Saturday, January 9, 2016

BALOZI SEIF AWEKA JIWE LA MSINGI UJENZI WA BARABARA YA KILOMITA 35 ITAKAYOANZIA KIJIJI CHA OLE

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif AliIddi akikata utepe kuashiria akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa Bara bara ya Kilomita 35 itakayoanzia katika Kijiji cha Ole kupitia Vitongoji,Mfikiwa na kumalizikia katika Kijiji cha Kengeja Mkoa wa Kusini Pemba. Wa kwanza kutoka Kushoto ni Afrisa Mdhamini Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano Pemba Nd.Hamad Ahmed Baucha na nyuma yake ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Nd.Tahir Abdullah.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais waZanzibar Mh. Moh’d Aboud Moh’d wa kwanza kutoka kulia akibadilishana mawazo na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mh. Ali Juma Shamuhuni kwenye sherehe ya uwekaji wa jiwe la msingi la Bara bara ya Ole hadi Kengeja. Kulia ya Waziri Shamuhuni ni Mkuu wa Wizaya ya Chake chake Bibi Hanuna Ibrahim Masoud na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kaskazini Pemba Mzee Mberwa Hamad Mberwa.

Baadhi ya Wafanyakazi wa Wizara ya Miundombinu naMawasiliano pamoja na Wananchi waliohudhuria uwekaji wa jiwe la msingi la Bara bara ya Ole hadi Kengeja ikiwa ni shamra shamra za maadhimisho ya sherehe za Kutimia miaka 52 ya Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964, 

Balozi Seif Ali Iddi akizungumza na Wananchi pamojana Watendaji wa Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano mara baada ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Bara bara ya Ole hadi Kengeja. 


 Kijana Halima Juma akifanya manjonjo yake wakatiakisoma utenzi maalum katika hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa bara bara ya Ole hadi Kengeja ambapo Mgeni rasmi alikuwa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi. Picha na –OMPR – ZNZ.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema kwamba azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuendelea na matengenezo ya bara bara pamoja na ujenzi wa nyengine mpya umelenga kuimarisha sekya ya usafiri wan chi kavu.

Alisema kuundwa kwa mfuko wa bara bara ni hatua iliyokusudiwa kusimamia vyema Bara bara zinazojengwa katika maeneo mbali mbali Nchini chini ya Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano ili zitoe huduma bora ya mawasiliano.

Balozi Seif Ali Iddi alieleza hayo wakati akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa Bara bara ya Kilomita 35 itakayoanzia katika Kijiji cha Ole, Vitongoji, Mfikiwa na kumalizikia katika Kijiji cha Kengeja.

Alisema maendeleo makubwa katika sekta ya mawasiliano yamepatikana hasa katika ujenzi wa bara bara Tano katika Mkoa wa Kaskazini Pemba zilizopata ufadhili wa Mfuko wa Milenia wa Marekani { MCC } na Bra bara Tano za Vijijini ndani ya Mkoa wa Kusini Pemba zilizofadhiliwa na Shirika la Maendeleo Norway (Norad ).

Aliwaomba Wananchi wote Nchini kuwa walinzi wa miundombinu inayojengwa na kuimarishwa na Serikali Kuu ili ichangie kwa kiasi kikubwa kupunguza umaskini kwa vile utatoa fursa kwa Wananchi hao kuitumia miundo mbinu hiyo kwa faida yao.
Balozi Seif alionyesha masikitiko yake kutokana na tabia kwa baadhi ya watu kuharibu kwa makusudi miundombinu ya Bara bara, majengo ya Skuli, Hospitali, huduma za Umeme pamoja na Maji.
Alionya kwamba katika kuilinda miundombinu hiyo inayompasa kila mwananchi awe mlinzi Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar haitomstahamilia Mtu au kikundi chochote kitakachojaribu kurejesha nyuma maendeleo ya Taifa kwa kuharifu rasilmali hizo.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwanasihi Wananchi kujiepusha na tabia ya kujenga katika maeneo ya hifadhi ya Bara bara ambayo Serikali wakati wowote huamua kuyatumia kwa upanuzi wa Bara bara kulingana na mahitaji ya usafiri wa kisasa sambamba na mabadiliko ya harakati za Kitaifa.
Alisema wapo watu wenye fikra na hamu ya kupenda kujenga kando kando ya bara bara ndani ya Mita 15 maeneo ambayo Serikali Kuu haitakuwa na haki wala wajibu wa kulipa fidia kwa watu hao waliokiuka sheria na taratibu za bara bara.
Aliwaonya watendaji wa Serikali kuwa makini katika kukabiliana na watu wanaoamua kujenga majengo ya kudumu katika maeneo yasiyostahiki wala kuruhusiwa.
Alisema mfumo wa watendaji hao kusubiri watu wafanye makosa ndipo wachukuwe hatua dhidi ya wahusika hao ikiwemo kuwavunjia majengo yao waelewe kwamba wanakaribisha hasara inayoweza kuepukwa mapema kwa
pande zote husika.

Mapema akitoa Taarifa ya kitaalamu ya ujenzi wa Bara bara hiyo ya Ole Kengeja Katibu Mkuu Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano Zanzibar Dr. Juma Malik Akil alisema ujenzi huo unatarajiwa kuchukuwa kipindi cha
miezi sita ambapo kwa sasa tayari wahandisi wamefikisha kilomita Tano.

Dr. Malik alisema hatua ya kilomita 11 zilizoanzia Ole zifafikia katika Kijiji cha Mfikiwa chini ya makandarasi wa Idara ya Utunzaji na utengenezaji wa Bara bara Zanzibar {UUB }.
Alisema Bara bara hiyo inayojengwa kwa kiwango cha lami ikiwa na Madaraja 13 na uwezo wa kuhimili magari zaidi ya Tani Kumi inafadhiliwa na mfuko wa Kimataifa Mafuta {OPEC }.
Katibu Mkuu huyo wa Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano Zanzibar alifahamisha kwamba ukanda wa Mashariki ya Kisiwa cha Pemba unatarajiwa kukomboka kutokana na ujenzi wa bara bara hiyo itakayorahisisha usafiri.
Aliushukuru mfuko wa Kimataifa wa Mafuta { Opec } kwa kugharamia ujenzi wa bara bara hiyo unaokadiriwa kufikia Dola za Kimarekani Milioni Kumi na Mbili kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba Mh. Mwanajuma Majid alisema Wananchi wa Kisiwa cha Pemba nama wajibu wa kuishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa jitihada zake zinaziendelea kukwamua kero zinazowakabili Wananchi ikiwemo miundombinu ya bara bara, umeme, huduma za Maji pamoja na afya.
Mh. Mwanajuma aliitanabahisha jamii kwamba wakati umefika kwao
kujishughulisha na kazi za maendeleo badala ya ile Tabia ya baadhi ya watu kukaa vijiweni wakaendelea kudanganyana.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

No comments: