atakufa.”

Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Dk. Leonard Subi, alisema kuwa majeruhi wote waliolazwa katika Hospitali ya Maweni hali zao zinaendelea vizuri na kwamba wote wanaongea tofauti na siku waliyofikishwa hospitalini.

Alisema kuwa wanaendelea na matibabu katika wodi namba tano na saba.
Waliouawa na mtuhumiwa huyo Machi 8, mwaka huu ni Rudia Richard (70), Ezema Razalo (65) na Sebastiani Julius (22), wote wakazi wa Kijiji cha Bitale.

Waliyojeruhiwa ni Pendo Jumbe (35), Jumbe Budio (50), Richard Manase (60), Lith James (55), Shukrani Manase (30), Doto Issa (24) , Remmy Kagiye (8) na Seraphina Mayage (65), wakazi wa kijiji kicho na kwamba walipata majeraha makubwa na hali zao siyo za kuridhisha wakiwa wamelazwa katika Hospitali ya Mkoa wa Kigoma Maweni

Kisusi hakueleza sababu za mauaji hayo, lakini alisema kuwa kuna taarifa kwamba mtuhumiwa ni mgonjwa wa akili.

Miili ya marehemu ilizikwa juzi katika maeneo tofauti.

CHANZO: NIPASHE

No comments: