Advertisements

Thursday, June 22, 2017

SERIKALI KUENDELEA KUSAIDIA WAKIMBIZI

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ramadhani Mwinyi, akizungumza na waandishi wa habari wakati wa Siku ya Maadhimisho ya Wakimbizi Duniani iliyofanyika katika ukumbi wa Little Theatre, jijini Dar es Salaam.Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
Mratibu wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa (UN) nchini Tanzania, Alvaro Rodriguez, akizungumza wakati wa Siku ya Maadhimisho ya Wakimbizi Duniani iliyofanyika katika ukumbi wa Little Theatre jijini Dar es Salaam.
Wasanii ambao ni wakimbizi walioko katika kambi ya Nyarugusu mkoani Kigoma, wakiburudisha wageni waliohudhuria Siku ya Maadhimisho ya Wakimbizi Duniani iliyofanyika katika ukumbi wa Little Theatre jijini Dar es Salaam.
Wasanii wa kundi la Mpoto Theatre, wakiigiza igizo katika Siku ya Maadhimisho ya Wakimibizi Duniani,igizo hilo lilihusu mauaji yanayotokea nchi mbalimbali zilizoko kwenye vita ambapo hupelekea wananchi wake kukimbilia nchi nyingine na kuomba hifadhi ya ukimbizi.Maadhimisho hayo yamefanyika katika ukumbi wa Little Theatre, jijini Dar es Salaam.
Wasanii wa kundi la Mpoto Theatre, wakiigiza igizo katika Siku ya Maadhimisho ya Wakimibizi Duniani,igizo hilo lilihusu mauaji yanayotokea nchi mbalimbali zilizoko kwenye vita ambapo hupelekea wananchi wake kukimbilia nchi nyingine na kuomba hifadhi ya ukimbizi.Maadhimisho hayo yamefanyika katika ukumbi wa Little Theatre, jijini Dar es Salaam. 

Na Abubakari Akida

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ramadhani Mwinyi, amesema Serikali itaendelea kutoa huduma kwa wakimbizi ikishirikiana na mashirika mbalimbali ya ndani na nje ya nchi, huku akiziomba nchi zenye machafuko kukaa na kutatua changamoto zinazopelekea watu kukimbia nchi zao.

Akizungumza wakati wa kuadhimisha Siku ya Wakimbizi Duniani, iliyofanyika katika ukumbi wa Little Theatre jijini Dar es Salaam Balozi Mwinyi alisema Serikali ya Tanzania imekuwa ikisaidia masuala ya wakimbizi kutoka awamu ya kwanza ya Muasisi wa Taifa na Rais wa Kwanza, Mwalimu Julius Nyerere, ikiwepo kuwapa huduma za afya na elimu ili waweze kutimiza ndoto zao walizokuwa nazo kabla ya kuzikimbia nchi zao na kwamba ikiwa leo tunaadhimisha siku ya wakimbizi duniani lazima wote tudhamirie kumaliza tatizo hili.

“Tuunge nguvu ya pamoja kuhakikisha tunamaliza migogoro kupitia njia ya mazungumzo ili tuweze kumaliza tatizo la wakimbizi duniani, na tushirikiane nan chi zinazohifadhi wakimbizi, mashirika ya kimataifa tukijua jukumu la kutatua changamoto hii ni letu,” alisema Balozi Mwinyi

Akizungumza kwenye maadhimisho hayo, Mratibu wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa (UN) nchini Tanzania, Alvaro Rodriguez, alisema Umoja wa Mataifa kupitia Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi Duniani(UNHCR) limekuja na mkakati maalumu wa kuwahudumia wakimbizi nan chi zinazohifadhi wakimbizi (CRRF),lengo ikiwa ni kukabiliana na changamoto za kimaendeleo zinazowakabili wakimbizi katika makambi mbalimbali.

Naye Mwakilishi wa UNHCR Tanzania,Chansa Kapaya alisema shirika lake litaendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kuhakikisha wakimbizi wanaendelea kupokea misaada muhimu ya kibinadamu,katika mazingira ambayo yanawaruhusu kuishi kwa usalama na hadhi.

Tarehe 20 mwezi Juni dunia inaazimisha Siku ya Wakimbizi Duniani huku ikikadiriwa kila baada ya sekunde ishirini mtu mmoja hukimbia nchi yake na kuacha familia, nyumba na mali akikimbia machafuko, migogoro na aina mbalimbali za uhalifu kwa binadamu na kundi linaloathirika zaidi ni watoto wadogo wanaokadiriwa kuwa wengi katika idadi ya jumla ya 65.6milioni ya wakimbizi duniani.

IMEANDALIWA NA KITENGO CHA MAWASILIANO SERIKALINI-WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI


No comments: