Advertisements

Tuesday, April 20, 2021

WAZIRI DKT. DAMAS NDUMBARO: HATUWEZI KUWAUA NYANI WANATULETEA DOLA

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Damas Ndumbaro ( wa kwanza kushoto) akiwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja wakizungumza na baadhi ya Watumishi wa Hifadhi ya Taifa ya Kilimanjaro mara baada ya kufanya mkutano wa hadhara na Wananchi wa kata ya Mashati iiliyopo katika wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro ambapo Waziri Dkt. Ndumbaro ameagiza nyani hao wanaovamia makazi ya watu wahamishiwe katika Hifadhi zilizo mbali na makazi ya Watu. Watatu kulia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Allan Kijazi
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Damas Ndumbaro akizungumza na baadhi ya Watumishi wa Hifadhi ya Taifa ya Kilimanjaro mara baada ya kufanya mkutano wa hadhara na Wananchi wa kata ya Mashati iliyopo katika wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro ambapo Waziri Dkt. Ndumbaro ameagiza nyani hao wanaovamia makazi ya watu wahamishiwe katika Hifadhi zilizo mbali na makazi ya Watu. Watatu kulia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Allan Kijazi
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Damas Ndumbaro akihutubia mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kata ya Mashati iliyopo katika wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro ambapo amewahakikishia Wananchi hao wanaolalamikia Nyani na Tumbili kuvamia makazi yao kuwa watahamishiwa katika Hifadhi zilizo mbali na makazi ya Watu.


Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Damas Ndumbaro amekataa ombi la Wakazi wa Rombo la kutaka kuwaua nyani na tumbili wanaodaiwa kuvamia makazi yao na kuharibu mazao kwani wanaleta fedha (dola)

Baadala yake Waziri Ndumbaro amemuagiza Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori, Dkt. Maurus Msuha kwa kushirikiana na Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori (TAWIRI) pamoja na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori (TAWA) kuwahamisha nyani hao kwa kuwapeleka katika Hifadhi zilizo mbali na makazi ya Watu.

Waziri Ndumbaro ametoa agizo hilo jana wilayani Rombo mkoani Kilimanjaro baada ya kupata malalamiko hayo kutoka kwa Wananchi,

Amefafanua kuwa Wizara haiwezi kuwaua nyani hao kwa kuwa nyani na tumbili ni moja ya vivutio vya Utalii vinavyotuletea pesa nyingi nchini kwa ajili ya maendeleo ya Taifa.

Aidha, Dkt. Ndumbaro ameiagiza Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori (TAWIRI) kuanza kufanya utafiti wa kuwapeleka nyani hao katika mazingira ambayo yatakuwa sawa na ya Rombo ili wasiweze kupata shida yoyote kutokana na kubadailisha mazingira.

Nyani hao wanadaiwa kuvamia makazi na kuanza kung’anganiana chakula pamoja na kudaiwa kuwachukua Watoto wadogo wa Binadamu na kuanza kukimbia nao porini ambako wakati mwingine huwajeruhi.

Awali Mbunge wa Rombo ambaye pia ni Waziri wa Maliasili na Utalii, Prof. Adolf Mkenda alisema licha ya nyani hao kuwasumbua Wapiga kura wake lakini Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Hifadhi ya Taifa ya Kilimanjaro imekuwa ikifanya jitihada ya kuwaondoa nyani hao.

Hata hivyo, Prof, Mkenda ameishukuru Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Taasisi zake jinsi inavyowasaidia Wananchi wa Rombo katika maendeleo kwa kuwajengea shule pamoja na Zahanati.

Kwa upande wake Diwani wa Katangara Mrere, Mallel Venance amesema nyani hao wamekuwa tatizo sio katika kata yake tu bali ni Wilaya nzima

”Wanakuja katika makazi yetu wakiwa katika makundi kati ya 40 na 100 na katika baadhi ya vijiji wamekuwa wakiharibu mazao hali inayopelekea sisi kama wazazi kushindwa kuchangia chakula katika shule ambako watoto wetu wanasoma, Tukuomba Mhe. waziri tusaidie tunakuwa masikini kwa ajili ya nyani hawa.

No comments: