Friday, September 20, 2024

HAFLA YA UFUNGUZI WA TAMASHA LA UTAMADUNI WA MZANZIBAR


Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo itaendelea kuweka Mazingira bora ya kuendeleza sanaa na utamaduni wa Mzanzibari nchini kwa maslahi mapana ya vizazi vya sasa na baadae.
Hayo yamesemwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwa niaba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dkt Hussein Mwinyi katika hafla ya ufunguzi wa Tamasha la ishirini na Tisa ( 29 ) la Utamaduni wa Mzanzibari lililofanyika katika uwanja wa Misuka Mahonda Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Amesema Serikali tayari imeanza ujenzi wa nyumba ya Sanaa Mwanakwerekwe kwa lengo la kuviendeleza vipaji vya wasanii na wajasiriamali wanatengeneza bidhaa za utamaduni ambapo litakapomalizika litatumika kwa kufundishia sanaa mbali mbali na vitu vya utamaduni ambavyo vitasaidia kuitangaza Zanzibar nje ya nchi sambamba na kutoa fursa kwa wahitimu kuweza kujiajiri wenyewe.
Mhe. Hemed amesema Sekta ya Utalii inaendelea kukuwa kwa kasi kubwa visiwani Zanzibar na kutoa nafasi kwa Wazanzibari kuzitumia bidhaa za kiutamaduni na vyakula vya asili ambavyo vinawavutia watalii wengi wanaongia na kutoka Zanzibar na kuchangia kuongezeka kipato kwa mtu mmoja mmoja Nchi kwa ujumla.

Aidha Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ameielekeza Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kuwaandaa mapema walimu wenye sifa na uwezo ambao watakaoutumia kuwafundisha vijana na kuweza kutambulika duniani kote paamoja na kuweza kuajiriwa katika Mahoteli, Makampuni binafsi na Serikalini.

Sambamaba na hayo Mhe. Hemed amewahakikishia wazanzibari kuwa Serikali itaendelea kutoa kila aina ya ushirikiano ambao utahitajika katika kufanikisha maadhimisho ya Tamasha la Utamaduni wa Mzanzibari na matamasha mengine ili kuenzi na kudumisha fikra na falsafa za waasisi wa taifa hili.

Nae waziri wa Habari, Vijana,Utamaduni na Michezo Mhe.Tabia Maulid Mwita amesema Wizara ya Habari kupitia Idara ya Utamaduni na Sanaa imekuwa ikitoa elimu juu ya kulinda Utamaduni wa Mzanzibari kupitia TV, Radio na mitandao ya kijamii kwa lengo la kuhakikisha Mila, Silka na utamaduni wa Mzanzibari unaendelea kulindwa na kudumishwa vizazi na vizazi.

Aidha Mhe. Tabia amesema Wizara ya Habari haitasita kuwachukulia hatua wale wote watakaobainika kutokulinda na kuvunja Utamaduni za Mzanzibari ambao umekuwa ukiitangaza Zanzibar kupitia sanaa mbali mbali .

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kaskazini "B" Ndugu Hamid Seif Said amesema Mkoa wa Kaskazini Unguja umetekeleza utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi Mapinduzi kwa zaidi ya asilimia mia kwa kujengwa miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwemo Afya, Elimu, miundombinu ya barabara na masoko ya kisasa.

Mhe. Hamid amesema Tamasha la Utamaduni wa Mzanzibari linatoa somo na fundisho kwa vizazi vya sasa juu ya kutunza na kudumisha Utamaduni, Mila na Silka za Mzanzibari kwa faida ya Taifa.

Mapema Makamu wa pili wa Rais wa Zanzibar alipokea maandamano ya wasaniii mbali mbali sambamba na kukagua mabanda ya mauonesho ya wasanii na wajasiriamali waliofika katika ufunguzi wa tamasha hilo.

Imetolewa na kitengo cha Habari ( 0MPR)

No comments: